RSS

NGUVU YA FIKRA CHANYA: USIKATE TAMAA!

‘NGUVU YA FIKRA CHANYA’. USIKATE TAMAA! (The power of positive thinking.)

Inaniumiza moyo kuona watu wengi siku hizi, hasa vijana wanadharau neno la Mungu, na pengine hata kuachana na neno lake kabisa kwa sababu ya kufuatisha au kutafuta kutimiza kile wanachokiita ‘kusudi’ au ‘hatma’ katika maisha. Wanadhani wanatakiwa kula na kunywa kutoka katika chanzo kingine tofauti na neno lake Mungu – na chanzo wanachotumia kula na kunywa ni filosofia za dunia hii, mawazo na fikra za wasiowaamini, wale wasiomjua Mungu, waishio pasi kumtegemea Mungu bali akili na nguvu zao binafsi kutimiza ndoto zao na hatmaye kufanikiwa. Kwa hali hii, hunywa toka kwenye mto utiririshao mkondo wake wa maji toka kwa ibilisi mwenyewe.

Wanafuatisha mafundusho ya udanganyifu. Mafundisho haya yaliibuka miaka ya 1950, japokuwa kuna mafundisho tofauti tofauti ya namna hii wote huandika kwa kichwa cha habari kinachowiana na hiki,  ‘Nguvu ya Fikra Chanya’. Wahubiri wengi maarufu wajiitao wakristo huyapigia debe mafundisho haya, na wale wenye uchu wa kufanikiwa kwenye taaluma zao na biashara kuliko kumfuata Yesu wamevutwa sana na kuyakubali mafundisho haya japo hayamo ndani ya maandiko ya Biblia. Fundisho mahsusi la ‘Nguvu ya Fikra Chanya’ ni lipi hasa? Wanafundisha nini watu hawa ambao humweka Mungu kando kabisa? Nitanukuu baadhi ya misemo yao utumikao zaidi, eti husema hivi,

‘Kila jambo hutegemea mtazamo wako; kama unataka kufanikiwa unahitaji kubadili mtazamo wako; mtazamo wako ukiwa hovyo huwezi kufanikiwa na utakuwa masikini miaka nenda rudi. Badili kufikiri kwako; uwe na fikra chanya tu na utafanikiwa. Kesho yako i mikononi mwako; kila jambo hutegemea maamuzi unayofanya mwenyewe; anza kunia makuu, anza kuunda ndoto kubwa, anza kujitafakarisha mambo makubwa. Jiamini; pambana na mwisho utashinda; usikate tamaa, usivunjwe moyo, njia ya mafanikio imejaa na vikwazo vya kufisha moyo kwa hiyo usikate tamaa. Lenga fikra zako kwenye mambo yatakayokusaidia kutimiza hatma yako. Ambatana na watu ambao watakusaidia kufikia ndoto zako. Unawezaje kufikia hatma yako kama hujagundua kusudi lako.”

Nilichonukuu ni baadhi ya kauli za wale wanapigia debe mafundisho ya ‘Nguvu ya Fikra Chanya’. Wapi walitaja ‘Mungu’ au ‘Yesu’? Hamna! Waliwaondoa kautoka katika fikra zao! Huu ni upinga Kristo, ama labda twaweza kusema ni mafundisho ya mpinga Kristo ya wale wasioamini, waliogeuza njia zao mbali na Mungu na wanataka kutimiza malengo yao na ndoto wakiamini ni juhudi zao na machaguo yao yatawapa kufanikiwa.

Inashangaza na kushtusha mno kuona kundi kubwa la wakristo wanabeba vichwani mafundisho haya  ya kujitegemea wenyewe yasiyopatana na Biblia. Hayamhusishi Mungu, hayamhusishi Kristo, bali wewe unakuwa kitovu cha mafanikio yako. Hakuna hata kauli moja niliyonukuu hapo juu itokayo ndani ya Biblia ama kuhusiana na Biblia kabisa. Pamoja na kwamba kuna baadhi ya maneno ni sawa na yaliyomo kwenye Biblia lakini dhana, dhima na hata vyazo vyake zi tofauti kabisa – ni kama utofauti kati ya nuru na giza. Kauli zote hizi hukuongoza katika kujiamini mwenyewe, maamuzi yako, uwezo na nguvu binafsi. Unachotaka wewe mwenyewew ni kitovu wa maisha yako sasa.

