RSS

Je, Tukusanyike Siku Gani Kati ya Jumamosi na Jumapili?

                    JE, TUKUSANYIKE  SIKU GANI  KATI  YA JUMAMOSI  AU JUMAPILI?

Watu wengi hujiuliza juu ya ‘sabato’ – Je, tukusanyike siku gani kati ya jumamosi au jumapili? Sawasawa na Agano Jipya, jumapili inaitwa ‘siku ya kwanza ya juma’ na inafuata ‘Sabato’, yaani, ‘jumamosi’.

“Hata sabato ilipokwisha, kupambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi.” (Mathayo 28:1). “Naye alipofufuka alfajiri siku ya kwanza ya juma…”. (Marko 16:9).

Hii ‘siku ya kwanza ya juma’ ndiyo siku ambayo Bwana Yesu alifufuka kutoka wafu, ingawa ni wazi kuwa Wakristo walikuwa na desturi au walianzisha desturi ya kukusanyika jumapili, yaani, ‘siku ya kwanza ya juma’. Maneno haya yanadhibitishwa na mistari hii, “Hata siku ya kwanza ya juma, tulipokuwa tumekutana ili kuumega mkate, Paulo akawahutubu…” (Matendo 20:7). “Siku ya kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake, kwa kadiri ya kufanikiwa kwake; ili kwamba michango isifanyike hapo nitakapokuja…” (1 Wakor.16:2).

Hata hivyo, hakuna agizo katika Agano Jipya, kwamba lazima tukusanyike jumapili, lakini tunao mfano wa desturi ya Wakristo wa wakati wa mitume, na desturi hiyo inaendelea mpaka sasa. Desturi hiyo haikuanza tu karne ya tatu baada ya kufa na kufufuka kwa Yesu, bali ilikuwa desturi ya waumini kuanzia mwanzo wa kanisa la Bwana! Katika Agano Jipya hamna mstari hata mmoja usemao wakristo walikusanya siku ya sabato au ilikuwa desturi yao au wala sheria ya wakristo kufanya hivyo! 

Kwa kweli ni jambo la kushangaza kwa sababu wengine wanadai kuwa tungekusanyika ‘jumapili’ – kwa Kiingereza ‘Sunday’ – ina maana tunaabudu sanamu, kwa sababu wanasema ‘Sunday’ inamaanisha siku ya ‘jua’! (sun=jua; day=siku). Warumi waliiita siku hiyo kwa ‘kuliheshimu’ jua. Kama tulivyoona, wakristo wa wakati wa mitume walikusanyika jumapili kabla ya jina ‘Sunday’ halijatokea! Zaidi ya hayo watu wa mataifa pia waliita majina ya siku kwa kadiri walivyopenda. Lakini ukweli uko wazi kabisa kuwa jambo hili haliwahusu wakristo wala imani yao! Kwa Kiingereza Jumamosi inaitwa ‘Saturday’ ambayo inatokana na Warumi ambao waliiita siku hiyo ‘Siku ya sayari Zohali’ (dies Saturni) kwa sababu Warumi waliheshimu sayari Zohali. Kwa hiyo, ina maana wasabato wanaabudu sayari Zohali? Je, wasabato wanakosa kwa kuabudu sanamu? Ni jambo la kushangaa kwa sababu watu wanajadiliana mambo yasiyo na maana wala msingi wowote, kwa maneno tu yasiyo na mantiki yoyote.

Lengo la somo hili ni kuonyesha hamna sheria katika Agano Jipya ambayo inatufundisha lazima tukusanye jumamosi. Kufanya hivyo ni kosa kubwa na udanganyifu. Lengo la somo hili siyo kutufundisha lazima tukusanyike jumapili. Nilinukulu mistari kuonyesha ilikuwa desturi ya wakristo kusanyika hasa jumapili. Lakini siyo sheria. Mwanzoni wakristo walikusanyika hata kila siku! Matendo ya Mitume 2:46. Ya mwisho, lengo la somo hili ni kuonyesha na kueleza tabia ya wokovu wetu ndani ya Kristo Yesu na vipi fundisho lile la kushika sabato linavyopinga lengo la Mungu kupitia Mwanawe. Ni wazi kumpenda Mungu, kumwamini, kumtii na kumabudu ni jambo la kila siku, kila wakati na kila nafasi – siyo la jumapili tu!

                                                      —————————————

Wayahudi walikwenda/ingia ndani ya sinagogi – Jumamosi (Sabato), na Bwana Yesu alizifuata desturi hizo ili awafundishe Wayahudi mpaka kifo chake msalabani. Na tukumbuke kuwa, sinagogi za Wayahudi ni tofauti kabisa na kanisa la Bwana Yesu (lililoanzishwa baada ya kufufuka kwake) kama tunavyoweza kusoma katika kitabu cha Matendo ya Mitume. Kwa matendo yake duniani Bwana Yesu hakuvunja sheria ya Musa. Kwa mfano, baada ya kumtakasa mtu yule aliyejaa ukoma, Yesu alimwambia, “Asimwambie mtu, ila, Nenda ukajionyeshe kwa kuhani; ukatoe kwa ajili ya kutakasika kwako kama Musa alivyoamuru, iwe ushuhuda kwao.” (Luka 5:14). Hayo ni maneno ya Bwana Yesu. Sasa, je, unaamini kama mtu au muumini akiponywa ukoma siku hizi ni lazima amtafute kuhani na kutoa sadaka kwa ajili ya kutakasika kwake kama Musa alivyoamuru?  Jibu ni hapana! Ni wazi kuwa Yesu aliifuata sheria ya Musa mpaka kufa kwake, na kama tumeelewa hapo, hiyo haimaanishi kwamba iliwabidi waumini wa kanisa la Kristo baada ya kifo cha Yesu waendelee kushika torati!

Lakini baada ya Yesu kumwaga damu yake pale msalabani, yote yalibadilishwa! Kwa mfano, mara moja “Pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini” (Marko 15:38). Je, nani anayetaka kulishona pazia lile, na kuliweka tena hekaluni – kwa sababu hamna pazia tena, wala hekalu la kidunia!  Kabla ya kifo cha Yesu msalabani watu wa Mungu walikuwa hawawezi kuingia katika hema/hekalu – pale Mungu alipo (isipokuwa kuhani mkuu mara moja kwa mwaka). Lakini sasa waumini wanaweza kuingia patakatifu-pa-patakatifu Mungu alipo, kwa njia ya Kristo Yesu (Waebr.10:19-22)!

Jambo muhimu tunaloweza kutafakari! Mungu mwenyewe aliagiza waweke pazia lile hemani (hekaluni) lakini kupitia kifo cha Mwanawe msalabani Mungu anaondoa Agano la kwanza ili kusudi alisimamishe Agano la pili ‘‘….Maana kama lile la kwanza (Agano la Kale) lingalikuwa halina upungufu, nafasi isingalitafutwa kwa lile la pili (Agano Jipya).” (Waebr 8:13). Hivyo basi hakuna mistari kutoka vitabu vya Injili (Mathayo – Yohana) tunayoweza kunukuu ili kuwafundisha watu washike torati ya Musa. (Na mitume pamoja na Roho Mtakatifu walithibitisha ukweli huu katika Matendo ya Mitume sura ya 15!) Desturi za Wayahudi walioifuata sheria ya Musa kabla ya kifo cha Yesu huwezi kamwe kufananisha na tabia na matendo ya kanisa la Bwana Yesu baada ya kufufuka kwake! Au unataka kutahiriwa?

Kwa hiyo mtume Paulo anafundisha kuwa ni jambo la udanganyifu kuwafundisha watu washike siku ya Sabato. Kwa sababu ya wokovu wetu ndani ya Kriso (Wakolosai 2:11-15) Paulo anasema,

“Basi, MTU ASIWAHUKUMU ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au SABATO; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.” (mst.16).

Paulo anaanzisha mstari huo na neno hili, “Basi..” Kwa nini? Kwa sababu ya mistari 14 na15, “(Yesu) akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.”

Baada ya kutangaza mambo makubwa Bwana Yesu aliyoyafanya msalabani, Paulo anaendelea kwa kusema, ‘Basi’ au ‘Kwa hiyo’, mtu asiwahukumu NINYI. Tutambue, Paulo hasemi ‘ndugu, msiwahukumu wengine.” Hili sili onyo ili tusiwahukumu wengine kwa ujumla. Paulo hakariri fundisho la Yesu aliposema, “Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi.” Hapana. Muktadha ni wazi! Anasema kwa sababu ya wokovu wetu katika Kristo Yesu, wewe USIWARUHUSU WENGINE wakuhukumu! Kwa nini wengine wangekuhukumu? Paulo anasema kwa wazi, “mtu asiwahukumu ninyi KATIKA vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au SABATO”. Unaona, muktadha unahusu mambo ya nje wa torati na unahusu wale ambao watatuhukumu (kwa kusema sisi sio wakristo kweli) kama tusipokubaliana na mafundisho yao ya kushika siku ya sabato. Walikuwepo watu wa dini – kama tunavyojua kwa kusoma hasa Matendo na Wagalatia – waliotaka wakristo waishi chini ya sheria, yaani, kushika mambo ya nje ya torati; kwa mfano watahiriwe au washike ‘siku’ ya torati. Paulo anafundisha hapo kama mtu akisema, “Lazima ushike sabato ili kumpendeza Mungu au kuokoka ‘kweli’, usimruhusu akuvute chini ya sheria hiyo na humjali kama anakuhukumu! Tunasoma kwenye Matendo 15 na Wagalaia juu ya watu waliojaribu kupotosha njia ya Ukweli kwa kuwalazimisha waumini wayarejee mambo ya torati ya Musa. Ni  vivyo hivyo siku hizi. Wasabato wanawahukumu wakristo kwa sababu hawashiki siku ya sabato! Paulo aliwaonya wakristo juu ya watu wa dini kama hao hao!

Hayo ni mafundisho ya Agano Jipya. Hatuwezi kusema au kufundisha kwamba ni lazima tukusanyike siku ya Sabato (jumamosi). Kama fulani akifundisha hivyo anawadanganya watu, sawasawa na maneno ya Paulo. Au je, tunataka kusema Paulo alifundisha uongo? Au tunataka kutumia mstari mmoja dhidi ya mstari mwingine kana kwamba Biblia siyo neno la Mungu? Mistari yote ina muktadha (mazingira) yake! Nani aliyekupa wewe ruhusa na mamlaka kupendelea mstari mmoja na kuudharau mstari mwingine au kutokujali kabisa? Hakika hiyo haitokani na Mungu.

Paulo anafundisha sehemu nyingine kama fulani kwa ajili ya dhamira yake akitaka kuishika au kuiheshimu siku moja kuliko siku nyingine, anao uhuru wa kufanya hivyo, lakini ni jambo la DHAMIRA YAKE tu. Siyo sheria wala mafundisho ya Agano Jipya, na hawezi kuwahukumu wengine wasioishika. Paulo anaeleza kwa wazi, “Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku, mwingine aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe.” (War 14:5). Ni vyema kusoma sura nzima. Lakini pia ni vyema kufundishwa na mistari ile inayohusu mada yetu, na siyo tu kujenga mafundisho binafsi kwa ajili ya kutumia mistari ile tunayoipenda na inayoonekana kuthibitisha mtazamo wetu.

Wokovu wetu siku hizi uko ndani ya Kristo, siyo kwa kushika Torati ya Musa. Kuna watu wasiijua Biblia tena hawaelewi hata Agano Jipya. Hawaelewi KWA NINI Yesu alikufa. Kwa mfano wanaposema, ‘Imeandikwa katika Kutoka 20:8-11 lazima tushiike sabato!’ Je! ina maana mtume Paulo alifundisha uongo?  Au alitaka kutudanganya? Au Unafikiri Biblia inajipinga yenyewe? Je! Unaamini Biblia siyo neno la Mungu? Au kwa nini watu wanapenda kujizika katika Agano la Kale?

Paulo anafundisha huwezi kumfuata na kumwamini Yesu wakati bado unataka kushika sheria ya Musa. Kama nilivyosema ni jambo la udanganyifu na la hatari sana. Mtume Paulo anaanza barua yake kwa Wagalatia kwa kusema, “Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia injili ya namna nyingine. Wala si nyingine; lakini wapo watu wawataabishao na kutaka kuigeuza injili ya kristo. Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe. Kama tulivyotangulia kusema, na sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo mliyoipokea, na alaaniwe.” Ni wazi anaongea juu ya wale waliotaka kufuata mambo ya sheria ya Musa. Paulo asingaliweza kutumia maneno makali zaidi namna hii.

Anasema ni ‘injili nyingine’, na kumbe, inatokea siku hizi! Watu wengine siku hizi wanasema kama usiposhika Sabato huna sehemu katika kanisa kweli la Bwana – ukienda barabarani huko! Utaona, wanavyoifuata sheria badala ya kuishi kwa imani tu, na udanganyifu wao hauna mwisho! Ndivyo ilivyo kuwa hata siku za mtume Paulo kama tulivyoona katika barua yake kwa Wagalatia. Bila shaka mafundisho hayo yanaharibu imani ya watu, sawasawa na mafundisho ya Paulo katika Wagalatia sura ya kwanza. Mafundisho haya yanawakilisha ‘injili nyingine’ ambayo inafundisha lazima kushika ‘siku, miezi, nyakati, na miaka’, na kuifuata sheria juu ya tohara.

Waumini wa makanisa ya Galatia walimwamini Yesu kuwa alikuwa Mwana wa Mungu; waliamini alikufa kwa ajili ya wokovu wao; waliamini juu ya nguvu na vipawa vya Roho Mtakatifu (Wagal.4:13). Lakini sasa! Kwa nini wanaonekana kutaka tena kushika siku, miezi, na miaka? Labda tunaweza kufikiri kuwa haina madhara kwa sababu ni wakristo waliookoka kupitia huduma ya mtume Paulo! Lakini sawasawa na neno la Mungu, kufanya hivyo ni hatari sana kwa wale wanaotaka kuzishika siku/nyakati(n.k) kwa Torati.

Paulo anaweka wazi, “Mmetengwa na Kristo, ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema…Nachelea, isiwe labda nimejitaabisha bure kwa ajili yenu.” (Wagal.5:4; 4:11).

Paulo alihuzunishwa sana, kwa sabau anasema wazi hivi “…..sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini KUYAREJEA TENA MAFUNDISHO YA KWANZA yaliyo manyonge, yenye upungufu, ambayo mnataka kuyatumikia tena? MNASHIKA SIKU, na miezi, na nyakati, na miaka.”(Wagal.4:9,10). 

Je!  Naweza kutengana na Kristo kwa sababu nataka kushika siku au miezi n.k? Mafundisho ya neno la Mungu yako wazi sana! Kwa mfano, kama ukishika mambo ya sheria ya Musa, labda sabato au kutahariwa, uwe na uhakika kuwa imani yako ni bure! Yaani umeweka tumaini lako katika mambo yasiyofaa, ambayo Mungu Mwenyewe ameyaondoa! Kristo alikufa ili umtegemee yeye tu, ili uokolewe kupitia neema Yake na uishi ndani Yake na kupitia yeye, usiweke tumaini lako juu ya kitu cho chote! Ukisema, ‘Namwamini Yesu na tena nashika sheria ya Musa,’ hapo unajidanganya mwenyewe! Hatupaswi kutegemea mfumo wa nje wa Torati ili kumpendeza Mungu. Wala kushika Torati ya Musa ili kuhesabiwa haki, au kuhesabiwa kuwa watu wa Mungu. Hatuwezi kutakaswa na mambo ya nje kwani Wokovu, haki, utakatifu, viko ni NDANI ya Kristo, kupitia Kristo Yesu mwenyewe! Lazima tuwe ndani ya Kristo! Na hayo yote yanatokana na Kristo Yesu kwa utukufu wa Mungu! Kama ilivyoandikwa,

“Maana yale YASIYOWEZEKANA kwa sheria, kwa vile ilivyokuwa DHAIFU kwa sababu ya mwili, Mungu, kwa kumtuma Mwanawe mwenyewe katika mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kwa sababu ya dhambi, aliihukumu dhambi katika mwili; ILI HAKI YA TORATI YATIMIZWE NDANI YETU sisi, tusioenenda kwa kufuata mambo ya mwili, bali mambo ya roho.” (Warumi 8:3,4).

Mafundisho ya mtume Paulo ni sawa na mafundisho ya mitume wengine na wazee wa huko Yerusalemu. Walikuwepo waumini wanaotoka Yerusalemu waliojitahidi kuifuata sheria ya Musa nao walisema, “Msipotahiriwa kama desturi ya Musa hamwezi kuokoka.” Ndipo, “Mitume na wazee wakakusanyika wapate kulifikiri neno hilo.” Lakini Petro alisema, “mbona mnamjaribu Mungu na kuweka kongwa juu ya shingo za wanafunzi, ambalo baba zetu wala sisi hatukuweza kulichukua. Bali twaamini kwamba tutaokoka kwa neema ya bwana yesu vile vile kama wao…Kwa sababu hiyo, mimi naamua hivi; tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika Mataifa; bali tuwaandikie kwamba wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu,  kwa maana tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake, katika kila mji husomwa kila sabato katika masinagogi.” (Matendo.15:1,6,10,11,19-21). Na baada ya majadiliano hayo kanisa la             Yerusalemu waliituma barua hiyo kwenye makanisa mengine katika Mataifa,

“Kwa kuwa tumesikia ya kwamba watu waliotoka kwetu WAMEWASUMBUA kwa maneno yao, wakipotosha roho zenu, ambao sisi hatukuwaagiza…ILIMPENDEZA ROHO MTAKATIFU na sisi, TUSIWATWIKE MZIGO ILA HAYO yaliyo ya lazima, yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati. Mkijizuia na hayo, mtafanya vema. Wasalamu.” (Matendo 15:28,29)

Kutokana na mistari hiyo, ni wazi kuwa Roho wa Mungu aliwaongoza mitume wa kanisa kufanya maaumuzi hayo! Hawakuwaagiza waumini wa makanisa katika Mataifa kutahiriwa, wala kushika Sabato, wala kushika mwezi, wala kushika lolote lihusulo mambo ya nje ya Torati ya Musa, ila wajiepushe na damu na nyama zilizosongolewa (na kujiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na uasherati). Kwa hiyo, mtume Paulo anasisitiza, “Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au SABATO.”

Kama kuna watu wanaotaka kushika sheria ya Musa basi wajitahidi sana kwa ajili ya sheria, wakati mwingine husema, ‘Lakini kushika sabato ni sehemu ya amri kumi.’  Kwanza! Hata mitume nao huko Yerusalemu walijua hivyo, lakini hawakuweka mizigo ya kushika sabato mabeguni mwa waumini. Pili! Je! Unafikiri mtume Paulo alimpinga Mungu katika mafundisho yake? Tatu, kama ukitaka kuzifuata amri kumi, je, hujui kuwa haitoshi? Je! Hujalisikia Mwana wa Mungu alivyosema? “Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue, na mtu akiua, itampasa hukumu. BALI MIMI NAWAAMBIENI, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu…Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:21,22; 27,28). Kama ni hivyo, vipi maagizo yaliyoandikwa katika vibao vya mawe yatakuwezesha kutimiza haki ambayo maneno ya Yesu yanaiwakilisha? Je, unataka kushika torati badala ya kupokea Roho ya Yesu na kujazwa matunda ya haki iliyo kwa njia ya Yesu Kristo? (Wafilipi 1:10). Je,unadharau maisha ya Yesu ndani yako ili kushika torati ya Musa? Je, unampinga Mungu na unakataa kuupokea ‘moyo mpya’ kama Mungu alivyoahidi, “Nami nitawapa ninyi moyo mpya, nami nitatia roho mpya ndani yenu, nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani ya mwili wenu, nami nitawapa moyo wa nyama.”? (Ezekiel 36:26)

Kumbuka! ‘Kiwango’ cha haki ya Injili ya Yesu Kristo kinapita kiwango cha Torati ya Musa kwa kiasi kikubwa sana! Kwa hiyo basi, unaishi kwa kufuata sheria au kwa uzima wa Kristo ndani yako? Maana imeandikwa, “torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo.” (Yoh.1:17). Je! Unaishi kwa uongozi wa torati ya Musa au kwa uongozi wa neema na kweli katika Yesu Kristo? Sheria yoyote ambayo ipo NJE yako haiwezi kuokoa, haiwezi kukuwezesha kuishi kama mkristo – ili uweze kuishi kwa uongozi wa neema na kweli ya Kristo lazima uzaliwe mara ya pili, toka juu! Na ubatizwe kwa Roho Mtakatifu ili Yesu Kriso aishi ndani yako! Bila kuwa na Yesu ndani yako huwezi kuishi maisha ya Ukristo, wala kitimiza haki ya torati. Hayo yote yanawezekana kwa sababu ya neema ya Mungu pekee, na kwa sababu inatokana na neema, lazima tupokee kwa imani! “Kwa hiyo ilitoka katika imani, iwe kwa njia ya neema… Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani.” (Warumi 4:16; Waefeso 2:8).

Biblia ni moja – hamna mabishano (contradictions) kati ya mistari! Wengine wanapenda kunukuu mistari kutoka Agano la Kale kuwalazimisha watu kushika Sabato (wakusanyike jumamosi), lakini kama tulivyoona hapo juu, katika makanisa ya Agano Jipya haikuwa sheria kama hiyo miongoni mwa Wakristo. Pia ilikuwa desturi (siyo sheria) ya washirika kukusanyika jumapili katika Agano Jipya (Matendo 20:7; 1 Wakor.16:2).

(Kwa lugha ya Kigiriki katika Agano Jipya waandishi wanatumia neno moja juu ya vitabu vitano vya kwanza ya Biblia (Mwanzo-Kumbukumbu), na neno hili ni ‘nomos’. Lakini katika Biblia ya Kiswahili wametafasri neno hili kwa maneno mawili, yaani, ‘torati’ au ‘sheria’. Kwa hiyo, katika somo hili ninatumia maneno yote ‘torati’ (ya Musa) na ‘sheria’ (ya Musa) kwa maana neno moja linahusika vitabu vitano vya kwanza ya Biblia (Mwanzo-Kumbukumbu) na la pili linazingatia amri kumi. Biblia ya Kingereza inafuata mfumo wa Kigiriki yaani inatumia neno moja tu ‘the law’.)

                                               ————————————–

Mafarisayo walimshitaki Yesu kuwa anawaruhusu wanafunzi wake wavunje sheria ya Musa, kuvunja sabato (Marko 2:23-28). Lakini Bwana Yesu aliwajibuje? Kwanza! Aliwakumbusha mafarisayo kuwa Daudi alifanya jambo lisilo la halali kadiri ya sheria. Sawa sawa na Torati ya Musa, makuhani pekee  ndio walitakiwa kula mikate ya Wonyesho/Hekaluni, lakini Daudi aliingia katika hema na akaila mikate ile! Jambo la maana sana na la ajabu ambalo tunaliona hapo ni kuwa Bwana Yesu alitetea tendo lililofanywa na  Daudi ingawa Daudi kwa wazi kabisa alivunja amri ya sheria! (Hesabu 24:5-9). Daudi alipohitaji chakula, ilikuwa ni muhimu zaidi machoni pa Bwana, Daudi apate chakula ili aishi kuliko kuifuata amri za sheria ihusuyo mambo ya nje tu! Ndipo Yesu anasema, “Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu, wala si mwanadamu kwa ajili ya sabato.” Kwa maneno hayo Bwana Yesu anaweka wazi kabisa kwamba sabato iliwekwa kwa ajili ya KUMTUMIKIA MWANADAMU na siyo iwe ‘bwana’ juu yake! Huu ndiyo ukweli wa msingi ambao Mwana wa Mungu anatudhihirishia sasa! Bwana Yesu anaendelea kutufundisha mambo mapya na ya muhimu sana kwa kusema maneno hayo, “Mwanawa Adamu ndiye Bwana wa sabato pia.” Ina maana gani? Ina maana ya kuwa Mungu aliyetoa maagizo juu ya mambo ya nje kupitia Torati ya Musa (katika Agano la Kale), Yeye anayo mamlaka ya kubadilisha agano lile kwa ajili ya faida ya mwanadamu, kwa ajili ya wokovu wake – Yeye ndiye Bwana wa sabato! Na hivyo ndivyo Mungu alivyofanya kupitia Mwanawe. Torati haikuweza kutuokoa, kwa hiyo Mungu alitoa Agano JIPYA na kupitia Agano hili tunaweza kusafishwa na  kuokolewa na dhambi! Torati  ilitolewa kwa mkono wa Musa bali neema, kweli na wokovu zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo. Siku hizi watu wengine wanafanya kosa lile lile ambalo mafarisayo walilifanya, yaani, wanafanya sabato kuwa ‘bwana’ na kwa njia hiyo hawamheshimu wala hawamjali Bwana Yesu ambaye ni ‘Bwana wa wote’, na aidha hawapokei wokovu ule ambao Yeye alikufa ili kutupa/kutuletea. Wanampinga Yesu vivyo hivyo mafarisayo walivyofanya.

Mungu alimpa Ibrahimu Agano la Tohara (Matendo 7:8) na wakati wa Agano la Kale ilikuwa ni lazima mtu kupata tohara ili torati ya Musa isije ikavunjika (Yohana 7:23), lakini baada ya kufa kwa Yesu mambo yote ya nje yameondolewa. Mifumo yote ya kuwatakasa watu wa Mungu chini ya torati ya Musa imeondelewa katika Kristo Yesu!

Kama ilivyoandikwa, “Basi hata agano la kwanza lilikuwa na kawaida za ibada, na patakatifu pake, pa KIDUNIA.” (Waebr.9:1). Lakini “ile SHERIA HAIKUKAMILISHA neno” (Waebr.7:19). Kwa hiyo Mwana wa Mungu alikuja naye “kwa toleo moja AMEWAKAMILISHA HATA MILELE HAO WANAOTAKASWA.” (Waebr. 10:14). Basi, Kristo Yesu ni kuhani mkuu wetu sasa, na kwa hiyo, “ukuhani ule ukibadilika, hapana budi sheria nayo ibadilike.” (Waebr.7:19). Ndio maana Mungu alifanya Agano Jipya, “Kwa kule kusema Agano jipya, amelifanya lile la kwanza kuwa kuukuu. Lakini kitu kianzacho kuwa kikuukuu na kuchakaa ki karibu na kutoweka” (Waebr.8:13). Agano la Kale lilijionyesha kuwa kuukuu Mungu amefanya Agano Jipya!

Mambo yote ya nje juu ya Agano la Kale yameondelewa kwa sababu yalikuwa ‘kivuli’ tu. Huwezi kula ‘kivuli’; huwezi kunywa ‘kivuli’; ‘kivuli’ hakiwezi kukulisha; huwezi kushika ‘kivuli’; huwezi kusimama juu ya ‘kivuli’; ukijaribu kuishi kwa ‘kivuli’ utakufa! ‘Kivuli’ hakiwezi kukupa uzima wala haki! Kivuli hakiwezi kukuhuisha wala kukufanya uwe safi kwa ndani!  

“…wako watoao sadaka kama iagizavyo sheria; watumikiao MFANO NA KIVULI CHA MAMBO YA MBINGUNI, kama Musa alivyoagizwa na Mungu, alipokuwa tayari kuifanya ile hema…” (Waebr.8:4,5)

Unaona? Sadaka zote na mifumo yote ndani ya hema zilikuwa mifano na kivuli tu cha mambo ya mbinguni, mambo ya kiroho, mambo ya Yesu Kristo, mambo ya uzima wa milele! Mifano tu! Kivuli tu! Kivuli hakiwezi kukutakasa kwa ndani, wala kukuweka huru mbali na dhambi! (Waebr.9:13,14). Torati / sheria ya Musa – haziwezi kuhuisha! Haki haipatikani kwa sheria! “…kama ingalitolewa sheria iwezayo kuhuisha, yamkini haki ingalipatikana kwa sheria.” (Wagalatia 3:21).

“Basi torati, kwa kuwa ni KIVULI CHA MEMA YATAKAYOKUWA, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, HAIWEZI WAKATI WO WOTE KUWAKAMILISHA WAKARIBIAO…Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi…AONDOA LA KWANZA, ILI KUSUDI ALISIMAMISHE LA PILI. Katika mapenzi hayo mmepata utakaso kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu.” (Waebr10:1,4,9,10).

Labda unaweza kufikri kuwa mambo haya yanahusu mfumo wa hema tu, hapo utakuwa unakosea. Paulo anatumia lugha ile ile juu ya siku ya sabato. Soma!

Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, AU SABATO; mambo hayo ni KIVULI cha mambo yajayo; BALI MWILI NI WA KRISTO. Mtu asiwanyang’anye thawabu yenu…” (Wakolosai 2:16-18).

Umeona? “Mtu asiwanyang’anye thawabu yenu!” Sabato ni jambo la kivuli tu, la nje tu, la mfano tu, lakini Yesu alikufa ili tusiishi kivulini bali ndani Yake Kristo – na kupitia Yeye tu, tumejazwa matunda ya haki! (Wafilpi 1:11). Mungu apewe sifa! “Maana katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili. Na ninyi mmetimilika KATIKA YEYE…” (Wakolosai 2:16-18).

Mambo haya yote (ya nje) ya Agano la Kale yalipewa, yaliagizwa kwa lengo la kutufundisha juu ya Yesu Kristo – yanawakilisha mambo yale ambayo Yesu Kristo angetenda msalabani ili kutuokoa, kututakasa na kutuweka huru mbali na dhambi! Hivyo basi kwa nini watu wanataka kurejea kivuli?

Kama nilivyotangulia kusema, Mungu alimpa Ibrahimu agano la tohara (Matendo 7:8) na wakati wa Agano la Kale ilikuwa lazima mtu kupata tohara ili torati ya Musa isije ikavunjika; lakini sasa, kwa sababu ya kifo cha Yesu msalabani, hamna tohara ya mwili kwa waumini; BADALA YAKE inasema, “Na ninyi mmetimilika katika yeye…Katika yeye mmetahiriwa kwa tohara ISIYOFANYIKA KWA MIKONO, kwa kuuvua mwili wa nyama, kwa tohara ya Kristo.” (Wakolosai 2:10,11). BADALA YA damu ya wanyama, Mwana wa Mungu alimwaga damu yake! BADALA YA kuhani mkuu tu kuingia Patakatifu pa Patakatifu pa kidunia mara moja kwa mwaka tu, SASA kupitia damu ya Yesu, wale waokolewao wamekaribishwa na kuhimizwa kupaingia Patakaifu pa kweli mbinguni kwa Roho. Soma kwa makini sana Waebrania 9:6-12,24; 10:19-22! Ni andiko muhimu sana. Labda ninukuu kwa sehemu tu:

“Roho Mtakatifu akionyesha neno hili, ya kwamba njia ya kupaingia patakatifu ilikuwa haijadhihirishwa bado, hapo HEMA YA KWANZA ilipokuwa ingali ikisimama…Kwa sababu Kristo hakuingia katika patakatifu PALIPOFANYIKA KWA MIKONO, ndio MFANO wa patakatifu halisi; bali aliingia MBINGUNI, ili aonekane usoni pa Mungu kwa ajili yetu…Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu…”

Je, unajua kwa dhati ukweli wa mistari hiyo katika maisha yako ya kiroho? Je, unafahamu ukweli huo kutokana na uzoefu wako, au ni jambo la ujuzi tu, au hata inaonakana kama kitu kigeni kwako? Au unaishi kivulini tu?

BADALA YA kwenda hekaluni kwa jinsi ya kidunia, Biblia inasema juu ya waumini “mmejengwa pamoja kuwa MASKANI ya Mungu katika ROHO…..SISI tu hekalu la Mungu aliye hai…” (Waefeso 2:22; 2 Wakor6:16). Kwa sababu hiyo, BADALA YA kuishika sabato ya nje, Yesu kristo amefufuka sasa, neno la Mungu linatuhimiza tuingie kwenye ‘raha’, yaani, pumziko Lake! “Basi, ikiwa ingaliko ahadi ya kuingia katika raha yake (pumziko lake) na TUOGOPE, mmoja wenu asije akaonekana ameikosa.” (Waebr.4:1).

Kumbe! Jambo la ajabu sana! Kwa hiyo basi kupitia lile Mungu alilolifanya ndani yetu katika Kristo Yesu sisi tuaminio tunaweza na zaidi ya yote inatubidi tuingie rahani, yaani katika pumziko la Mungu mwenyewe – kwa imani, katika damu ya Yesu na kwa Roho wa Mungu. Inatubidi kuingia kwa imani katika ya raha (pumziko) ya Mungu.Unaamini maneno hayo?

Katika Agano la Kale Mungu alisema, “Ikumbuke siku ya Sabato uitakase…Kwa kuwa kwa siku sita, BWANA aliumba mbingu na nchi, bahari na vyote vilivyomo ndani yake, lakini akapumzika siku ya saba. Kwa hiyo BWANA akaibariki siku ya Sabato na kuifanya takatifu.” (Kutoka 20:8,11)

 [ Kwa maneno mengine sabato kimsingi ni siku ya ‘pumziko’. Lazima kuitakasa na kutokufanya kazi. Na kwa mjibu wa torati, siyo halali kufanya kazi yoyote siku ya sabato wala wewe au familia yako yote, tena siyo halali kupika chakula siku ya sabato, kwa maana sabato ni siku ya ‘pumziko’ na kutokana na Agano la Kale, mtu akifanya kazi siku hiyo lazima auawe (Kutoka 20:8-11; 31:14-17; 35:2,3; Hesabu 15:32). Sawasawa na kitabu cha mwanzo sura ya kwanza, kila siku ilianza jioni ya siku na ilikwisha jioni ya kesho yake. ]

Maana sisi TULIOAMINI tunaingia katika raha (pumziko) ile…” (Waebr.4:3). Raha au Pumziko hili inahusu nini! Kumbe, mwandishi wa Waebrania anaitaja Mwanzo 2:2, Kwa maana ameinena siku ya saba mahali fulani hivi, Mungu alistarehe (alipumzika) siku ya saba, AKAZIACHA KAZI ZAKE ZOTE…” (Waebr.4:4). Ina maana kuwa kwa mara ya kwanza katika historia ya wanadamu waumini wanaweza kuingia katika raha ya kweli, raha ya kiroho, raha ya Mungu mwenyewe! Sikiliza, “Kwa maana yeye aliyeingia katika RAHA YAKE amestarehe mwenyewe KATIKA KAZI YAKE KAMA VILE MUNGU ALIVYOSTAREHE KATIKA KAZI ZAKE” (Waebr.4:10). Raha hiyo ni raha ya Mungu ya siku ile alipopumzika katika kazi zake zote!

Kupitia wokovu katika Kristo yesu, inatubidi kustarehe ili kupata pumziko katika kazi zetu kama vile Mungu alivyopumzika! Unaamini hiyo! Kwa sababu imeandikwa, “Basi, na TUFANYE BIDII kuingia katika raha ile, ili kwamba mtu ye yote asije akaanguka kwa mfano huo huo wa kuasi.” (Waebr.4:11).

Kwa hiyo neno la Mungu linatangaza, “Kwa maana mmeokolewa KWA NEEMA, KWA NJIA YA IMANI; ambayo hiyo HAIKUTOKANA NA NAFSI ZENU ni kipawa cha Mungu; wala SI KWA MATENDO, mtu awaye yote asije akajisifu. Maana TU KAZI YAKE, TULIUMBWA KATIKA KRISTO YESU, tutende matendo mema, ambayo TOKEA AWALI MUNGU ALIYATENGENEZA ILI TUENENDE NAYO.” (Waefeso 2:8-10).

Hamna neno la kushika sabato ‘ya nje’ kwa waumini katika Agano Jipya! BADALA YAKE tumehimizwa kuingia katika raha (pumziko) ya Mungu – hiyo ni ‘sabato’ ya kweli! Sikilize maneno hayo:

Katika siku ya saba Mungu alikuwa amekamilisha kazi aliyokuwa akiifanya, hivyo SIKU YA SABA AKAPUMZIKA kutoka kazi zake zote. Mungu akaibariki siku ya saba akaifanya takatifu, kwa sababu katika siku hiyo alipumzika KUTOKA KAZI ZOTE za kuumba alizokuwa amefanya” (Mwanzo 2:2). Tumeitwa kuingia katika raha hiyo! “Kwa hiyo kama anenavyo Roho Mtakatifu, Leo kama mtaisikia sauti yake, MSIFANYE MIGUMU MIOYO YENU…” (Waebr.3:7,8)

Katika torati imeandikwa, “Ikumbuke siku ya Sabato uitakase. Kwa siku sita utafanya kazi zako zote, lakini siku ya saba ni Sabato kwa BWANA Mungu wako. Siku hiyo hutafanya kazi yo yote…Kwa kuwa kwa siku sita, BWANA aliumba mbingu na nchi, bahari na vyote vilivyomo ndani yake, lakini akapumzika siku ya saba. Kwa hiyo BWANA akaibariki siku ya Sabato na kuifanya takatifu.” (Kutoka 20:8-11). Maneno hayo yanahusu maneno ya Mungu kwenye Mwanzo 2:2 na maneno hayo yanatajwa katika Waebrania sura ya 4 (lakini ukweli wa pumziko la Mungu unafundishwa pia katika sura ya 3). Kwa hiyo basi ‘sabato’ iliyotajwa katika Kutoka 20:8-11 ni jambo la nje tu, ni mfano au kivuli cha raha au pumziko lile la kweli la Mungu, ambalo tunaliingia kwa imani! Kama tulivyoona, haya siyo maneno yangu, bali ya Paulo aliyesema ‘sabato’ ni kivuli  tu.

(Kwa upande mwingine mwandishi kwa Waebrania anaongea juu ya nchi ya ahadi katika sura 3 na 4, lakini anaeleza watu wa Mungu jangwani hawakuingia ‘raha’ ile kwa sababu hawakumwamini Mungu. Ndipo anasema “Maana kama Yoshua angaliwapa raha, asingaliinena siku nyingine baadaye, Basi IMESALIA RAHA YA SABATO KWA WATU WA MUNGU.” Mwandishi katika sura hizo anasisitiza kuwa raha ile siyo raha ya dunia hii yaani nchi ya Kanaani bali raha ya Mungu mwenyewe-[makao ya milele])

                                                    ————————————–          

Katika siku za mtume Paulo kulikuwa na watu waliiotetea sheria na waliojitahidi sana kwa ajili ya torati ya Musa. Watu hao walimlaumu mtume Paulo wakisema anawapotosha watu kwa mafundisho yake! Walimshtaki Paulo kuwa anafundisha watu kuwa wanao uhuru wa kufanya dhambi na kuvunja amri kumi za Mungu kwa sababu anasema ‘sisi hatuwi chini ya sheria bali chini ya neema’. Paulo anataja watu hao, “…Kwa nini tusiseme (kama TULIVYOSINGIZIWA, na kama wengine wanavyokaza kusema ya kwamba twasema hivyo), NA TUFANYE MABAYA, ILI YAJE MEMA? Ambao kuhukumiwa kwao kuna haki.” (Warumi 3:8). Katika Agano Jipya tunaona makanisa yalipata shida sana na hasa walitaka waumini waishi chini ya torati/sheria, na Paulo alitumia muda mwingi katika nyaraka zake kuyapinga mafundisho yao!