Na hata hivyo, baadhi ya kauli zina viashiria vya ukweli ndani yake, ni kama tu vile shetani kwa kile achomwambia Eva kwamba wangefanana na Mungu kama wangekula tunda katika mti wa ujuzi wa mema na mabaya; maana baada ya kula tu, Bwana Mungu anasema, ‘Tazama mtu amekuwa mmoja wetu, ajue mema na mabaya’. Kwa hiyo maneno ya ibilisi yalikuwa na viashiria vya ukweli ndani yake lakini haukuwa ukweli wote, haukuwa ukweli timilifu. Kwa hivyo ikawapelekea kutenda dhambi, kujitenga na kutomtegemea Mungu. Na HIVYO NDIVYO mafundisho tajwa hapo juu yatakutenda kama utayashika katika maisha yako.

Msemo wao mmoja husema, ‘Mungu hukubariki rohoni tu, lakini ni utashi wako utakaokupa kung’ara zaidi kimafanikio.’ Fikra hizi si kwamba zinatoka nje ya Biblia lakini huwakilisha matukano dhidi ya Mungu. Ni kashfa kwa Mungu. Tazama, yeye anajua kama shomoro wakidondoka juu ya ardhi, anashindwa vipi kujua kila hatua ya maisha yangu na yako? Mungu anatufahamu kwa kina, anafahamu yote kutuhusu, toka tuamkapo hata muda tulalapo usiku.

Tunadhani kweli Mungu haguswi na machaguo yetu, kwamba hajihangaishi na mwelekeo ambao maisha yetu inabidi yaufuate? Tunafikiri zipo nyakati inabidi tujichagulie vya kufanya pasi kumhusisha Mungu ili tupenye kimafanikio? Tunafikiri hivyo kweli? Je? Hatusomi Biblia? Tu wafuasi wa Kristo au la? Imeandikwa kwenye waraka wa Waefeso ile sura ya pili na mstari wa kumi kwamba

“Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu tutende matendo mema AMBAYO TOKEA  AWALI MUNGU ALIYATENGENEZA ILI TUENDANE NAYO.”

Tunaujua mstari huu? Ama tunajiona tu salama tunapojiondoa mikononi mwa Mungu, nje ya maongozi yake na kufuatisha tuamuavyo? Hivi kweli tunafikiri kwa kukabidhi maisha yetu kwa Kristo na kumwamini kwa kila hatua tupigayo ambapo nyakati zingine huwa tunakosea; kwamba kufanya hivyo kutatukosesha hatma zetu? Mungu ndio dira na mwongozo wa maisha yetu, ni kila kitu maishani mwetu. Ndivyo ama sivyo?

Ni wazi kwamba kupitia jumbe ambazo watu wengi hutuma kwenye mtandao wa Facebook hawaijui Biblia, kwamba hawaongozwi na neno la Mungu kwenye maisha yao, hawafahamu asili ya Mungu na yeye ni nani hasa; zaidi hawajui kwamba hawajimiliki tena bali wanamilikiwa na Yeye aliyewapenda na kuwafia.Tunaewezaje kufikiri kwamba njia pekee ya kufikia malengo na “ndoto” zetu ni kwa kutumia fikra zetu chanya, na kama tusipofuata njia hii inamaanisha kuachwa pasipo msaada, kama kipande cha ubao kinavyosafiri juu ya maji, huku ni kuongozwa na masumbufu ya maisha pasipo mwelekeo, bila hatma wala tumaini.

Inawezekanaje wakristo wawe na mtazamo wa namna hii? Kama twazungumza kuhusu kubadili mtazamo wetu ili kubadililisha maisha yetu, basi mtazamo huu wa uongo na kashfa hii kwa Mungu ni mtazamo unaohitaji mabadiliko. Kutofuata mafundisho ya mpinga Kristo ya nguvu ya fikra chanya haina maana kwamba utayasumbukia maisha yako! Yupo Mungu akupendaye sana hata alimtoa mwanae afe kwa ajili yako, si kwa ajili ya kukusamehe tu, bali kukuokoa toka katika dhambi na kukubariki kwa baraka za rohoni zitokazo mbinguni. Lakini zaidi, anayo njia ya kukupitisha. Je, unatamani kujua mapenzi Yake juu ya maisha yako? Je, unautafuta ufalme na haki Yake kwanza? Sasa kwa nini unywe sumu toka katika mto wa nguvu ya fikra chanya? Je, unaogopa? Waogopa kweli kweli? Je! Ni kweli unaamini kwamba kwa kumwamini Mungu, kwa kuweka maisha yako mikononi mwake, kwa kumkabidhi kabisa kila hatua upigayo unaweza kukosa mambo au vitu ambavyo Mungu amekuandalia?