Kumbe! Hata siku hizi! Watumishi wa Mungu tunasingiziwa ya kwamba tunawafundisha watu kuwa wanaweza kufanya uzinzi, kuiba, kuabadu sanamu n.k kwa sababu tunatumia lugha ya Agano Jipya, yaani, ‘sisi hatuwi chini ya sheria bali chini ya neema’. Wanadai kuwa tunatoa ruksa kuvunja amri za Mungu kwa kutumia maneno hayo. Ni dhahiri kwamba watu hao hawajasoma Biblia tena hawaelewi Agano Jipya. Hata hivyo mashitaka kama hayo ni uongo mtupu. Hali ya kushika siku ya sabato imewafanya wengine kuwa viziwi na vipofu. Inawafanya hata hawawezi kuelewa maneno ya Paulo, wala yale tunayoyafundisha hivi leo. Paulo anafundisha kwa wazi kabisa, “Tuseme nini basi? Tudumu katika dhambi ili neema izidi kuwa nyingi? Hasha! Sisi tulioifia dhambi tutaishije tena katika dhambi?” (Warumi 6:1,2). Kwa nini wale wanaojitahidi kwa ajili ya torati hawaelewi tunayoyasema? Paulo anaendelea kwa kusema, “Ni nini basi? Tufanye dhambi kwa sababu hatuwi chini ya sheria bali chini ya neema? Hasha!” (Warumi 6:15). Kwa nini hawayaelewi hayo? Ukweli ni kinyume cha wanavyodai! Paulo asema  tena, “Kwa maana dhambi haitawatawala ninyi, kwa sababu hamwi chini ya sheria, bali chini ya neema.” (Warumi 6:14). Unaona? Dhambi haitatutawala sisi! Kwa nini? Kwa sababu ‘hatuwi chini ya sheria’ – bali chini ya neema! Ina maana kama mtu akiishi chini ya sheria, dhambi inamtawala! Watu wengine hawaelewi kuwa kuishi ‘chini ya sheria’ – maana yake sheria haiwezi kutakasa, kuhuisha, wala kutuweka huru mbali na dhambi. Wanafikiri, ‘Usipokuwa chini ya sheria, unaweza kufanya dhambi’, na wanashtuka! Kama vile hawajawahi soma au kusikia Injili isemayo! Tunaokolewa kwa neema na tunaishi kwa imani, siyo kwa torati ya Musa. Je, ina maana tunao uhuru kutenda dhambi? Hasha! Je, kwa nini watu haelewi maneno ya Paulo anasemapo, “Basi, je! twaibatilisha sheria kwa imani hiyo? La hasha! Kinyume cha hayo twaithibitisha sheria.” (Warumi 3:31)

Paulo anaeleza kwa wazi lengo la Mungu kupitia Agano Jipya, “Maana yale YASIYOWEZEKANA kwa SHERIA, kwa vile ilivyokuwa dhaifu kwa sababu ya mwili, Mungu mwenyewe, kwa kumtuma Mwanawe katika mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kwa sababu ya dhambi, aliihukumu dhambi katika mwili; ILI HAKI (kwa tafsiri nyingine ‘maagizo’) YA TORATI ITIMIZWE NDANI YETU SISI.” (Warumi 8:3,4)

HATA HIVYO, baada ya kuyaelewa mambo hayo hapo juu, baadhi ya wale wanaotetea sabato wanaendelea kusema kama hushiki sabato ina maana unafundisha amri kumi za Mungu zilifutwa na unaruhusu watu kuiba, kufanya uzinzi, kuabudu sanamu n.k.. Tunaweza kushangaa, kama vile Paulo alivyoshangaa pia! (Wagaltia 1:6). Je, kwa nini hawajui kuwa kwa neema ya Mungu, kupitia wokovu wetu katika Yesu Kristo na kwa kumwamini Yesu, “tulipokwisha kuwekwa huru mbali na dhambi, tulifanywa kuwa watumwa wa haki?” (Warumi 6:18). Paulo anasema, “Ni dhahiri ya kwamba hakuna mtu ahesabiwaye haki mbele za Mungu katika sheria; kwa sababu MWENYE HAKI ATAISHI KWA IMANI.” Wengi wanayo shida au hawaelewi mafundisho juu ya sheria katika Agano Jipya, yaani, tunaishi kwa ‘imani’, siyo kwa sheria. Hata hivyo, sheria (torati) siyo mbaya! Tatizo ni ufahamu mdogo!

                                              ————————————–

Labda nitoe mfano huu: Tumeambiwa lengo letu ni kufika kisiwa Fulani na agizo/sheria inasema ni  lazima tufikie. Kisiwa hicho kiko umbali wa kilometa elfu moja (km1000). Na ili tufike maagizo yanasema lazima tuogelee kilomita elfu moja! Huo unaitwa Mpango wa Kwanza. Wengi walijaribu, na wote walikufa! Sasa yule aliyetoa sheria tufikie kisiwa kile kwa kuogelea anatueleza tena, “Sheria iko sawa. Sijabadilisha lengo la kufika kisiwani. Lakini ni lazima nilibadilishe NJIA ya kutimiza lengo langu la sheria. Kwa hiyo badala ya kuogelea (yaani, kulitimiza lengo kwa UWEZO WAKO  tu) kufikia kisiwa kile, nimetengeneza boti kubwa, lenye enjine yenye nguvu sana kwa ajili yako ufikie kwenye kisiwa kile! Huo sasa unaitwa Mpango Mpya! Kwa hiyo, panda boti tu kwa imani! Utafika kisiwani na utatimiza lengo la sheria yangu! Kanuni ya boti ni moja tu ‘Ni lazima ukae ndani ya boti hii niliyoitayarisha kwa ajili yako.” (Kwa hiyo, neno la Mungu linasema, “yale YASIYOWEZEKANA kwa sheria, kwa vile ilivyokuwa dhaifu kwa sababu ya MWILI.”) Wengine wanamwamini mwenye kutoa sheria na wakupanda botini mara moja kwa imani. Wengine watakataa kupanda boti wakisema, “Hapana! Hatutaacha kuishi kwa sheria yetu, yaani sheria ya kuogelea. Lakini kumbuka! Lengo ni tufike kwenye  kisiwa na kama tukipanda boti, na tunaweza kwenda tupendapo na hatutakosea lengo, wala kushindwa kufikia kisiwani. Nafasi yetu sisi ni kuwa ni waaminifu na kumtii mwenye kutoa sheria! Tutaendelea kuogelea! Ninyi wengine mtapotoshwa!”

Ukweli ni kwamba kwanza! Wale waliochagua kuendelea kuishi kwa mpango wa kwanza hawamtii mwenye kutoa sheria wala hawamwamini – waliupinga mpango wake wakati wakidai walikuwa waaminifu! Pili! ni wazi kuwa hawatatimiza lengo la sheria! Wamepinga njia ile ambayo inawawezesha kufika kisiwani huko! Mwenye kutoa sheria anaeleza zaidi, “Nilitengenza Mpango wa Kwanza kukuonyesha huna uwezo kutimiza lengo la sheria yangu! Nilitaka utambue kuwa haifai kuumini uwezo wako wala kujitumainia ukifikiri unaweza kutimiza lengo la sheria yangu kwa juhudi yako, unakosea sana! Nilitoa Mpango wa Kwanza ili kukutayarisha na kukuleta kwenye njia yangu ya kukuokoa!” Kama ilivyoandikwa, “Lakini kabla ya kuja ile IMANI tulikuwa tumewekwa chini ya sheria, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa, Hivyo TORATI IMEKUWA KIONGOZI KUTULETA KWA KRISTO, ili tuhesabiwe haki kwa imani, lakini, iwapo imani imekuja, HATUPO TENA CHINI YA SHERIA KAMA KIONGOZI”. (Wagalatia 3:23-25).

Lakini hata hivyo wengi wanakataa na wanapinga Neno la Mungu kwao. Imeandikwa, “mwisho (au lengo la) wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki.” (1 Tim.1:7). Lakini hao wanakataa kwenda njia ambayo Mungu ameweka mbele yao kutimiza lengo Lake, na wanabaki kama inavyosema katika mstari wa 7, “Wengine wakiyakosa hayo wamegeukia maneno ya ubatili; WAPENDA KUWA WAALIMU WA SHERIA, INGAWA HAWAYAFAHAMU WASEMAYO WALA MAMBO YALE WAYANENAYO KWA UTHABITI.” (1 Tim.1:8). Kumbe! Kwa ‘kushika sheria ya Agano la Kale’, wanakosa kabisa lengo la sheria ile ile! Huo ni udanganyifu na hiyo ni hali ya upofu!

Paulo alitangaza, “Maana mimi kwa njia ya sheria NALIIFIA SHERIA ili NIMWISHIE MUNGU. Nimesulibiwa pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu…Siibatili neema ya Mungu; maana, ikiwa haki hupatikana kwa njia ya sheria, basi Kristo alikufa bure.” (Wagal.2:19-21).

                                               ————————————–

Yesu alitangaza, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza” (Mathayo 5:17). Unafikirije? Ina maana lazima tutahiriwe siku hizi? Je, inamaanisha lazima tuchinje mbuzi na mafahali kila mwaka kwa ajili ya dhambi zetu? Je! ina maana tunapaswa kushika kila kilicho andikwa kwenye torati? Hapana! Neno la Mungu linasema, ‘Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo.” (Yoh.1:17). Maneno hayo yanawakilisha mabadiliko makubwa sana! Paulo anatueleza kwamba, “…MWISHO wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki” (1 Tim.1:5). Lile neno ‘mwisho’ katika mstari huo lina maana pia ‘tekelezo’ au ‘utimilifu’ kwa lugha ya asili ya Agano Jipya (Kigiriki). Sheria ina lengo au shabaha. Lengo hili linatokana na kusudi la Mungu la mwanzoni, yaani, tuwe wenye haki na watakatifu katika upendo (Waefeso 1:4). LAKINI, kwa sababu ya dhambi, sheria haikuweza kutupeleka tutekeleze lengo hili! Kristo Yesu mwenyewe anawakilisha ‘mwisho’ wa sheria yaani, anawakilisha utekelezo na utimilifu wa sheria ndani Yake mwenyewe. Sawasawa na tabia yake Yesu ni Mwenye Haki, ni matakatifu, ni mwenye upendo. Yesu hahitaji kujaribu KUFIKA lengo au kusudi la Torati – yeye mwenyewe anawakilisha kwa tabia yake ile hali ya haki, ya utakatifu na ya upendo ambao sheria ilituelekezea! “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yoh.14:9).  Kwa hiyo Yesu, anawakilisha ‘mwisho’ au ‘utimilifu’ wa sheria. Na kama ‘mwisho’ au ‘utimilifu’ wa sheria umeshakuja, yaani Yesu Kristo, sheria haihitajiki tena! Tunahitaji kuzaliwa toka juu na kupokea Roho Mtakatifu.

Kwa hiyo imeandikwa “Kwa maana Kristo ni mwisho wa sheria, ili kila aaminiye ahesabiwe haki.” (Warumi 10:4). Zaidi ya hayo imeandikwa, “kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.” (Warumi 5:19). Na tena, “Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye.” (2 Wakor.5:21). Yaani, kwa imani katika Kristo Yesu tunahesabiwa haki; pia tunazaliwa mara ya pili toka juu, yaani ‘tunapata kuwa haki ya Mungu katika Yeye.’!

Yesu Kristo hutubatiza katika Roho Mtakatifu ili tupate maisha Yake ndani yetu! “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine ili akae nanyi hata milele, ndiye Roho wa kweli …ninyi mnamtambua maana anakaa kwenu naye ATAKUWA ndani yenu, Sitawaacha ninyi yatima, NAJA KWENU….Siku ile ninyi mtatambua ya kuwa mimi ni ndani ya Baba yangu, NANYI NDANI YANGU, NAMI NDANI YENU.” (Yoh.14:16-20). Hiyo ndiyo Injili! Unaona hiyo siyo dini. Hayo ni zaidi sana ya maagizo nje yetu! Yeye aliye ndiye ‘utimilifu wa sheria’ kwa tabia yake yenyewe, Yesu Kristo, ni Yeye ajaye kukaa ndani yetu ili haki itimizwe ndani yetu kupitia maisha Yake ndani yetu! Kwa hiyo, Yohana anasema, “atendaye haki yuna haki, kama Yeye alivyo na haki…Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu.” (1Yoh.3:7; 4:17). Huo ndio wokovu mkuu sana! Na kwa hiyo inasema, “Basi tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii?” (Waebr.2:3). Kwa kweli ni wokovu mkuu upitao akili zote!

Yesu Kristo mwenyewe ni tekelezo (mwisho) wa sheria na sisi tunaingia katika utimilifu huyo kupitia Kristo, kwa imani, na kwa Roho Mtakatifu! “Maana katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili. Na ninyi MMETIMILIKA KATIKA YEYE aliye kichwa cha enzi yote na mamlaka.” (Wakolosai 2:9,10). Yatafakari mambo hayo; ulishwe na ukweli huo! Na uishi kwa ukweli huo!

Kama mtu anafikiri maneno ya Yesu, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” yanamaanisha kwamba lazima wakristo washike torati, haelewi Injili wala wokovu wa Mungu katika Kristo Yesu, wala maneno ya Yesu! Mtu yule ni kama wale ambao “wapenda kuwa waalimu wa sheria, ingawa hawayafahamu wasemayo wala mambo yale wayanenayo kwa uthabiti.” (1 Tim1:7). Tulisoma kwamba Yesu alikufa msalabani “…ili haki ya torati ITIMIZWE ndani yetu sisi…” Na sisi tumepewa Roho Mtakatifu ili kulitimiza lengo hili. Imeandikwa, “Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria… Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Warumi 13:8; Wagal.5:14). Na Mungu amefanya hiyo kuwezekana kupitia Roho Mtakatifu, kama ilivyoandikwa “kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi.” (Warumi 5:5). Na kwa sababu ya hiyo, tunaweza kupendana kweli kweli na kutimiza haki kutokana na yale Mungu aliyoyafanya NDANI YETU – badala ya kujaribu kwa uwezo wetu tu kuishi kwa maneno yaliyoyaandikwa katika vibao vya mawe ambayo yapo nje yetu!

                                               ————————————–

Kama ukielewa mambo hayo, umeshatambua ya kwamba Agano Jipya siyo jambo la kupata Roho Mtakatifu ili wewe uweze ‘kuishi kwa torati’ wala ‘kuwa chini ya torati’ wala ‘kushika torati ya Musa.’ Kupitia Agano Jipya sisi huzaliwa mara ya pili toka juu, sisi huzaliwa na Mungu, sisi hutokana na Mungu, na tunaishi siyo kwa sheria bali kwa uzima ule ambao Mungu ameweka ndani yetu! Kama ilivyoandikwa, “kutahiriwa si kitu, wala kutokutahiriwa, bali KIUMBE KIPYA” na tena, “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya, Lakini vyote pia vyatokana na Mungu.” (Gal.6:15; 2kor. 5:17,18). Na Petro anatangaza, “Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa WASHIRIKA WA TABIA YA UUNGU…” (2Petro 1:4).

Agano Jipya kwa msingi siyo jambo la ‘maneno’ bali la nguvu, la Roho, la Uzima! “Maana ufalme wa Mungu hauwi katika maneno, bali katika nguvu.” (1 Wakor 4:20). Paulo anasema, “Naye ndiye aliyetutosheleza kuwa wahudumu wa Agano Jipya; si wa andiko, bali wa Roho; kwa maana andiko huua, bali roho huhuisha.” Yaani, ukiishi kwa torati, yaani, kwa maneno yaliyoandikwa ‘nje’ yako, yatakuua. Lazima kuzaliwa na Roho wa Mungu na kuwa mhudumu wa Roho! “Ninyi ndinyi barua yetu … mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama.” (2 Wakor.3:2,3). Amen! Kama wewe ni mhudumu wa andiko tu, unawaua watu wa Mungu kiroho! Na kosa kubwa la ‘mafundisho ya torati’ yanawadanganya watu wasibatizwe na Roho Mtakatifu na yanawazuia watu kuishi kwa Roho Mtakatifu!

Siandiki maneno hayo kwa sababu napenda kushindana na watu! La hasha! Kwa upande moja, napenda kuondoa utata juu ya mada hii. Kwa upande mwingine inanihuzunisha sana, kwani baadhi ya watu wanadanganywa pasipo kutambua inatokeaje. Inanihuzunisha mno, kwa sababu – kadiri ninavyojua – baadhi ya watu hao wanaheshimu sana Biblia na wanataka kuishi maisha ya utakatifu, lakini bila kuelewa wafanyalo! Ndiyo maana Paulo aliandika juu ya Wayahudi “Ndugu zangu … nawashuhudia kwamba wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa. Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe, hawakujitia chini ya haki ya Mungu, kwa maana Kristo ni mwisho wa sheria, ili kila aaminiye ahesabiwe haki.” (Warumi 10:1-4). Ni matumaini yangu na dua yangu kuwa hata mmoja ataguswa moyoni mwake kwa somo hili na Mungu afunguke macho kuuona wokovu ule ambao uko ndani ya Kristo Yesu!

                                               ————————————–

Sasa tusemeje! Torati ni mbaya? Hapana! Sasa kwa nini Torati/sheria iliwekwa? Sababu ziko wazi,

“Basi twajua ya kuwa mambo yote inenayo torati huyanena kwa hao walio chini ya torati, ili kila kinywa kifumbwe, na ulimwengu wote uwe chini ya hukumu ya Mungu; kwa sababu hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki mbele zake kwa matendo ya sheria; kwa maana kutambua dhambi huja kwa njia ya sheria. Lakini sasa, haki ya Mungu imedhihirika pasipo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii, ni haki ya Mungu iliyo KWA NJIA YA IMANI KATIKA YESU KRISTO kwa wote waaminio.”(Warumi 3:19-22).

Torati iliwekwa ili KUTUONYESHA NA KUTUDHIHIRISHA sisi tu wenye dhambi chini ya hukumu ya Mungu – torati haikuweza kutuokoa na dhambi! “Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na Wayunani ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi.” (Warumi 3:9). Kwa mafundisho hayo tunaelewa kuwa Torati haiwezi kutuokoa kutoka katika dhambi na kutufanya tuwe wenye haki! Ilipewa kutudhihirisha kutokuweza kwetu kutimiza haki ya Mungu!

Hapo Paulo anaongelea lengo la sheria tu lakini tusisahau maneno ya Yesu juu ya Roho Mtakatifu, yaani, “Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu KWA HABARI YA DHAMBI, na haki, na hukumu” Kwa hiyo ina maana kwamba siku hizi, dhambi haitambuliwi kwa njia ya sheria tu, bali kwa kazi ya Roho Mtakatifu! Sasa kwa nini baadhi ya watu wanashitakiwa na dhamiri zao kuhusu dhambi? Kwa sababu wanavunja sheria? Yesu anaendelea kutufundisha “Kwa habari ya dhambi KWA SABABU HAWANIAMINI MIMI.” (Yoh.16:8,9). Kwa hiyo Wayahudi walipomwuliza Yesu,“Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu? Yesu alijibu, “Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye.” (Yoh.6:28,29). Na tena, “Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyemwamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu HAKULIAMINI jina la Mwana pekee wa Mungu.” (Yoh.3:18). Pasipo kumwamini Yesu, haki ya Torati haiwezi kutimizwa ndani yetu, hivyo dhambi ya kuu ni kutokuamini!

Yesu aliendelea kueleza juu ya huduma ya Roho Mtakatifu: “atauhakikisha ulimwengu KWA HABARI YA HAKI..…” Kwa nini? Je. kwa sababu watu huvunja sheria? Hapana! Bwana Yesu anatuambia kwa wazi, “kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala HAMNIONI TENA.” Yesu Kristo ndiye ile haki ya Mungu mwenyewe ya milele. Sikiliza maneno ya ajabu sana “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu. Yeye kwa kuwa ni mng’ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake…” (Waebr.1:1-30). Basi, kwa upande moja tunaweza kusema Yesu sasa ni kile ‘kipimo’ cha haki, yeye ni mng’ao wa utukufu wa Mungu. Na sasa kupitia Yesu Kristo sisi kupata kuwa washirika wa tabia Yake, ya Uungu. “Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi” (Wakor.1:30) ‘Uzima wa milele’ siyo jambo la muda, ni jambo la hali ya kiroho, hali ya tabia – ni Mungu mwenyewe! “Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake.” (Yoh.5:26). Kwa hiyo Mungu hakuweza kutupa uzima wa milele bila kutupa Yeye mwenyewe, bila kutupa Roho Yake. Baba na Mwana wanao ‘Uzima’. Kwa sababu ya kifo na ufufuo wa Yesu sasa, “Mungu alitupa uzima wa milele…”. Lakini na tuelewe kwa kina sana, “…na uzima huu UMO KATIKA MWANAWE. Kina cha wokovu wetu kinadhihirishwa na maneno yafuatayo, “Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu…” (2 Petro 1:4).

Inasema, “Mungu hawezi kusema uongo.” (Waebr.6:18). Je, unafikiri Mungu hasemi uongo kwa sababu anashika sheria fulani? Hapana! Hamna sheria ihusuyo Mungu, kama Biblia inadhihirisha, “sheria haimhusu mtu wa haki” ( 1Tim.1:9). SAWASAWA NA TABIA YAKE Mungu hawezi kusema uongo! Siyo jambo la sheria, ni jambo la tabia, la hali ya kiroho! Na huu ndio msingi wa Agano Jipya! Kwa hiyo Petro anaandika, “ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu.” Ni wazi wakristo wanaendelea kujaribiwa na sisi tunaweza kuchagua kujipendeza / kufanya dhambi, au ‘kukaa’ ndani ya Kristo. Kama ilivyoandika, “mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.” (Waefeso 4:22-24). (Somo hili halihusu moja kwa moja mwenendo wa waumini, majaribu na jinsi ya kuyashinda dhambi, lakini unweza kusikiliza mafundisho juu ya jambo hili kwa kwenda  https://somabiblia.wordpress.com/kuwekwa-huru-mbali-na-dhambi/.)

‘Lengo’ la sheria au ‘mwisho’ wa sheria ni Yesu Kristo! Kwa hiyo watumishi wa Mungu katika Matendo ya Mitume walihubiri ‘Yesu Kristo’, siyo ‘sheria’ (Matendo 8:5,35; 9:20), na Paulo alitangaza, “naliazimu nisijue neno lo lote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulibiwa.” (1 Wakor.2:2). Yesu alikuwa sura ya kweli ya haki ya Mungu wakati alipokuwepo duniani, lakini aliwaambia wanafunzi wake lazima ‘aende zake’ na baada ya ‘kuondoka’ kwake ulimwengu hautakuwa sura hiyo ya haki mbele macho yao. KWA HIYO Roho Mtakatifu ‘atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya haki’ kwa sababu ‘hamnioni tena’! Lakini baada ya hapo Roho Mtakatifu atakapokuja yeye atamtukuza Yesu (Yoh.16:14), yaani, Roho wa Mungu atafanya kazi katika dhamira ya watu juu ya haki ile iliyo ndani ya Kristo Yesu. Kwa hiyo, tunamhubiri Yesu, wala siyo sheria. Ndiyo maana Roho wa Mungu anamtukuza Yesu, wala siyo sheria.

                                               ————————————–

Je, unafikiri Torati ilipewa kukufanya mtakatifu? Sikilize neno la Mungu, “sheria iliingia ili kosa lile liwe kubwa sana; na dhambi ilipozidi, neema ilikuwa nyingi zaidi.” (Warumi 5:20). Maana yake ikiwa unaishi chini ya sheria kosa litazidi kuwa kubwa sana.  Maneno haya yanamaanisha  nini? Je! Mungu anataka tufanye dhambi?  La hasha! Lengo la Mungu pamoja na sheria aliyoitoa ni kuidhihirisha hali ya tabia yetu, yaani, kadiri ya uwezo wetu na hali yetu ya kiroho, sisi hatuwezi kuwa wenye haki kwa undani kama vile Mungu alivyopanga tangu kuwekwa misingi ya dunia. (Huu ni mwanzo lakini baadaye tutaangalia  maisha ya watu walioishi ‘kwa haki’ katika Agano la Kale na maana yake.)  Kumbuka! Kadiri unavyojitahidi kuitii sheria iliyo nje yako, ndivyo nguvu ya dhambi inavyozidi ndani yako! Kwa sababu ya hiyo sheria iliwekwa ili tuelewe kwa undani sana tunahitaji kuokolewa!

Kama ilivyoandikwa  “Kwa maana tulipokuwa katika hali ya mwili, tamaa za dhambi, ZILIZOKUWAKO KWA SABABU YA TORATI, zilitenda kazi katika viungo vyetu HATA MKAIZALIA MAUTI MAZAO.” (Warumi 7:5). Na tena, “Torati ni nini basi? Iliingizwa kwa sababu ya makosa, HATA AJE HUYO MZAO aliyepewa ile ahadi…Lakini andiko limeyafunga yote chini ya nguvu ya dhambi, MAKUSUDI hao waaminio wapewe ile ahadi KWA IMANI ya Yesu Kristo. Lakini KABLA YA KUJA ILE IMANI TULIKUWA TUMEWEKWA CHINI YA SHERIA, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa. HIVYO TORATI IMEKUWA KIONGOZI KUTULETA KWA KRISTO, ili tuhesabiwe haki kwa imani Lakini iwapo imani imekuja hatupo tena chini ya kiongozi.” (Wagal 3:19, 22-25).

Kwenye 1 Wakor.15:56 Paulo anatangaza, “Uchungu wa mauti ni dhambi, na NGUVU ZA DHAMBI NI TORATI.” Ina maana kama ukiishi kadiri ya torati, unaongeza nguvu ya dhambi katika maisha yako, utakuwa mfungwa wa dhambi! Sasa, ni nani anayetaka kuishi chini ya sheria? Ni nani anayependa kutoa dhambi nguvu katika maisha yake? Ni nani anayetaka kukataa wokovu wa Bwana? Kwa upande mwingine, Paulo anamshukuru Mungu akisema katika mstari ufuatao, “Lakini Mungu na ashukuriwe atupaye KUSHINDA kwa Bwana wetu Yesu Kristo.”

Kwa mjibu wa fundisho la Biblia, Torati iliwekwa ili ituonyesha sisi ni mwenye dhambi na dhambi ina nguvu katika maisha yetu na sisi wenyewe hatuna uwezo wa kutimiza HAKI YA MUNGU katika maisha yetu. KWA HIYO mtu akisema, “Mimi ninaishi chini ya sheria”, ina maana sawasawa na mafundisho ya Agano Jipya, yeye anampinga Mungu; yeye anajitukuza mbele ya Mungu; yeye anajidanganya! Kwa nini? Kwa sababu kwa maneno hayo ni kama anasema, “mimi mwenywe, kwa uwezo wangu binafsi, naweza kuyatii maagizo ya Mungu, naweza kuwa mwenye haki!” Na kutokana na mafundisho ya Agano Jipya, Sheria au Torati ni jambo la nje yetu ambayo inahusika na UWEZO WETU wenyewe  – ambao hautoshi kabisa kutimiza haki ya Mungu kwa sababu ya hali yetu ya kiroho, (Warumi 5:12; Waefeso 2:1,2). Agano Jipya na imani kwa Yesu INAHUSU UWEZO WA MUNGU NDANI YETU kutufanya wenye haki na kutimiza haki ya Mungu ndani yetu! (War 5:19; 8:4; 2 Wakor.5:21; 1 Pet 4:17,18). Kwa hiyo katika Agano Jipya hamna usemi usemao – ‘tupo chini ya sheria’ au ‘lazima tushike torati’ au ‘tunaishi kwa sheria’. Kusema hivyo ni kuupinga mpango wa Mungu wa Ukombozi wa mwanadamu! Kinyume chake, imeandikwa, “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria.” (Wagal.4:4).

                                               ————————————–

Ili kutumiza haki ya Mungu katika maisha yetu, kwanza ni lazima hali ya kiroho yetu ibadilike! (Ebr. 10:1-4). Na sheria haiwezi kuibadilisha hali yetu ya kiroho! Kwa hiyo katika Agano Jipya lugha hiyo inatumiwa, “kwa sababu hamuwi chini ya sheria, bali chini ya neema.” (Warumi 6:14), “Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria.” (Wagal.5:18), “Bali sasa tumefunguliwa katika torati, tumeifia hali ile iliyotupinga, ili sisi tupate kutumika katika hali mpya ya roho, si katika hali ya zamani, ya andiko.” (War 7:6).

Kama nilivyosema, sheria ni jambo la ‘andiko’ nje yetu – haiwezi kubadilisha hali ya mwenye dhambi. Injili ya Agano Jipya ni jambo la Roho wa Mungu ndani yetu! Kama torati ya Musa iliyoandikwa katika vibao vya mawe ingaliweza kubadilisha hali ya watu, Mwana wa Mungu Kristo Yesu asingelikufa msalabani! Kama ilivyoandikwa, “Torati haipatani na ahadi za Mungu? Hasha! Kwa kuwa, kama ingalitolewa sheria iwezayo kuhuisha, yamkini haki ingalipatikana kwa sheria. Lakini andiko limeyafunga YOTE CHINI YA NGUVU YA DHAMBI, MAKUSUDI hao waaminio wapewe ile ahadi kwa imani ya Yesu Kristo.” (Wagalatia 3:21,22). Torati iliyoandikwa katika vibao vya mawe nje yetu haina uwezo wa ‘kuhuisha’, yaani kutupa ‘Uzima’, kwa hiyo haki haipatikani kwa sheria bali kwa imani katika Yesu Kristo! Kwa mfano! Kama nikimwagiza nyoka, “Awe kondoo!” yule nyoka anaweza kujitahidi kadiri anavyoweza awe kondoo lakini hataweza kulitimiza agizo langu kamwe! Kwa sababu hawezi kuibadilisha hali ya tabia yake, ingawa nyoka anaweza kujaribu kula majani; anaweza kujaribu ‘kusimama’; anaweza kujitahidi kwa kadri awezavyo lakini atabaki kuwa nyoka. Kumbe! Njia ni mmoja tu – kumsulibisha na kumfanya kiumbe kipya! Halelluya! Mwana wa Mungu Kristo yesu hakufa ili ‘kutuboresha’, bali alikufa ili kutusulubisha.

Sikiliza maneno ya Mwana wa Mungu: “Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye.” (Yoh.3:14,15)  Hamna njia ya kuokoa au kuboresha ‘utu wetu’ isipokuwa  kuusulubisha utu wetu! Biblia iko wazi na ya ajabu! “Mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, TUSITUMIKIE DHAMBI TENA”. Na kama tulivyoona, Paulo alitangaza, “Nimesulibiwa pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali KRISTO YU HAI NDANI YANGU; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu.” (War. 6:6; Wagal. 2:20).

Wale wanaojitahidi kwa ajili ya sheria, wanajifanya vipofu juu ya ukweli huo huo hapo juu na wanawazuia wengine wasiijue nguvu wa Kristo ndani ya maisha yao, wanawapotosha wengine wasitimize amri za Mungu! Sikiliza Paulo, “Hata imekuwa mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya lakini vyote pia vyatokana na Mungu.” (2 Wakor.5:17,18).

Torati iliyoandikwa katika vibao vya mawe ilishindwa kuibadilisha hali yetu ya kiroho, kwa hiyo Mungu alimtoa Mwanae wa pekee afe kwa ajili yetu! Kwa hiyo ni lazima mtu azaliwe mara ya pili, (kuzaliwa na Mungu) yaani, kufanywa kiumbe kipya! Badala ya kuifuata sheria iliyo nje yetu kwa uwezo wetu ambao hautoshelezi kabisa, kupitia kifo cha Mwana wa Mungu, kwa uweza wa Mungu utu wetu wa kale umesulubishwa pamoja na Yesu, ili tusitumikie dhambi tena! Zaidi ya hayo, Yesu alimwagika damu yake msalabani ili tupokee Roho Mtakatifu! Sasa siyo jambo la maagizo yaliyoandikwa nje yetu, lakini kupitia Roho wa Mungu anaweka ‘sheria’ zake katika nia zetu, na katika mioyo yetu! (Waebr.8:7-10). Kwa Roho Mtakatifu Yesu mwenyewe anakuja kuishi ndani yetu! (Yoh 14:15-20, Wagal.2:20, Kol 1:27). Ni kwa ‘imani’ kwani imani inahusu uwezo wa Mungu ndani yetu; wakati kuishi kwa ‘torati ya Musa’ ina maana unaishi kwa uwezo wako tu ambao hautoshi kabisa. Wale wanaoishi kwa imani wanamtukuza Mungu (Ebr 11:6) na wale wanaoishi kwa kuifuata torati wanapinga kusudi la Mungu – kama ilivyokuwa siku za Paulo, ni vivyo hivyo siku hizi.

“Tuseme nini, basi? Ya kwamba watu wa Mataifa, wasioifuata haki, walipata haki; lakini ni ile HAKI ILIYO YA IMANI; bali Israeli wakiifuata sheria ya haki HAWAKUIFIKILIA ILE SHERIA. Kwa sababu gani? Kwa sababu HAWAKUIFUATA KWA NJIA YA IMANI, bali kana kwamba KWA NJIA YA MATENDO. Wakajikwaa juu ya jiwe lile likwazalo…” (Warumi 9:30-32).

Ni vilevile juu ya wao wote  wanaojitahidi kwa ajili ya torati siku hizi! Ni kama nilivyosema hapo juu kupitia mfano wangu. Lengo la torati inabaki lile lile (yaani, haki, upendo na uzima), lakini njia ya kulitimiza lengo hili imebadilika! Paulo anaenedelea kueleza juu ya wao wanaotaka kushika sheria ya Musa, “Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe, HAWAKUJITIA CHINI YA HAKI YA MUNGU. Kwa maana KRISTO ni mwisho wa sheria, ili kila aaminiye ahesabiwe haki. Kwa maana Musa aliandika juu ya haki itokayo kwa sheria ya kuwa, Mtu afanyaye hiyo ataishi kwa hiyo.” (Warumi 10:3-5).

Unaona jinsi neno la Mungu lililivyo wazi! Wao wanaojaribu kuishi kwa kuifuata sheria ya Musa hawajitii chini ya haki ya Mungu! Wanafikiri ni waaminifu lakini kwa msingi wanataka kuithibisha haki yao wenyewe na wanakosa kabisa kutimiza amri za Mungu. Kama nilivyosema katika somo hili, kwa sababu ya hiyo, wakristo hawatumii usemi “tupo chini ya sheria”, kwa sababu Agano Jipya linatangaza ‘hatuwi chini ya sheria’!

                                               ————————————–

Lakini wanaendelea kutokujali mistari hiyo yote katika somo hili na wanajitahidi kutafuta tafuta mistari yo yote inayoweza kuthibitisha udanganyifu wao. Kwa mfano, wananukuu, “Naye azishikaye amri zake hukaa ndani yake yeye naye ndani yake” (1 Yoh.3:24). Na kudai, “Unaona! Lazima kushika sheria!” Lakini ni wazi mstari huo hauhusiki na jambo la kushika torati au kuishi ‘chini ya torati’. Ni nani azishikaye amri za Mungu? Ni yule anayekaa ndani ya Yesu na Yesu naye ndani yake! Yeye anaweza kuitimiza amri ya Mungu kwa sababu, kama Yohana alivyoandika katika sura ile ile, “Kila akaaye ndani yake hatendi dhambi.” (1 Yoh.3:6). Unaona!, Anasema yeye AKAAYE NDANI YA KRISTO hatendi dhambi. Ina maana tunatimiza amri za Mungu, na siyo kuishi kwa sheria ya Musa wala kuishi kwa ‘sheria’ fulani mpya iliyo nje yetu, bali kwa sababu Yesu Kristo amekuja kuishi ndani yetu! Haki haitokani na jitihadi yangu ya kuishi sawasawa na sheria yo yote iliyo nje yangu, bali kwa sababu nimezaliwa na Mungu! Mungu apewe sifa! “Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao wake WAKAA NDANI YAKE; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu.”(1 Yoh.3:9). (Vipi wale wanaoishi chini ya sheria wanavyoweza kutusingiza kwamba tunatoa ruksa kwa watu kutenda dhambi! Je! hawajasoma kuhusu nguvu wa Mungu jinsi inavyotuokoa na dhambi?).  Yohana anaendelea kueleza tunashindaje, “Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo IMANI YETU.” (1Yoh.5:4).  Tatizo, wengi wao wanaojitahidi kwa ajili ya ‘sheria’ hawawezi kuelewa tunawezaje kumtii Mungu pasipo kuishi kwa kushika ‘sheria’, yaani, kuishi ‘chini ya torati’ ya Musa. Wanafikiri mara usemapo ‘hatuwi chini ya sheria’ wanafikri tuna maana siyo lazima kumtii Mungu! Tena wananukuu mstari kama huu “Mkinipenda, mtazishika amri zangu.” (Yoh.14:15). Kwa kufanya hivyo, wanaweka wazi hawaelewi Agano Jipya; hawaelewi utofauti kati ya kuishi ‘chini ya sheria’ (iliyo nje yetu) na kuishi kwa imani na kuzishika amri za Bwana (kupitia neema na uzima wa Bwana ambao umewekwa ndani yetu.) Labda tungejaribiwa kusema ni jambo la maneno tu – kimsingi hamna utofauti kati ya imani yetu na imani yao! Lakini kama ilivyokuwa siku za Paulo, vivyo hivyo hata siku hizi. Wale  wanaotaka kushika sheria hawaelewi Agano Jipya, na mafundisho yao yanatengenza ‘injili nyingine’, kama Paulo alivyoandika. Walimshtaki wakisema ‘anawaruhusu watu wanaweza kufanya dhambi, na wanatushtaki vivyo hivyo siku hizi.

Na wanaendelea kutafuta tafuta mistari, lakini kwa sababu mafundisho yao hayapo katika Agano Jipya ni lazima wachague mistari bila kujali muktadha ambayo hauhusiki na mada yetu! Na hakika huo ni udanganyifu. Wamejifanya vipofu juu ya mambo yale yaliyo wazi! Kwa mfano, wanataja mistari kama Matendo 13:14, 16:3,17:2. Hasa huu (Mstr 13:14) unaosema, “Lakini wao wakatoka Perge, wakapita kati ya nchi, wakafika Antiokia, mji wa Pisidia, wakaingia katika sinagogi siku ya sabato, wakaketi.” Sasa, sijui kwa nini baadhi yao wananukuu mistari hiyo! Haihusu mada yetu! Haihusu makusanyiko ya wakristo, ya kanisa la Bwana Yesu! Mistari ile inahusu kuhubiri kwa Injili kwa wale wasiompokea Yesu kama Mwokozi wao! Katika sura ile ile ya 13 tunasoma kuwa Paulo na Barnaba walipelekwa na Roho Mtakatifu kuhubiri Injili! Na Paulo anatangaza kwenye Warumi 1:16, “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa MYAHUDI KWANZA, na kwa Myunani pia.” Na tunajua Paulo alichukua mzigo mzito sana kwa ajili ya Wayahudi, kama alivyosema,  “ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili; ambao ni Waisraeli…”. (Warumi 9:3,4) Basi, hatushangai kama anatumia fursa kuhubiri Kristo siku ile ile na mahali pale ambapo Wayahudi hukusanyika kila juma, yaani,kuingia katika sinagogi siku ya sabato! Kama Paulo alivyosema, “Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili NIWAPATE WAYAHUDI; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate walio chini ya sheria.” (1 Wakor.9:20). Hiyo ni jambo la kuhubiri Injili, haihusu siku ile ambayo Wakrsito walikusanya! Kama nilivyosema, wananukuu mistari bila kufikiri, bila kujali muktadha  Mara wanapoona neno ‘sabato’ au ‘sheria’ katika Agano Jipya wanafikire wameshinda – haijalishi muktadha ni ya namna gani!

Kadhalika, baadhi yao pia wananukuu Yak 4:11, “Ndugu, msisingiziane; amsingiziaye ndugu yake, au kumhukumu ndugu yake, huisingizia sheria na kuihukumu sheria. Lakini ukiihukumu sheria, huwi mtenda sheria, bali umekuwa hakimu.” Mstari huo pia hautufundishi lazima tuishi chini ya sheria au kwa sheria ya Musa! Anatufundisha kama vile Bwana Yesu alivyotufundisha, “Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi”, naye anathibitisha mambo yale Yohana aliyoyaandika, “Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi (au ‘kuvunja kwa sheria’).” (Yoh.3:4). Yakobo hatusisitizi kuishi kwa sheria! Yakobo mwenyewe anatusisitiza, “SEMENI ninyi, na KUTENDA kama watu watakaohukumiwa kwa sheria YA UHURU”; siyo kwa ‘sheria ya Musa’ au ‘kwa torati’! (Yak.2:12). Sheria ya uhuru ni nini? Biblia inafafanua! “Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi….Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli” (Yoh.8:34-36).  Kupitia Yesu Kristo na wokovu wake tumewekwa huru tusiwe watumwa wa dhambi tena!

Yesu Kristo anafanya hivyo kwa kutubatiza sisi kwa Roho Mtakatifu! “Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha HURU, mbali na sheria ya dhambi na mauti.” Tumewekwa huru mbali na dhambi na maagizo wa sheria yatatimizwa ndani yetu siyo kwa kuishi kwa maneno yaliyoyaandikwa nje yetu, bali kupitia uzima wa Yesu ndani yetu kwa Roho Mtakatifu!

Yakobo anatufundisha pia kuwa, “Lakini aliyeitazama SHERIA KAMILIFU ILIYO YA UHURU, na KUKAA HUMO, asiwe msikiaji msahaulifu, bali MTENDAJI WA KAZI huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.” (Yak.1:25). Hamna neno la kuishi kwa torati ya Musa!  Anatusistiza tukae katika sheria ya uhuru, vivyo hivyo Paula aliwasistiza Wagalatia “Kristo alitupa uhuru, akataka tubaki huru. Hivyo simameni imara wala msikubali tena kulemewa na kongwa la utumwa.” (Wagalatia 5:1). Paulo aliyaandika maneno hayo kwa sababu Wagalatia walitaka kurudi kuishi kwa sheria! Na tena Yakobo anatumia lugha ifuatayo, “Lakini mkiitimiza ile SHERIA YA KIFALME kama ilivyoandikwa, Mpende jirani yako kama nafsi yako, mwatenda vema.” (Yak.2:8). Paulo anafundisha vilevile, “Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo. Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako. Lakini mkiumana na kulana, angalieni msije mkaangamizana. Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili.” (Wagalatia 5:13-16). Ni wazi kama Wakristo tunao uhuru wa kumfuata Yesu au kujipendeza, lakini ni kwa njia gani tunaishi katika haki na utakatifu? Au Kwa kushika sheria?. Ni kwa kuishi kwa Roho Mtakatifu – ‘‘enendeni kwa Roho’! Sasa tunaweza kumpenda jirani yetu siyo kwa kushika torati bali “kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi.” (Warumi 5:5). Unaona, maagizo, yaani haki ya torati hutimizwa ndani yetu kwa sababu mambo yale ambayo Mungu amefanya ndani yetu kupitia kifo na ufufuo wa Mwanae wa pekee na kwa kutupa Roho Mtakatifu!

(Sheria kamilifu iliyo na uhuru, na sheria ya kifalme, na sheria ya uhuru ambayo Yakobo anaitaja, hiyo yote ni matokeo ya kazi ya Mungu ndani yetu kwa kutujaza na Roho Mtakatifu, na kumimina pendo la Mungu ndani ya mioyo yetu kwa Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi. Kama alivyosema mtume Paulo, “kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu, imeniacha huru bali na sheria ua dhambi na mauti.” Vilevile Paulo anaposema “mchukuliane mizigo na kuitimiza hiyo sheria ya Kristo’.” (Wagalatia 6:2) – hiyo sio sheria mpya ya inje bali ni pendo la Kristo ndani yetu ambalo linafanya kazi wakati wote, ili tuwapende wengine.

Paulo alitangaza “Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu bali mwenye sheria mbele za Kristo) ili niwapate hao wasio na sheria.” (1Kor 9:21). Anaposema bali mwenye sheria mbele ya Kristo, hapo tena haina maana kuwa ni sheria mpya ya inje, bali hapo anaeleza juu ya ukweli ule ule ambao alifundisha katika Warumi 6:15. “Ni nini basi, tufanye dhambi kwa sababu hatuwi chini ya sheria bali chini ya neema? Hasha!” Baada ya kusema ‘nalikuwa kama sina sheria’ yeye hataki watu wafikiri ina maana tunaweza kufanya dhambi, kwa sababu, kama tulivyoona, walikuwapo watu ambao walimsingizia juu ya jambo hili (Warumi 3:8). Kimsingi, sheria ya Kristo siyo maandiko nje yetu bali ni Roho wa Kristo Yesu ndani yetu – ‘sheria’ ya Kristo kimsingi haitofautiani na tabia ya Kristo, na kwa hiyo lazima mtu azaliwe mpya!)

Adam alifanya dhambi. Mara moja alianguka gizani, mautini na katika nguvu ya shetani – ni ‘sheria’ (Warumi 5:12; Waefeso 2:1,2; Matendo 26:18), sheria ya dhambi na mauti! Sheria ya dhambi na mauti inatufanya watumwa wa dhambi. Sasa, sheria ya Musa iliyoandikwa katika vibao vya mawe haiwezi kutuokoa kutoka katika hali hiyo! Yesu Kristo aliziondoa dhambi zetu na aliiharibu nguvu ya shetani pale msalabani (Yoh.1:29; Waebr.2:14; Wakolosai 2:13-15), na “kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa” (Waebr.10:14). Alifanya hayo (na zaidi!) “ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, TUPATE KUPOKEA AHADI YA ROHO kwa njia ya imani.” Sheria ya Roho wa Uzima inatokana na mambo yale Yesu Kristo aliyoyafanya msalabani! Matokeo ya kifo na ufufuo wa Yesu Kristo yanatuletea sheria ya Roho wa Uzima ambayo yanatuweka huru mbali na dhambi! Shetani hawezi kuyabadilisha au kuyaharibu mambo yale Yesu Kristo aliyoyafanya msalabani! Ni ‘sheria’! Lakini siyo ‘sheria mpya ya MAAGIZO’ bali ni ‘sheria ya kiroho’, ni ‘nguvu ya Roho’, ni ‘uzima wa Yesu ndani yetu’ ambao – sawasawa na maneno ya Yohana – ‘hauwezi kufanya dhambi’.Yakobo, Yohana na Paulo wanakubaliana. Ni fundisho mmoja tu! Biblia ni mmoja. Hamna mabishano! – Halelluya!

Tuendeleeni…

Kadhalika, baadhi yao wananukuu, “Kwa maana katika torati ya Musa imeandikwa, Usimfunge kinywa ng’ombe apurapo nafaka. Je! Hapo Mungu anangalia mambo ya ng’ombe? Au yamkini anena hayo kwa ajili yetu? Naam, yaliandikwa kwa ajili yetu…Ikiwa sisi tuliwapandia ninyi vitu vya rohoni, je! ni neno kubwa tukivuna vitu vyenu vya mwilini?’’ (1 Wakor.9:9-11). Tena tunaona kwenye mistari hiyo Paulo hafundishi lazima tuishi ‘chini ya sheria’ bali anatafsiri maneno hayo kutoka Agano la Kale ili kutufundisha ukweli wa kiroho, yaani, ni jambo la haki kuwasaidia watumishi (na MAHITAJI yao) ambao Mungu aliwatumia kutubariki!

Kadhalika, baadhi yao wananukuu Mathayo 19:18 – Mtu mmoja alimwuliza Yesu, “Mwalimu, nitende jambo gani jema, ili nipate uzima wa milele?” Na Yesu alimwambia, “ukitaka kuingia  katika uzima, zishike amri. Akamwambia, Zipi? Yesu akasema, Ni hizi, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, Waheshimu baba yako na mama yako, na Mpende jirani yako kama nafsi yako” Sasa je, siku hizi kama mtu akikuuliza ‘afanye nini apate uzima wa milele’, Je! Utamjibu, “Azishike amri za Mungu” au utajibuje? Mazungumzo hayo hapo juu yalitokea KABLA YA KUFA YESU msalabani! Ukisoma nyaraka za matendo ya mitume huwezi kupata ni wapi mitume walipohubiri Injili ya Yesu Kristo kwa maneno ya “Shikeni sheria ya Musa nanyi mtapata uzima wa milele!” Badala yake tunasoma,  “Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka?  Wakamwambia,  Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako.” (Matendo 16:30,31). Au kwa nini Yesu alikufa kama watu wanaweza kutumiza haki ya torati bila uzima wa Yesu ndani yao? Kwa msingi Agano la Kale liliendelea mpaka Yesu alimwagika damu yake msalabani na lile pazia la hekalu lilipasuka – kutoka hapo Injili hutangazwa!

Fungu lingine ambalo wananukulu ni katika kitabu cha Isaya sura ya 66 na mstari 23. Tena inaonyesha kwamba hawajali na wanapuuza kabisa muktadha/mazingira ya maandiko. Hasa kama mstari unaonyesha neno ‘sabato’, kumbe, wanafikiri kuwa wanaweza kuthibitisha kauli yao, kuwa wamewashinda wengine! Labda niseme kwa ufupi na kwa urahisi, katika  mstari 15-24, inaonekana kuwa na unabii juu ya wakati ujao. Ni ngumu kusema maneno hayo ni halisi (literal) kabisa; inawezekana kwa kiasi kuwa kama alama/mithali/mfano (symbolic/figurative) wa ukweli. Hata hivyo, sawasawa na lengo la somo langu ni muhimu tu kutambua fungu hili halihusu siku hizi, yaani  siku za neema ya Injili!  Kwa mfano, tunasoma, “Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema Bwana. Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza hao hawatakufa, wala moto huo hauta zimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.” Mistari hii haihusu siku hizi kwa sababu hakuna sehemu mambo kama haya yamewahi kutokea. Bali mistari hii inahusu wakati ujao na maana ya maneno hayo yataelewaka wazi kwa wakati wake! Kwa wakati huo, ni wazi mistari hii haitufundishi kwamba lazima wakristo washike torati ya Musa siku hizi! Na kama mtu akisema inatufundisha hivyo, basi mtu huyo anacheza na maneno tu – inaonyesha wazi kuwa hasomi Biblia kwa makini, wala haliheshimu neno la Mungu. Au Je! anataka kusema kuwa mtume Paulo ni mtume wa uongo? 

                                                ————————————–

Kuhusu (watu wa Mungu) kabla ya Kalvari.

Ibrahimu ameitwa rafiki ya Mungu (Isaya 41:8). Basi Ibrahimu alikuwa ni mtu mkuu sana, lakini tuinasoma kuhusu mambo ya haki  katika Agano Jipya juu ya ukweli ufuatao, “Basi, tusemeje juu ya Ibrahimu, baba yetu kwa jinsi ya mwili? Kwa maana ikiwa Ibrahimu alihesabiwa haki kwa ajili ya matendo yake, analo la kujisifia; lakini si mbele za Mungu. Maana maandiko yasemaje? Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa haki. Lakini kwa mtu afanyaye kazi, ujira wake hauhesabiwi kuwa ni neema, bali kuwa ni deni.” (Warumi 4:1-4). Kama ilivyoandikwa kwenye Mwanzo, “akamwamini Bwana, naye akamhesabia jambo hili kuwa ni haki.”(Mwanzo 15:6).

Katika Agano la Kale watu walikubaliwa  mbele za Mungu pale tu walipoamini rehema, neema na msamaha wake, kama Daudi alivyosema, , “Heri aliyesamehewa dhambi, Na kusitiriwa makosa yake. Heri Bwana asiyemhesabia upotovu, Ambaye rohoni mwake hamna hila.” (Zaburi 32:1,2).

Katika nyakati za kuishi kwake  Ayubu, Mungu angeweza kusema juu yake. , “…hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.” (Ayubu 1:8). Lakini tunapoliangalia hili kwa undani zaidi, Ayubu mwenyewe lazima alikiri kwamba, “Lakini mtu huwaje mwenye haki mbele za Mungu? …Je! Mimi nitamjibuje, Na kuyachagua maneno yangu kuhojiana naye? Ambaye, nijapokuwa mimi ni mwenye haki, nisingemjibu; Ningemsihi-sihi mtesi wangu.” (Ayubu 9:2,14,15).

Musa, Samweli na Eliya walikuwa ni watu wakuu wakati wao wa kuishi, lakini hata hivyo wasingaliweza kuruhusiwa kuingia patakatifu pa patakatifu! Basi kwa hiyo kitu fulani kwa ndani na kikubwa sana kimetukia kwa sababu ya Kalvari, ambacho kumewaosha na kuwatakasa wanadamu kwa namna ya uhalisia ambayo sasa Mungu anaishi nao nakukaa ndani yao! Sisi si ‘wazuri sana’ kuliko watu niliowataja hapo juu kwa sirika, lakini sasa kwa sababu ya Kalvari ambayo haikupatikana kwao wakati wa kuishi kwao, sasa imefanywa ipatikane kwetu sisi.

Na hiyo ndiyo sababu ambayo Yesu alisema “Nami nawaambia, katika wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana; lakini aliye mdogo katika ufalme wa Mungu ni mkuu kuliko yeye.” (Luka 7:28). Ni kwa sababu ya kile ambacho Mungu amekifanya kupitia kifo na ufufuo wa mwanae na lile toleo la Roho Mtakatifu kwetu, tumefanyiwa mabadiliko ya ndani kiroho kwa namna ambayo wale ambao waliishi chini ya Agano la Kale wasingalijua kabisa! Sio kwamba sisi ni watu ‘wakubwa sana’ kuliko wao, lakini ni kwa sababu sisi tumeletwa katika jambo ambalo ni kubwa zaidi pamoja na huduma ambayo ni kubwa zaidi! Kule kumwagika kwa damu ya Yesu pamoja na ule ufufuo wake  umebadilisha kila kitu, ndani na inje, vyote viwili! Kwa hiyo imeandikwa juu ya watu wa Agano la Kale, “Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, HAWAKUIPOKEA AHADI; kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia KUTUWEKEA SISI KITU KILICHO BORA, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi.” (Waebr.11:39,40).

Yesu alimwaga damu yake ili kwamba sisi tupate kuipokea ahadi yake ya Roho Mtakatifu (Yoh.14:16; 16:7; Matendo 1:4,5; Wagalatia 3:13,14): “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani.” (Wagalatia 3:13,14).

Ibrahimu alihesabiwa haki kwa imani, lakini hakupokea ubatizo wa Roho Mtakatifu (ahadi ya Roho) kwa sababu Yesu Kristo alikuwa bado hajafa na kutukuzwa. Bwana Yesu alipaswa kumwaga damu yake na kuzibeba dhambi zetu pale msalabani na kuyashinda mauti kabla Roho Mtakatifui hajatolewa na kukaa ndani yetu milele! Biblia inafafanua wazi kabisa kuwa ile ahadi ya Roho Mtakatifu ilitolewa tu baada ya ufufuo wa  wa Yesu Kristo: “Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa…. Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya Roho Mtakatifu, amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia. (Yoh.7:39; Matendo 2:33). Kama vile Ibrahimu, tunahesabiwa haki kwa imani, lakini ingawa imani kwa wakati ule ilileta kuhesabiwa haki, isingewaleta katika “ahadi ya Roho Mtakatifu”. Wagalatia 3:14 inatuweka wazi kuwa tunahesabiwa haki kwa imaani ili kwamba katika imani hiyo tuweze pia kupokea ahadi  ya Roho Mtakatifu, ambayo watu wa Agano la Kale hawakuijua.

Ebu niseme tena hapa kuwa Biblia haijichanganyi yenyewe, lakini inaonyesha maendeleo ya kimsingi na lazima. Biblia inajieleza yenyewe kwamba Roho Mtakatifu aliwavuvia watu kwa ajili ya huduma nyakati za Agano la Kale, lakini hiyo inapaswa kutofautishwa na ahadi ya Roho Mtakatifu ambayo tunaipokea kupitia ubatizo wa Roho Mtakatifu. Yohana Mbatizaji alijawa na Roho Mtakatifu toka tumboni mwa mama yake (kwa ajili ya huduma yake) lakini hakujua kabisa juu ya ahadi ya Roho Mtakatifu ambao unawafanya watu waweze kuwa viumbe vipya katika Kristo! Biblia sio kazi ya kithiologia ambayo kila kitu kinaelezwa kwa mpangilio – inatupasa kuelewa mambo kulingana na mktadha/hitimisho ambalo Biblia yenyewe inaliweka kwa uwazi!

Biblia inaeleza kuhusu Roho Mtakatifu nyakati za Agano la Kale (Kutoka 31:3; Hesabu 11:17; Waamuzi 3:10; 1 Samweli 10:6, 16:14; 2 Mambo ya Nyakati 15:1) lakini utaweza kuona kutokana na mistari hiyo hapo juu, kimsingi hiyo inahusu huduma. Ahadi ya Roho Mtakatifu, ubatizo wa Roho Mtakatifu nayo pia inahusu huduma lakini kimsingi zaidi ni ule ujio wa Roho Mtakatifu kama nafsi ndani ya maisha yetu, na kupitia yeye sisi tunafanyika kuwa nyumba au maskani ya Baba na Mwana (Yoh 14:16-23), na ni makazi ya Mungu – Wasfeso 2:22. Hawakujua hilo kabla ya Kalvari! Ni nguvu ya damu ya mwanakondoo wa Mungu pekee inatusafisha ndani kabisa ili kwamba Kristo aje kuishi ndani yetu kwa Roho Mtakatifu. “Yeye atawabatizeni kwa Roho Mtakatifu ma kwa moto”! Na matokeo ya jambo hili ni kwamba “kile ambacho sheria haikufanya katika hicho ilikuwa dhaifu kwa mwili, Mungu amekifanya hicho kupitia mwanae ili kwamba ile haki inayotakiwa kwa sheria ipate kutimilizwa ndani yetu. Amen!

Katika Agano la Kale hukupaswa kufanya uzinzi. Katika Agano Jipya inasemwa ikiwa utamwangalia mwanamke hata kuwaka tamaa, utakuwa umezini ndani ya moyo wako. Chini ya sheria katika Agano la Kale hukupaswa kuua mtu yeyote kwa sababu zako bibnafsi, katika Agano Jipya wewe utakuwa kwenye hatari ya hukumu hata ukimchukia au kumwonea wivu ndugu yako tu pasipo sababu yoyote! Katika Agano la Kale Waisrael waliwaua maadui zao, katika Agano Jipya hatupasi kumwua yeyote! Katika Agano la Kale hakuna aliyeweza kusema “Kristo anaishi ndani yangu”!

Ndiyo, kulikuwa na watu wakuu katika Agano la Kale kulingana na agano lililokuwa chini yao nyakati zile. Ndio, baadhi ya watu hao walikuwa kama Ayubu, alikuwa ni mtu ‘mkamilifu’ na welekevu, mwenye kumcha Mungu, akimhofu Mungu na kuepukana na maovu. Ayubu alikuwa ni mtu ‘mkamilifu’, lakini sasa huo ulikuwa ni wakati tofauti, na agano tofauti! Hawakujua kupokea ahadi ya Roho Mtakatifu ni kitu gani na wala kufanyika kiumbe kipya katika Kristo ambapo vitu vyote ni vya Mungu ili kwamba wapate kudhihirisha maisha ya Kristo!

Utukufu ule tunaoujua katika Kristo unamulika kwa wingi utukufu ambao Musa aliujua katika mlima Sinai! (soma Wakor.3:5-11).

Unaona, ule utukufu ambao Musa alikuwemo ni kama si kitu ukilinganisha na utukufu wa ushirika tulionao sasa pamoja na Baba na mwana! Sisi si ‘bora’ sana kuliko watu wakuu wa nyakati za Agano la Kale – lakini tumeletwa katika baraka zizidizo, baraka bora sana! “Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.” (Warumi 5:19).

Katika Warumi 7:14 inasema kuwa “Kwa maana twajua ya kuwa torati asili yake ni ya rohoni; bali mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi.” Ninatumaini baadaye kuandika makala kuhusu Warumi 7, lakini ebu niseme hapa kuwa katika mstari huu wa Biblia kuwa upo wazi kuwa Paulo haongelei kuhusu Wakristo. Katika mstari huu Paulo anaelezea mkweli ya kimsingi juu ya kwa nini watu hawakutimiza kile ambacho sheria ilihitaji, na kwa nini sheria haikumbadilisha mtu kiroho. Anaeleza kuwa zile amri zinawakilisha ile haki ya Mungu na kwa mtazamo huo sheria ilihitaji nguvu ya kiroho ili kuitimiliza! Mwili haukutimiliza! Ndiyo wanadamu waliweza kumhofu Mungu na kujizuia na uovu katika nyakati za Agano la Kale, na kulikuwepo na watu wa namna hivyo, lakini hawakuijua nguvu ya utakaso ya damu yake Yesu wala uweza wa ufufuo wake kwa wakati ule (na Mungu alijua hivyo). Na kwa hiyo utimilifu wa haki ambao sheria ilikuwa inaelekeza ulikuwa mbele yao nyakati hizo, kwa sababu Paulo anasema ‘bali mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi.’ Mimi kama mwanamume msingi wa hali yangu bila wokovu wa Yesu ni hii – mimi ni mtu wa mwilini nimeuzwa chini ya dhambi. Hii ndio sababu ilimpasa Mungu kumtuma mwanae aje afe kwa ajili yetu! Sheria inahitaji maisha ya kiroho, ili kutimiza matakwa ya haki, lakini ‘mimi ni wa mwilini.’ Hii ndiyo sababu liko Agano Jipya ili kubadili msingi wa hali ya mwanadamu ili kumfanya awe “wa kiroho”, yaani, yampasa mtu yule apokea maisha ya Kristo ndani yake, na ni maisha yake Kristo ndani yetu ndiyo yanayotimiza haki ambayo imeelekezwa katika (Wafilipi 1:11).

Mpango wa Mungu toka mwanzoni ulikuwa ni kutufanya sisi tufanane nae. Inawezekanaje mtu ambaye ni wa kimwili na ameuzwa chini ya dhambi aishi kama Mungu ambaye ni Roho – Mungu ni upendo, Mungu ni mvumilivu, Mungu ni mwenye neema na rehema, amejaa wema na kweli! Inawezekanaje mtu ambaye ni wa kimwili ameuzwa chini ya dhambi aishi namna hii? Kutokana na fundisho tunalolipata kutoka katika kitabu cha Warumi 7, sheria ilitolewa ili kumwonyesha mwnadamu kuwa anaiishi namna hii! Ulipaswa kupata maisha ya Roho wa Mungu ndani yako ili uishi kama yeye aishivyo – hicho ndicho Agano Jipya lilicho kifanya na kukifanya kiwezekane. Hii ndiyo sababu inayomfanya Yohana aandike kuwa, “Yeye asemaye kuwa anakaa ndani yake imempasa kuenenda yeye mwenyewe vilevile kama yeye alivyoenenda,” na tena “katika hili pendo limekamilishwa kwetu ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu, kwa kuwa kama yeye alivyo ndivyo na sisi tulivyo ulimwenguni humu”(1Yoh 2:6,4:17). Je, tunaliamini neno la Mungu?

Paulo alipoandika mistari hii, ni wazi kabisa kuwa yeye ‘alikuwa hajauzwa chini ya dhambi’. Hilo haliwezekani! Sisi hatujauzwa sasa chini ya dhambi! Tumenunuliwa kwa thamani (1 Wakor. 6:19,20). Tumekombolewa, tumenunuliwa kwa damu ya thamani ya Kristo Yesu. (1Petro 1:18,19).

Asingepaswa kujizungumzisha yeye mwenyewe kama mkristo tunaweza kuona kwa uwazi kabisa hapo katika hiyo Warumi 7, kwamba mtume Paulo alikuwa anaongea kuhusu maisha yake yeye mwenyewe alipokuwa anaitumikia sheria kabla maisha mapya ya Yesu ya wokovu.  Anasema katika ule mstari wa 5, “Kwa maana tulipo kuwa katika haali ya mwili…..”. Hiyo ndiyo ilikuwa hali yake katika siku zake za nyuma! Katika ule mstari wa 14, alikuwa anaelezea kweli ya kimsingi kabisaa kuhusiana na sheria na mwanadamu. Paulo hakuwa ni mtu wa mwilini, bali yeye alikuwa ni mtu aliyeishi kulingana na Roho na akifundisha wengine ili waishi kulingana na kile ambacho Mungu amekifanya ndani yao kwa Roho Mtakatifu. (Soma Warumi 8:1-16).

Kwa hiyo, Paulo anasema, “bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu. Naye ndiye aliyetutosheleza kuwa wahudumu wa agano jipya; si wa andiko, bali wa roho; kwa maana andiko huua, bali roho huhuisha. Basi, ikiwa huduma ya mauti, iliyoandikwa na kuchorwa katika mawe, ilikuja katika utukufu, hata Waisraeli hawakuweza kuukazia macho uso wa Musa, kwa sababu ya utukufu wa uso wake; nao ni utukufu uliokuwa ukibatilika; je! Huduma ya roho haitazidi kuwa katika utukufu?” (2 Wakor.3:5-8). Je Unaona? Ile sheria iliyoandikwa na kuchorwa katika mawe, Paulo anaiita ‘huduma ya mauti’! Jisome menyewe sehemu iliyobakia ya sura ile. Paulo anaweka wazi hapo kuwa wale wanaofundisha amri za Agano la Kale wanayo huduma ya mauti – wanawazuia watu kufahamu ule utukufu na wokovu wa Agano Jipya. Utukufu wa wokovu ambao Kristo anauleta umejificha kutoka kwao! Kusoma na kuendelea kufundisha sheria na kujaribu kuishi kwa kuzifuata sheria, inafanana ni pazia linalo wapumbaza watu hawa wasiujue ukweli na nguvu ya waokovu wake Kristo. (2 Wakor.3:15,16).

Kwa kifupi ile warumi 7 inaelezea hali ya mtu anayejaribu kuishi kwa sheria, lakini katika kujaribu kwake kufanya hivyo, anajikuta tu kuwa dhambi ina nguvu na inaendelea kufanya kazi ndani yake ili kumfanya ayafanye yale asiyopenda kuyafanya. Kwa nini? Kwa sababu ‘sheria ni kiroho’ na yeye ni ‘mtu wa mwilini’ aliyeuzwa chini ya sheria’! KRISTO ALIKUFA ILI KUYABADILI HAYO! Ile Warumi sura ya 6 na ya 8 inaelezea mambo hayo kwa uwazi zaidi! Sura hizi mbili zinaelezea juu ya hali ya mtu, hiyo iko tofauti na kile tulichokisoma katika ile sura ya 7. Katika ile sura ya 7, Paulo anaelezea moja kwa moja kwa hao waijuayo sharia. Sio tu kwamba anaelezea juu ya kusudi na zuizi la sheria, bali anaweka wazi kwa wote kuwa mtu hawezi kuendelea kuishi kwa sheria na hapohapo ukamfuata Kristo!

“Ndugu zangu, hamjui (maana nasema na hao waijuao sheria) ya kuwa torati humtawala mtu wakati anapokuwa yu hai? Kwa maana mwanamke aliye na mume amefungwa na sheria kwa yule mume wakati anapokuwa yu hai; bali akifa yule mume, amefunguliwa ile sheria ya mume. Basi wakati awapo hai mumewe, kama akiwa na mume mwingine huitwa mzinzi. Ila mumewe akifa, amekuwa huru, hafungwi na sheria hiyo, hata yeye si mzinzi, ajapoolewa na mume mwingine. Kadhalika, ndugu zangu, ninyi pia mmeifia torati, kwa njia ya mwili wa Kristo, mpate kuwa mali ya mwingine, yeye aliyefufuka katika wafu, kusudi tumzalie Mungu matunda. Kwa maana tulipokuwa katika hali ya mwili, tamaa za dhambi, zilizokuwako kwa sababu ya torati, zilitenda kazi katika viungo vyetu hata mkaizalia mauti mazao.” (Warumi 7:1-5).

Ina maana kuwa kama ukitaka kumfuata Yesu na wakati huohuo unaishi chini ya torati wewe ni kama ‘mzinzi’. Kama tukiishi kwa sheria ya Musa tunazalia mauti mazao, lakini  tukiishi kwa imani katika Kristo, tutamzalia Mungu matunda! Chagua tu! Huwezi kufanya yote mawili kwa pamoja; aidha utakuwa mzinzi kuhusu Injili! Kama nilivyosema ninatumaini kuandika makala kuhusu Warumi 7, na kuichambua mstari kwa msitari ili kuielezea kwa ufasaha na uwazi na utimilifu zaidi.

                                               —————————————

Yote yanao mktadha wake! Usiku unaweza kuziona nyota mbinguni nazi zinang’aa, tena hupendeza na unaweza kumshukuru Mungu kwa ajili ya nuru zake. Lakini mara tu jua lizukapo, hamna nyota tena! Nuru yake imetoweka! Ni vilevile kuhusu Agano Jipya  na wokovu ambao Yesau hutuletea!

“Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang’aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye. Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana. Yesu akaja, akawagusa, akasema, Inukeni, wala msiogope. Wakainua macho yao, wasione mtu ILA YESU PEKE YAKE.” (Mathayo 17:1-8).

Huwezi kulinganisha au kusawazisha Yesu Kristo na watu wa Mungu walioishi hapo zamani kabla ya Kalvari. Lakini kutokana na hayo ni muhimu pia kuelewa kuwa huwezi kulinganisha mambo yale  yaliyowezekana chini ya sheria ya Musa na yale ambayo kwa sasa yanawezekana kupitia wokovu wa Yesu Kristo! Jambo lile lisilowezekana chini ya torati, sasa limefanyika liwezekane kupitia Yesu Kristo! Huwezi kulinganisha watu walioishi wakati wa  Agano la Kale na watu ambao walibatizwa kwa Roho Mtakatifu katika Kriso Yesu kwa sababu ya Agano Jipya!

Upungufu wa Agano la Kale haukudhihirishwa kwa wazi kabla ya kuja kwa Mwokozi Yesu Kristo! Lakini sasa Mungu ‘ametupa nuru ya elimu ya utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo.’ Sasa tunayaona yote katika nuru ya Yesu Kristo na alilolifanya msalabani!

Imeandikwa, “kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12). Lakini sasa Yesu Kristo ‘aliihukumu dhambi katika mwili’ na yeye ‘ni mwanakondoo wa Mungu aiondoaye dhambi za ulimwengu.’ Na tena imeandikwa, ‘aliyebatili mauti na KUUFUNUA UZIMA, na kutoharibika kwa ile Injili” na hayo yote ili ‘kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mtu mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.” (Warumi 8:3; Yoh.1:29; 2 Tim.1:10; Warumi 5:19). Je unayatambua mabadiliko yale makubwa sana ambayo Mungu aliyafanya kupitia mwanawe?

Kwa sababu hali ya kiroho ya watu wakati ule kabla ya Kalvari, Mungu alitudhihirisha kwa uwazi maana hakuwa na mtu aliyeweza kupaingia mahali pale alipo (isipo kuwa kuhani mkuu mara moja kwa mwaka). Pazia lile lilizuia watu wa Mungu wasiingie kwa sababu ya dhambi zao na kwa sababu ya hali ya kiroho chao! Na ilikuwa ni lazima watu wa Mungu watoe sadaka kwa ajili ya dhambi kila mwaka! “Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao. Kama ndivyo, je! Dhabihu hazingekoma kutolewa; kwa maana waabuduo, wakiisha kusafishwa mara moja, wasingejiona tena kuwa na dhambi? Lakini katika dhabihu hizo liko kumbukumbu la dhambi kila mwaka. Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi.” (Waebr.10:1-4). Lakini kwa toleo la Yesu Kristo imeandikwa, ‘Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa.”(Waebr 10:14).

Basi, kutokana na ukweli huo tunaona kuwa torati ya Musa haikuweza kubadilisha hali ya mtu ya kiroho, wala kuwatakasa kweli kweli, wala kuwakamilisha. Mifumo ya torati ya Musa haikuwawezewsha waumini waingie mahala patakatifu pa Mungu alipo. Kinyume chake torati ya Musa imetolewa ili kuthibitisha na kuwaonyesha watu hali zao kiroho inayowazuia kuingia pale alipo Mungu. Kwa hiyo, ‘Mungu aondoa la kwanza (ambao ni mpango wa kwanza chini ya torati ya Musa) ili kusudi alisimamishe la pili; (toleo la Yesu Kristo msalabani na Agano Jipya). Waebr 10:14. Jambo la muhimu hapo ni kuyatambua hayo yote si suala la kuzisaamehe dhambi tu! Kwa toleo la Yesu Kristo dhambi zetu zimeondolewa, na kwa ile damu yake Yesu hatupati msamaha wa dhambi tu, bali kwa damu yake tunasafishwa kwa undani zaidi na kutufanya sasa tuingie pale Mungu alipo. “Basi ndugu, kwa kuwa tunaujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu….” (Waebr 10:19).

Kama yuko mtu fulani anasema kuwa hali ya kiroho ya waumini wale waliokuwa chini ya torati ya Musa kabla ya Kalvari haitofautiani na hali ya waumini ambao wamepata wokovu kupitia Yesu Kristo, basi hapo ndipo mtu huyo atakuwa haelewi hali ya watu kabla ya Kalvari, wala Injili, wala wokovu ule ambao Mungu ametupatia kupitia kifo cha mwanawe msalabani.  Kama hamna tofauti yoyote, kwani Yesu alikufa?

Najua kuwa narejea kwenye mambo yale yale ambayo tayari nimekwisha yaandika hapo juu. Lakini mambo hayo ni ya kimsingi. Ni lazima tuyaelewe mambo hayo pale tunapoyaangalia maisha ya watu wa Agano la Kale! Kwa kupitia Biblia nzima tunajifunza sasa  juu ya Yesu Kristo na wokovu wake. Lakini kama Biblia ni neno la Mungu (na ndivyo lilivyo) kwa nini basi waopo watu wanaopinga mpango wa Mungu kupitia mwanae Yesu Kristo ili waweze kubakia katika mpango wa kale ambaop Mungu mwenyewe ameuondoa?

“Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo… Katika ungwana huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa.”

David Stamen  © 2015       

Unaweza kupakua somo hili kwa kubonyeza link hiyo: Jumamosi au Jumapili

Pamoja na somo hapo juu ni vizuri kusoma somo lifuatalo:

Chimbuko Na Upotofu wa Kanisa la Waadventista Wasabato

Nimeyagusa mambo mengi na inawezekana kabisa watu wanayo maswali mengine. Unaweza kusoma na kusikiliza zaidi juu ya Maagano, Injili na wokovu wetu, na ubatizo katika Roho Mtakatifu kwa kubonyeza links hapo chini:

https://somabiblia.wordpress.com/uzima-wa-milele-ni-nini-injili-ni-nini/

https://somabiblia.wordpress.com/maagano-ya-mungu/

https://somabiblia.wordpress.com/kuwekwa-huru-mbali-na-dhambi/

https://somabiblia.wordpress.com/ubatizo-kwa-roho-mtakatifu-na-moto/

Unaweza kusoma zaidi pia kwenye http://www.wasabato.com

 

 

51 responses to “Je, Tukusanyike Siku Gani Kati ya Jumamosi na Jumapili?

  1. Pingback: somabiblia
  2. fadhil

    August 13, 2015 at 8:25 pm

    kwa hiyo kanisa la kristo limejengwa juu ya msingi wa mitume ,manabii na yesu ndiye jiwe kuu la pemben (efeso 2:20,22) ,sasa ukisoma (matendo 17:1,3 na matendo 13:42,44 ) sijaelewa vzur kwamba ilikuwa desturi ya paulo kufanya nn ? je naka kanisa la leo tunatakiwa kufanyaje?

     
    • dsta12

      August 13, 2015 at 9:36 pm

      Je, ulisoma makala au siyvo? Je, hujasoma niliyoyaandika hapo juu, yaani, “Na wanaendelea kutafuta tafuta mistari, lakini kwa sababu mafundisho yao hayapo katika Agano Jipya ni lazima wachague mistari bila kujali muktadha ambayo hauhusiki na mada yetu! Na hakika huo ni udanganyifu. Wamejifanya vipofu juu ya mambo yale yaliyo wazi! Kwa mfano, wanataja mistari kama Matendo 13:14, 16:3,17:2. Hasa huu (Mstr 13:14) unaosema, “Lakini wao wakatoka Perge, wakapita kati ya nchi, wakafika Antiokia, mji wa Pisidia, wakaingia katika sinagogi siku ya sabato, wakaketi.” Sasa, sijui kwa nini baadhi yao wananukuu mistari hiyo! Haihusu mada yetu! Haihusu makusanyiko ya wakristo, ya kanisa la Bwana Yesu! Mistari ile inahusu kuhubiri kwa Injili kwa wale wasiompokea Yesu kama Mwokozi wao! Katika sura ile ile ya 13 tunasoma kuwa Paulo na Barnaba walipelekwa na Roho Mtakatifu kuhubiri Injili! Na Paulo anatangaza kwenye Warumi 1:16, “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa MYAHUDI KWANZA, na kwa Myunani pia.” Na tunajua Paulo alichukua mzigo mzito sana kwa ajili ya Wayahudi, kama alivyosema, “ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili; ambao ni Waisraeli…”. (Warumi 9:3,4) Basi, hatushangai kama anatumia fursa kuhubiri Kristo siku ile ile na mahali pale ambapo Wayahudi hukusanyika kila juma, yaani,kuingia katika sinagogi siku ya sabato! Kama Paulo alivyosema, “Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili NIWAPATE WAYAHUDI; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate walio chini ya sheria.” (1 Wakor.9:20). Hiyo ni jambo la kuhubiri Injili, haihusu siku ile ambayo Wakrsito walikusanya! Kama nilivyosema, wananukuu mistari bila kufikiri, bila kujali muktadha Mara wanapoona neno ‘sabato’ au ‘sheria’ katika Agano Jipya wanafikire wameshinda – haijalishi muktadha ni ya namna gani!” Je, hujasoma juu ya lengo la somo hili, yaani, “Lengo la somo hili ni kuonyesha hamna sheria katika Agano Jipya ambayo inatufundisha lazima tukusanye jumamosi. Kufanya hivyo ni kosa kubwa na udanganyifu. Lengo la somo hili siyo kutufundisha lazima tukusanyike jumapili. Nilinukulu mistari kuonyesha ilikuwa desturi ya wakristo kusanyika hasa jumapili. Lakini siyo sheria. Mwanzoni wakristo walikusanyika hata kila siku! Matendo ya Mitume 2:46. Ya mwisho, lengo la somo hili ni kuonyesha na kueleza tabia ya wokovu wetu ndani ya Kristo Yesu na vipi fundisho lile la kushika sabato linavyopinga lengo la Mungu kupitia Mwanawe. Ni wazi kumpenda Mungu, kumwamini, kumtii na kumabudu ni jambo la kila siku, kila wakati na kila nafasi – siyo la jumapili tu!” Natumaini ni wazi sasa lakini nashangaa umeuliza swali hili kwani jibu lipo kwenye makala yenyewe.

       
  3. Anonymous

    September 25, 2015 at 11:57 pm

    kwaiyo siku ya sabato ni juma pili? na kama ni juma pili naomba uniambie mafungu yanayo saport kuwa sabato ni juma pili?

     
    • dsta12

      September 27, 2015 at 5:13 pm

      Nashangaa na swali lako. Ni wazi hujasoma makala yangu vizuri! Jibu lipo kwa wazi katika makala yenyewe!

       
    • leniwelo kibona

      December 19, 2016 at 7:47 pm

      inachekesha sana kama haya mafungu yanadanganya
      matendo 13:42-43
      matendo 17:1-3
      isaya 66:22-23
      basi hakuna haja ya kusoma biblia kwann tusome wakati inatudanganya
      lakini ole wako ubadilishaye kweli kuwa uwongo na uwongo kuwa ukweli.

       
      • dsta12

        December 19, 2016 at 9:06 pm

        NI wazi hujasoma makala, Ieniwelo. Ungalisoma, usingaliweka comment yako ya hapo juu. Nilijishughulisha na maswali yale kwenye makala.

         
      • ngongoloekuilin

        January 17, 2017 at 10:37 am

        Mmmmhhhh?

         
      • Bukela John Maduhu

        July 6, 2018 at 2:24 pm

        Amen

         
  4. Gibdon Kagaruki

    October 3, 2015 at 4:21 am

    Mtumishi ubarikiwe sana kwa mafundisho mazuri sana japo yanaitaji sana aikili za Rohoni na si hizi darasani. Kwa mafundusho haya kwa kiasi nimeelewa kwa nini Mungu alijifunua kwa mtime Paulo. Pia nimeelewa kuwa Mungu anafunua kwa nyakati tofauti tofautitofauti hivyo usipokuwa makini unaweza kuchwa. Mfano kama unaenda ulaya ukifika wakati wa kupanda ndege wewe ukasema nimezoa kupanda Gari kamwe ulaya hufiki. Mfano kuogelea na boti na mfano wa njoka kuishi kama kondoo vimeniganya nielewe zaidi mpango wa sasa kwa mwadamu. Kwa ujumla mpango was Mungu kwa sasa ni kushughulika na mwanadamu kuanzia rohoni yaani kwenye chanzo cha mema na mabaya.
    Ubarikiwe sana MTU wa Mungu.

     
    • Anonymous

      October 17, 2015 at 8:42 am

      Tunashukuru kwa Maelezo maarefu na kuuita ukweli kua ni uongo.
      Hujasoma hata mathayo 24 yesu alipowaonya wafuasi wake juu ya siku za mwsho “ombeni kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi wala siku ya sabato” hivyo inaonesha Yesu alijua kua wafuasi wake wataendelea kutunza sabato mpaka atakaporudi na kuendlea

      Mnatia chumvi sana maana halisi ya kuhesabiwa haki kwa Imani
      Mabishano yoote na maneno yako marefuu yasiyo elezeka uliyo yaandika lengo lako n zuri tuingie mbinguni lkn tufanye nini ? Mtu mmoja aliuliza swali muhimu kwa maisha yake na kwetu pia alimuuliza mwalimu anayeaminika kuliko wewe ya kua ” nifanye nini niingie peponi?” Yesu akamwambia “Zishike amri…” Sasa kwanini hakusema “we niamini tu” au “subiri nife msalabani”
      Km ninyi watia chumvi mnavyohubiri ? Hivi mnadhani mtatuboa macho tunaosoma Biblia?
      Kina kitu mna overlook nyie, we are saved by “faith” not “belief”
      Faith= Obidient + belief
      Hamuoni mnapingana na sauti ya Mungu?
      Soma warumi 2:13
      “Si hao waisikiao sheria walio wenye haki mbele za Mungu Bali wao waitendao ndiyo watakao hesabiwa haki”
      Paulo anasema waziwazi hao waitendao sheria ndiyo watakao hesabiwa haki…
      Lazima dhana ieleweke vizuri bila porojo na tafsiri hovyo za maandiko
      Kushika Amri 10 za Mungu hakutufanyi “tustahili” mbele za Mungu Bali kunatufanya “Tufae” kua raia wa Mbinguni.
      Kwanini Yesu alisema “ukitaka kuingia ktk uzima zishike Amri?” Yesu alifahamu maandiko vizuri sana soma zaburi 119:155
      “Wokovu u mbali na wasio haki kwakua hawajifunzi amri zako”
      Kumbe kuepuka amri za Mungu ni kuukimbia wokovu Ili uwe mbali na wewe…………

      NEEMA::::
      Fuatilia mlolongo huu uuelewe
      Sheria – dhambi (uasi wa sheria) – Neema (msamaha wa dhambi) – Yesu (ameleta Neema) – Injili (inamhubiri Yesu) – Kanisa (linahubiri injili)

      Walimu mnaotoboa macho ya watu Mungu ukitoa sheria kwenye sequence hiyo maana ake hakuna dhambi wala hakuna haja ya Neema wala Yesu

      Tunahubiri kua tunaokolewa kwa Neema lazma tueleze kazi ya Neema ni nini?
      Tito 2:10-12
      ” inatufundisha kuishi maisha ya haki ”

      Hivyo Neema siyo koti la kufichia dhambi mbele za Baba
      Maisha ya haki ni yapi hayo? = Ni maisha ya kuishi kwa kumcha Mungu yaani kutenda yanayo stahili
      Kumcha Mungu ni nini ? Hebu tuangalie definition aliyoisema Mungu mwenyewe pale Mlima Sinai
      Kumbkumb la torat 4:10-13
      Mungu akamwambia Musa niitie watu hawa niwafundishe namna ya kunicha Mimi siku zote akawahubiri amri 10 kwa hiyo kushika amri 10 za Mungu ndiyo maana halisi ya kumcha Mungu.

      PAMBANO LA MWISHO:::

      Shetani hafanyi vita na wasizishika amri zote za Mungu km zilivyotolewa wala sihitaji kuzirudia rudia

      Ufunuo 12:17
      “Joka akamsirikia mwanamke….akafanya vita juu ya wazao wake hao wazishikao amri za Mungu na kua na ushuhuda wa Yesu”

      Kwa hiyo usipotoshe watu wa Mungu juu kuishi kwa imani na kushika sheria za Mungu
      Mathayo 23:23 Mambo makuu ya sheria ni Imani,adili na Rehema kwa hiyo imani n moja ya Mambo makuu ya sheria
      Wakolosai 2 ni rahisi kueleweka kwa mtu mwenye akili wala hutamtoboa macho
      Kulikua na sabato za miaka,mapumziko ya miezi mengi tu na sherehe mbalimbali ambapo walikua wakipumzika(shabbat- pumziko) ambazo zilianza kipindi cha Musa zilikua zikisonda mambo yajayo mbele yaani Kristo lakini sabato ya Amri ya Nne inasonda nyuma kwenye uumbaji na kutukumbusha uwezo mkuu wa Mungu wa uumbaji sifa ambayo inamtofautisha Mungu na miungu ya uongo ambayo ina majina tu lkn haipo na wala hikuumba kwa hiyo unapotea sana usiufanye moyo wako mgumu.

       
      • Anonymous

        October 17, 2015 at 9:11 am

        Kua makini unapo elezea watu dhana ya kuhesabiwa haki kwa Imani na kushika sheria za Mungu…Yesu alikuja ulimwenguni kuishudia kweli pilato alimuuliza kweli ni nini? Yohana 18:37-38
        Kweli ni sheria ya Mungu (zaburi 119:142) na Ndiyo Neno la Mungu kiumjumla ndo mana Imesemwa “ktk amri hizi mbili hutegemea torati yooote na manabii” sheria ya Mungu Yesu alikuja kuishuhudia.
        Yesu alikuja kuihubiri amri

         
        • dsta12

          December 10, 2015 at 10:03 pm

          Uliandika, “Kweli ni sheria ya Mungu… ” Je, hujasoma maneno ya Mwana wa Mungu? Yeye alisema, “Mimi ndimi njia, na KWELI, na uzima…” (Yoh.14:6). Aidha, hujasoma, “torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na KWELI zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo.”

           
      • dsta12

        December 10, 2015 at 9:57 pm

        Inaonekana hujaelewa au hutaki kusoma somo langu. Uliandika, kwa mfano, “…Yesu akamwambia “Zishike amri…” Sasa kwanini hakusema “we niamini tu” au “subiri nife msalabani”…” Mimi nilijibu swali hili katika somo! Je, hujalisoma?

         
  5. MASHIMBA

    June 20, 2016 at 1:29 pm

    YESU ALIISHI KATIKA KIPINDI CHA AGANO LA KALE,BAADA YA KUFUFUKA NA KUPAA MBINGUNI MITUME WAKAISHI NA KUENDANA NA AGANO JIPYA BAADA YA YESU KULITIMIZA AGANO LA KALE

     
    • dsta12

      June 21, 2016 at 6:09 pm

      “Kwa maana manabii wote na torati walitabiri mpaka wakati wa Yohana.” Matayo 11:13

      ” Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu.” Luka 16:16

       
    • Anonymous

      October 13, 2021 at 12:55 pm

      barikiwa sana

       
  6. dsta12

    August 16, 2016 at 9:51 pm

    TANGAZO: UKIWEKA COMMENT ‘ANONYOMOUS’ (YAANI, BILA JINA), COMMENT YAKO ITAFUTWA. ASANTEENI.

     
  7. Filemoni wansato

    November 16, 2016 at 6:15 pm

    Ndugu umejaribu kujitetea kwa makala yako kuhusu kusanyiko la ibada jumamosi au jumapili.lakini ujue Mungu si kigeugeu kwamba angebadisha nakuwapa watu wa agano jipya yaani mataifa ibada tofauti na wayahudi au Israeli.Nabii Isaya alitangulia kuona hilo unaloliwaza nakulindika, kuhusu wokovu kwa mataifa,soma isaya 56:1-3,au sura yote.pia suala kuhu ibada ya jumapili au ukengeufu umenenwa na nabii danieli kuwa pembe ndogo ingejitukuza na kuangusha mahali patakatifu chini.soma danieli 8:11-12;7:25. Ilinenwa pia na yesu kama chukizo la uharibifu,soma mathayo 24:15,paulo pia ametaja kama siri ya kuasi 2wathes 2:3-7 au mtu wa dhambi maana dhambi ni uasi wa sheria.Na yohana kule patimo aliona ufunuo 14:12

     
    • dsta12

      November 16, 2016 at 7:22 pm

      Filemoni, ya kwanza hujaonyesha wapi nilikosa katika makala yangu, ulitoa kauli yako tu. Juu ya kauli yako na Danielli 8, unaweza kusoma makala nyingine kuptia link hapo juu, yaani, “Chimbuko Na Upotofu wa Kanisa la Waadventista Wasabato.”

       
  8. Anonymous

    December 16, 2016 at 5:40 pm

    habar gani warumi 7:7anamaanisha nn? nakala yako inapingana Na warumi.
    je unaelewa juu ya Neema Na sheria ,je naomba unifanunulie sheria aliyo andika Musa Na ya mungu kwa mkono wake

     
  9. SFAN

    February 16, 2017 at 4:23 am

    Tusemeje,basi? Torati ni dhambi? Hasha! walakini singalitambua dhambi ila kwa sheria….(warumi 7:7) pasipo sheria hatuwezi kutambua ni wap tumekosea na kutanga mbal na upendo wa MUNGU. Maana mtu awaye yote atakayeshika sheria yote,ila akajikwaa katka neno moja,amekosa juu ya yote Yak 2:10

     
    • Kennedy Meshuck

      February 20, 2017 at 11:21 am

      Nashukuru kwa mtoa mada na kwa ajili ya wote waliochangia mada hii kulingana na uchunguzi na utafiti na ujuzi mlio nao juu ya neno la Mungu.
      Jambo la msingi ambalo Mimi napenda kuliongezea ktk mjadala huu ni kuhusu mafundisho ya Paulo kwenye Biblia, yasionekane yanapotosha imani ya wakristo. Mzee Petro alitoa onyo na kuwa makini sana kuhusu nyaraka za Paulo akisema,”…….kama vile ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa;vilevile kama ktk nyaraka zake zote pia, akitoa humo habari za mambo hayo; katika nyaraka hizo yamo mambo ambayo ni VIGUMU KUELEWA nayo; na mambo hayo watu wasio na elimu,wasio imara HUYAPOTOA, kama vile wayapotoavyo na MAANDIKO mengine,kwa UVUNJIFU WAO WENYEWE. 2Petro3:15-16.
      Kwa hiyo napenda nikuletee vitu vichache kuhusu matumizi sahihi ya sheria kwa kuonesha jinsi ambavyo Paulo anataka tuelewe ktk maandiko au nyaraka zake. Na ni imani yangu kuwa huu ndio mtazamo wa Paulo juu ya matumizi ya sheria na imani ya Mkristo.

      Hebu angalia na utafakari matumizi yafuatayo ya sheria katika Biblia. Kwa kuelezea nimeweka matumizi sahihi na matumizi yasiyo sahihi ya sheria kwa Wakristo. Nianze na matumizi yasiyofaa ya sheria kwa wakristo.
      MATUMIZI YA SHERIA YASIYOFAA KWA WAKRISTO

      1. Kushika sheria ili uhesabiwe haki na uokolewe au kupata wokovu kwa sheria. ” lakini haki ya Mungu imedhihirishwa pasipo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii; ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote waaminio.” taz Rum 3:21 – 4:25;. ” Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo hsikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo….”
      Efeso 2:8-10.

      2. Kulazimisha Sheria ya maazimisho kwa wengine Galatia 4:9-10; Kolosai 2:16-17.

      3. Kuongeza sheria ya mapokeo ya kibinadamu kwenye sheria ya Mungu. Marko 7:1-15; Mathayo 15:1-9.

      4. Kusahau mambo ya msingi na kupendelea mambo madogo madogo. Mathayo 23:23-24″ Ole wenu waandishi na mafarisayo, wanafiki, kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lkn mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache. Viongozi vipofu,wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia.”

      5. Kujihusisha na utii wa nje wa sheria ya Mungu. Marko 7:18-23; Mathayo 15:15-20,23:27-28.

      MATUMIZI YA SHERIA YALIYO SAHIHI NA WALA AGANO JIPYA HALIHUKUMU.

      1. Kufikiri kuwa sheria ya Mungu ya maadili ni njema sana, ya haki, takatifu na ya kiroho Rum 7:12,14; 1Timotheo 1:8 linganisha na zaburi 19:8-12; 119.

      2. Kutamani kushika amri za Mungu za maadili katika roho ya uana (wala si katika roho ya utumwa) na katika nguvu za Roho Mtakatifu. Rum 8:2-4;3:31.

      3. Kuwasihi wengine kwa msingi wa sheria ya Mungu, wakati hili lifanywapo kwa nia iliyo sawa. Efeso 6:1-4.

      4. Kutoa wito wa kushika sheria ya Mungu ya maadili. Yakobo 2:6-12; Rum 13:8-10.

      5. Kutekeleza nidhamu ya kanisa. Galatia 5:18-23; 1Timotheo 1:5-11.

      Pia tuelewe tu kwa ujumla ya kuwa INJILI na SHERIA husimama kinyume tu cha kila mmoja – hususani katika nyaraka za Paulo – iwapo “SHERIA” inaeleweka kama “WOKOVU kwa SHERIA”, lakini si iwapo SHERIA inaeleweka kama SHERIA ya MUNGU iliyoandikwa katika agano la kale.
      Pia angalia hili kuwa Paulo analiona tangazo la maelezo ya sheria na Hukumu ya Mungu juu ya dhambi maalumu kama sehemu ya “INJILI”

       
      • Kennedy Meshuck

        February 20, 2017 at 11:30 am

        Nashukuru kwa mtoa mada na kwa ajili ya wote waliochangia mada hii kulingana na uchunguzi na utafiti na ujuzi mlio nao juu ya neno la Mungu.
        Jambo la msingi ambalo Mimi napenda kuliongezea ktk mjadala huu ni kuhusu mafundisho ya Paulo kwenye Biblia, yasionekane yanapotosha imani ya wakristo. Mzee Petro alitoa onyo na kuwa makini sana kuhusu nyaraka za Paulo akisema,”…….kama vile ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa;vilevile kama ktk nyaraka zake zote pia, akitoa humo habari za mambo hayo; katika nyaraka hizo yamo mambo ambayo ni VIGUMU KUELEWA nayo; na mambo hayo watu wasio na elimu,wasio imara HUYAPOTOA, kama vile wayapotoavyo na MAANDIKO mengine,kwa UVUNJIFU WAO WENYEWE. 2Petro3:15-16.
        Kwa hiyo napenda nikuletee vitu vichache kuhusu matumizi sahihi ya sheria kwa kuonesha jinsi ambavyo Paulo anataka tuelewe ktk maandiko au nyaraka zake. Na ni imani yangu kuwa huu ndio mtazamo wa Paulo juu ya matumizi ya sheria na imani ya Mkristo.

        Hebu angalia na utafakari matumizi yafuatayo ya sheria katika Biblia. Kwa kuelezea nimeweka matumizi sahihi na matumizi yasiyo sahihi ya sheria kwa Wakristo. Nianze na matumizi yasiyofaa ya sheria kwa wakristo.
        MATUMIZI YA SHERIA YASIYOFAA KWA WAKRISTO

        1. Kushika sheria ili uhesabiwe haki na uokolewe au kupata wokovu kwa sheria. ” lakini haki ya Mungu imedhihirishwa pasipo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii; ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote waaminio.” taz Rum 3:21 – 4:25;. ” Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo hsikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo….”
        Efeso 2:8-10.

        2. Kulazimisha Sheria ya maazimisho kwa wengine Galatia 4:9-10; Kolosai 2:16-17.

        3. Kuongeza sheria ya mapokeo ya kibinadamu kwenye sheria ya Mungu. Marko 7:1-15; Mathayo 15:1-9.

        4. Kusahau mambo ya msingi na kupendelea mambo madogo madogo. Mathayo 23:23-24″ Ole wenu waandishi na mafarisayo, wanafiki, kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lkn mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache. Viongozi vipofu,wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia.”

        5. Kujihusisha na utii wa nje wa sheria ya Mungu. Marko 7:18-23; Mathayo 15:15-20,23:27-28.

        MATUMIZI YA SHERIA YALIYO SAHIHI NA WALA AGANO JIPYA HALIHUKUMU.

        1. Kufikiri kuwa sheria ya Mungu ya maadili ni njema sana, ya haki, takatifu na ya kiroho Rum 7:12,14; 1Timotheo 1:8 linganisha na zaburi 19:8-12; 119.

        2. Kutamani kushika amri za Mungu za maadili katika roho ya uana (wala si katika roho ya utumwa) na katika nguvu za Roho Mtakatifu. Rum 8:2-4;3:31.

        3. Kuwasihi wengine kwa msingi wa sheria ya Mungu, wakati hili lifanywapo kwa nia iliyo sawa. Efeso 6:1-4.

        4. Kutoa wito wa kushika sheria ya Mungu ya maadili. Yakobo 2:6-12; Rum 13:8-10.

        5. Kutekeleza nidhamu ya kanisa. Galatia 5:18-23; 1Timotheo 1:5-11.

        Pia tuelewe tu kwa ujumla ya kuwa INJILI na SHERIA husimama kinyume tu cha kila mmoja – hususani katika nyaraka za Paulo – iwapo “SHERIA” inaeleweka kama “WOKOVU kwa SHERIA”, lakini si iwapo SHERIA inaeleweka kama SHERIA ya MUNGU iliyoandikwa katika agano la kale.
        Pia angalia hili kuwa Paulo analiona tangazo la maelezo ya sheria na Hukumu ya Mungu juu ya dhambi maalumu kama sehemu ya “INJILI” katika 1Timotheo 1:9-11 na Rum 2:12-15.

         
  10. Daniel Kabuti Kanunga

    March 12, 2017 at 7:27 pm

    Ndugu rudia kusoma biblia. Lakini uanzapo anza na maombi huku ukimwomba Mungu akutumie mwalimu was biblia yaani Roho Mtakatifu ambaye ndiyo kazi yake hapa duniani. Yesu anasema “msidhani ya kuwa nalikuja kutangua torati ya MUSA au manabii la sikuja kutangua Bali kutimiliza..”(Matayo 5:17,18,19.) Halafu jambo lingine ambalo nitakanusha kwa mujibu was biblia, ni Sabato.Nilizima na ni wajibu wa kila mwanadamu kuitunza Sabato(amri ya nne) na haina kikomo Isaya 66:22-24;Ebr 4:4-9,10,12.

     
    • Daniel Kabuti Kanunga

      March 12, 2017 at 7:52 pm

      Mtu anayempenda Yesu atafanya nini?
      “Mkinipenda mtazishika amri zangu” John 14:15.Ni mini kinachoashiria watu was Mungu siku zote?
      “Hakika mtazishika Sabato zangu kwa kuwa ni ishara kati ya Mimi na ninyi katika vizazi vyenu vyote…Basi mtaishika hiyo Sabato; kwa kuwa ni takatifu kwenu..”

       
    • dsta12

      March 12, 2017 at 9:44 pm

      Inaonekana hujasoma makala nzima kwani nilijishughulisha na mistari ile. Ungalisoma makala nzima usingaliandika maneno yale.

       
  11. Faustine Paulin

    April 7, 2017 at 10:03 am

    Rafiki unajua unacho kitetea Jumapili kama siku ya ibada imeweka na mamlaka ya kanisa la Roma (Mt. silvester ) na kusisitizwa na Mfalme wa Roma ya kipagani Costantino mwaka wa 321.kama unahitaji rejea za vitabu vinavyo eleza jambo hili uliza nikupe.
    Na sabato (jumamosi) imewekwa na Mungu mwenyewe (Mwanzo2:1,2,kutoka 20:10,marko 2:28)Swali kwako, Unatii mamlaka ya Mungu au Mamlaka za wanadamu? Pamoja na ku ng’ang’ana kujitetea. ujue nakutambua wewesio wakwanza kujaribu kupambana na Mungu unafanya marudio tu!

     
    • dsta12

      April 7, 2017 at 2:36 pm

      Faustine, sawasawa na Wasabato karibu wote hapo juu, umeandika comment kama hujasoma hata ukurasa wa kwanza ya somo langu. Majibu na points zako hapo juu utapata kwenye somo. Karibu ulisome.

       
    • Robert J. Zingu

      August 19, 2019 at 10:40 pm

      Faustine Pauline,
      Mosi, sina hakika kama umeisoma makala yote na kuielewa. Labda ukirudia kuisoma, unaeweza kuja na mtazamo tofauti.

      Pili, nimesoma somo hili mwanzo mwisho. Ndugu David Stamen, hajatetea watu kuabudu/kusali Jumapili au Jumamosi

      Alichokisema na kwa kunukuu mistari mbalimbali ya Biblia (Neno la Mungu) kwa maana ya Injili ya Yesu Kristo na mafundisho ya mitume ni kuwa, kushika au kuabudu siku yoyote iwe Jumamosi ama Jumapili ama hata kama ni siku zote saba za juma (Jumatatu – Jumapili) unakesha na kulia ndani jumba la kanisa, kama hujapokea neema ya wokovu wa kweli wa Yesu Kristo (Bwana wa Sabato) ni kazi bure na ni kupoteza muda na nguvu zako…!!

      Mungu alimtoa mwana wake wa pekee Yesu Kristo ili afe na kutukomboa. Kwa njia anasema kuwa tunapompokea na kumruhusu kuingia ktk mioyo yetu kisha akayatawala na kuyaongoza maisha yetu , NEEMA yake ya kutenda sheria zote za Musa inakuwa imerahisishwa….!!

      Kwenda kanisani kila Jumamosi kwa mwaka mzima ikiwa wewe ni MSABATO au kila Jumapili kwa WAKRISTO wa madhehebu mengine kama utamaduni na desturi (sheria) za kidini bila uongozi wa Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wako, it’s absolutely useless and meaningless!!.

      Ibada ya kweli na sahihi iko ndani ya MOYO na NAFSI ya MTU na kamwe siyo nje ya MTU maana yeye mwenyewe amesema, ataziandika SHERIA zake ndani ya mioyo na nia zetu!!

       
  12. amos juma

    April 13, 2017 at 9:22 pm

    nifundishe nielewe

     
    • Anonymous

      April 26, 2017 at 3:03 pm

      Shalomu mtumishi wa mungu. Hongera kwa masomo mazuri.Japo nasikitika wengi wanaopinga ni kwamba bado hawakufunuliwa macho yao na ROHOMTAKATIFU kuyaelewa. Na sababu ni pale mtu anapofikiri kwamba anajua NENO la Mungu na huku hajui ipasavyo,na hayuko tayari kujulishwa.YOH 8:32

      Wako mchungaji ISRAELI toka Arusha. Karibu Arusha 0754357107

       
      • Anonymous

        January 13, 2018 at 5:26 pm

        Bwana awabariki wote wale walioelewa na wale ambao hawajaelewa kuhusu SABATO naamini Mungu atawafunulia na watampokea kuwa Bwana na mwokozi wao
        Mbarikiwe Sana kwa mjadala huo Amina

         
  13. Rashid

    May 4, 2017 at 6:19 pm

    Muandaajia wa masomo haya jaribu kutafuta design nzuri ya kuyawasilisha kwa hadhiya yako.. yaani sisi wasomaji. Ni marefu mno kiasi si rahisi mtu kuscrow hadi chini akisoma. Jaribu kuyaweka au kuyapangilia kwa section au kwa namna yoyote isiyochosha…tofauti na hapo kuwapata wa kusoma somo zima itahitaji a lot of energy ambazo sio wote wanazo. Kumbuka lengo lako ni kuwasaidia watu kuwa na neno la kristo ndani yao. ASante

     
  14. ANDREW GILAYDA

    July 27, 2017 at 12:22 am

    Nasikitika “Mtumishi wa Mungu” amefuta comment yangu baada ya kumwambia kuwa ni “nabii wa uongo”!

     
  15. dsta12

    July 27, 2017 at 7:26 am

    TANGAZO: WAPO WALE WALIOANDIKA KWAMBA MAMBO NILIYOYAANDIKA KWENYE MAKALA SIYO KWELI AU HATA NAANDIKA ‘UONGO’. LAKINI HAKUNA HATA MMOJA MIONGONI MWAO ALIYESEMA NILIKOSA WAPI! NAOMBA KAMA UKIFIKIRI NILIKOSA, WAAMBIE WATU NI WAPI KATIKA MAKALA. SENTENSI IPI SIYO KWELI? WATU HAWAWEZI KUFUNDISHWA CHO CHOTE KAMA USIPOTAJA NILIKOSA WAPI KWENYE MAKALA. KUSEMA NILIKOSA AU NI UONGO TU HAITOSHI. MTU ASIPOFANYA HIVYO, NITAFUTA COMMENT YAKE. ASANTEENI.

     
  16. Alex

    January 8, 2018 at 9:46 am

    ILIKUWA NI DESTURI YA MITUME NA KANISA KATIKA AGANO JIPYA KUABUDU KATIKA SIKU YA SABATO YA JUMAMOSI

    Matendo ya Mitume 13:14
    Lakini wao wakatoka Perge, wakapita kati ya nchi, wakafika Antiokia, mji wa Pisidia, wakaingia katika sinagogi siku ya SABATO, wakaketi.

    Matendo ya Mitume
    13:27 Kwa maana wakaao Yerusalemu, na wakuu wao, kwa kuwa hawakumjua yeye, wala maneno ya manabii yanayosomwa kila SABATO, wameyatimiza kwa kumhukumu.

    Matendo ya Mitume 13:42
    Na walipokuwa wakitoka, wakawasihi waambiwe maneno haya SABATO ya pili.

    Matendo ya Mitume 13:44
    Hata SABATO ya pili, watu wengi, karibu mji wote, wakakusanyika walisikie neno la Mungu.

    Matendo ya Mitume 15:21
    Kwa maana tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila SABATO katika masinagogi.

    Matendo ya Mitume 16:13
    Hata siku ya SABATO tukatoka nje ya lango, tukaenda kando ya mto, ambapo tukadhani ya kuwa pana mahali pa kusali; tukaketi, tukasema na wanawake waliokutana pale.

    Matendo ya Mitume 17:2
    Na Paulo, kama ilivyokuwa desturi yake, akaingia mle walimo, akahojiana nao kwa maneno ya maandiko SABATO tatu,

    Matendo ya Mitume 18:4
    Akatoa hoja zake katika sinagogi kila SABATO, akajaribu kuwavuta Wayahudi na Wayunani.

    Unapochukua hivo vifungu vyako viwili vya siku ya kwanza ambavyo havina uhusiano na kuabudu kusema ndo desturi ya kuabudu siku ya kwanza unakua hauko serious…

     
    • dsta12

      January 8, 2018 at 1:03 pm

      Alex, ulinukuu yafuatayo: “Lakini wao wakatoka Perge, wakapita kati ya nchi, wakafika Antiokia, mji wa Pisidia, wakaingia katika SINAGOGI siku ya sabato, wakaketi.” Matendo ya Mitume 13:14.
      Lakini ni wazi kabisa mtume Paulo na wenzake walikwenda SINAGOGI kwa LENGO LA KUHUBIRI INJILI KWANZA kwa WAYAHUDI, kwa hiyo tunasoma kwenye sura ileile, “Paulo na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe KWENU KWANZA; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili uzima wa milele, angalieni, twawageukia MATAIFA.” Matendo ya Mitume 13:46.
      Ukweli huu unahusu kila mstari uliounukuu – inahusu makusanyiko ya WAYAHUDI ambao hawajasikia Injili. Haihusu makusunyiko ya Wakristo ambao walikusanyika kwa kawaida jumapili kama neno la Mungu linasema.
      Unaandika kama hujasoma Makala. Vipi huwezi kutambua yaliyo wazi kabisa, yaani, mistari ile uliyoinukuu inahusu makusanyiko ya Wayahudi? Unadhihirisha kwa maneno yako kwamba upo tayari kuharibu maana ya neno la Mungu ili ushike mafundisho yenu.

       
    • Laurent john

      May 24, 2022 at 12:56 pm

      NGOJA NIMSAIDIE MTUMISHI KUKUJIBU.
      je unaijua sabato ya pili ? Tena tumia maandiko hayo uliyo ya tuma mfano matendo 13:44, kuna watu hawa kuelewa kama wewe japo mitume walikua wamemaliza kuwa fundisha kuhusu sabato, wakataka kujua zaidi.
      Hawa kuelewa kwa sababu walikua tayali wamekumbatia sabato yao kama wewe ivo,
      Soma tena matendo 13:42, ukiweza kufahamu sabato ya pili basi umetoka kwenye kifungo,
      Pia Agano la kale lilikua na taratibu zake za kila kitu mfano ibada, pumziko ambayo ni sabato n.k lilipo ondolewa likaja jipyq, imara na hili lina sabato yake ya uumbaji mpya n.k njoo whatsapp nikusaidie usipo tee 0716806911 , mtumishi wa somo hili yuko sahihi kabisa.

       
  17. dsta12

    January 8, 2018 at 7:08 pm

    Alex, naomba wape watu mstari mmoja katika Agano Jipya ambao unaonyesha au kufundisha WAKRISTO baada ya kufufuka kwa Yesu walikusanyika siku ya sabato. Karibu.

     
  18. dsta12

    January 9, 2018 at 10:33 am

    Alex, alinukuu Isaya 66:22,23 na unataka kujadili juu ya fungu hili kama sijajishughulisha na point hiyo kwenye Makala yangu. Nimeshajishughlisha na mistari hiyo kwenye Makala – kama nilivyofanya juu ya point zako zote. Je, umesoma Makala? Kwa nini nikariri hapa tayari niliyoyaandika kwenye Makala? Hujali kabisa niliyoyaandika kwenye Makala, Alex, na unataka niweke post zako zote hapo kana kwamba sijaandika chochote. Hiyo siyo haki. Tena naomba wape watu mstari mmoja katika Agano Jipya ambao unaonyesha au kufundisha WAKRISTO baada ya kufufuka kwa Yesu walishika siku ya sabato. Mistari uliyoinukuu mpaka sasa kwenye Matendo inahusu kazi ya kuhubiri Injili kwa wasioamini, wawe Wayahudi , wawe Wamataifa. Karibu. Usipotoa mstari, watu wote watajua fundisho lako halina msingi katika Agano Jipya.

     
  19. Abel Moranga Onwonga

    February 17, 2018 at 6:10 pm

    Nimeshukuru kwa mafundisho .Nataka kujua Sana.

     
  20. Anonymous

    October 4, 2018 at 10:49 am

    Mungu akubariki sana mtumishi naendelea kujifunza vingi vzur

     
  21. majogo

    October 4, 2018 at 10:51 am

    Mungu akubariki sana mtumishi naendelea kujifunza vingi vzur

     
  22. majogo

    October 4, 2018 at 10:52 am

    Amen

     
    • Mwj. Edwin Benjamin Ernest

      October 31, 2018 at 8:33 pm

      Nakushukuru Mtumishi wa Mungu kwa somo zuri
      Kama wasabato wanaishika sheria na sabato mbona wamebaki na sabato ya siku katika juma tu,wakati kuna sabato ya mwezi,mwaka n.k na inatakiwa warushe jiwe na pale linapoishia ndipo mwendo wao uishie siku ya sabato wanayatimiza?

       
  23. Mary Mlola

    December 21, 2018 at 4:36 am

    Mtumishi Mungu akubariki sana….umeeleza vizuri mno…Hapo ni kumuomba Mungu afungue fahamu zao ili waielewe kweli ya Mungu wa ibrahimu, Izaka na Yakobo ni ipi na waachane na mapokeo….Mungu akupe imani na akufikishe mbinguni mtumishi……..

     
    • Anonymous

      October 15, 2019 at 5:16 am

      ni kwenye sabato hii ndipo palipo na muhuri wa Mungu hivyo watu wataletwa hukumuni kwa kwa uasi huu wa kuikataa amri halali ya Mungu

       
  24. lucas atilyo

    February 8, 2019 at 1:06 pm

    am blessed with this lesson, may God bless you!. nnachoshangaa mimi kwanini hawayaoni yote haya?!

     
  25. ASWILE MASEBO

    June 10, 2020 at 11:05 am

    nashukuru kwa mafundisho yote yaliyopita, nimekuwa nikichanganyikiwa kwanini watu wanasisitiza maandiko katika agano jipya? ina maana agano la kale limepitwa na wakati? na kama ndivyo kwanini mpaka sasa tunahubiriana kuhusu kushika amri za Mungu k.mf usiibe, usizini,usimshuhudie jitani yako uongo n.k wakati hayo yote yanapatikana katika agano la kale? naombeni majibu tafadhali ili niondokane na utata niliouona katika hii sayari ya tatu ya sintofahamu. ahsante

     
    • dsta12

      June 10, 2020 at 1:01 pm

      Asante Aswile. Kutokana na maswali yako inaonekana hujasoma makala yangu nzima au hujaelewa. Aidha, inaonekana huelewi tabia ya Agano Jipya. Majibu unayoyatafuta tayari yapo kwenye makala yangu na kwenye mafundisho ya mitume katika Agano Jipya.

       

Leave a reply to dsta12 Cancel reply