Unataka Mungu aziongoze hatua zako au unataka ujichagulie na kupita pasi kupata maelekezo yake? Inafikia hatua huwa najihoji mwenyewe kuhusu kinachofundishwa makanisani, ni kweli kabisa vijana wamebadilishwa na kuletwa kwenye wokovu uliomfanya Kristo afe?

Ni sehemu gani katika Biblia ambapo panaeleza kuwa ‘jitumainie mwenyewe’, au ‘uwe na mtazamo chanya na kisha utaweza kufanikiwa’, au kwamba ‘kubadilisha mtazamo ndio siri ya mafanikio’? Kwa nini sasa waumini wengi badala yake hawanukuu Biblia ili kutiana moyo wao kwa wao? Nafikiri sababu yao kubwa ni hii hapa: neno la Mungu halitupatii sisi fursa ya kuchagua kwenda njia zetu wenyewe. Na hilo ndilo haswa watu wanalolitaka kulifanya nyakati hizi za leo – ingawaje bado wanasema kuwa wao ni wafuasi wa Yesu Kristo. Wao wanayafuata mafundisho ya wasioamini kupitia mafundisho ya nguvu ya fikra chanya ili kwamba wapate KILE WANACHOKITAKA KWELI KWELI, huku wakijidhihirisha wazi kuwa IONEKANE kuwa hayo ndiyo mapenzi ya Mungu katika maisha yao! Kwa nini waumini hawa hawanukuu moja ya mistari muhimu sana na yenye kutia moyo kutoka ndani ya Biblia ambayo inahusiana na somo kama hilo? Kama vile Mithali 3:5-6, mstari unaosema, ‘MTUMAINI BWANA kwa moyo wako WOTE na wala USIZITEGEMEE AKILI ZAKO MWENYEWE. KATIKA NJIA ZAKO ZOTE MKIRI YEYE NAYE ATANYOOSHA MAPITO YAKO”. Kwa nini basi hawanukuu mstari kama huu? Sijaona popote katika kurasa za facebook ikizingatia juu ya maisha yetu yajayo. Je wanafikiri kuwa Mungu hawezi kuwaongoza wao ili kutimiza makusudio YAKE katika maisha yao? Je, hivyo ndivyo wanavyofikiri kumhusu Mungu? Mimi binafsi ninafikiri kuwa sehemu ya sababu zao kufanya hivyo ni hii hapa, kwamba mstari huu kama ilivyo mistari mingineyo ndani ya Biblia inamwingizia Mungu katika maswali, inamleta Mungu katika mazingira, inamleta Mungu katika maisha yako! KISHA PANA HOFU KUWA MAMBO YALE NINAYOYATAKA BINAFSI YANAWEZA YASIJE KUTOKEA! Na HII NDIYO SABABU YA UMAARUFU WA FUNDISHO HILI la nguvu au uweza uliomo katika fikira chanya! JAMBO HILI LINAWEKA MFUMO WA MAAMUZI NDANI YA MIKONO YA MTU, NA SIO KATIKA MIKONO YA MUNGU. Ni fundisho la kipagani, watu wasiomjua Mungu na kumtegemea.

Kwa nini waumini hawanukuu kutoka kitabu cha Zaburi 37:5, mstari ambao unasema kuwa, “Mkabidhi Bwana njia zako, mtegemee yeye, naye atakufanikisha.” Wazo kwamba Mungu anatubariki sisi kiroho ‘tu’ na kwamba kwa hiyo tujichukulie hatua ya kujiongoza katika maisha yetu kwa kufanya chaguzi zetu wenyewe tu, ni jambo la udanganyifu mkubwa. Ndiyo, kwa vyovyote tunapaswa kufikiri juu ya mambo fulani fulani, tunapaswa pia kufanya maamuzi juu ya mambo fulani, kwa vyovyote zipo fursa ambazo tunahitaji kuzipatia umuhimu. Hii ni hali ya kawaida kabisa katika maisha yetu. Wala hii sio sayansi ya roketi, hii siyo mambo ya mafumbo yaliyojificha. Hii ni kweli ya kila mtu aliyepata kuishi!  Swali ni hili, je, utatoa maisha yako, kwa kila hatua unayochukua, kwa kila fursa inayokuja katika Mungu aliye hai!? Hili ni jambo la muhimu tu! Huo ndio moyo wa jambo lenyewe! Kule kukabidhi kila hatua tunayoichukua katika maisha yetu, kila maamuzi tunayotaka kuyafanya mikononi mwa Mungu, haiyeyushi kusudi lake kwetu hapa duniani wala yale makusudi yake ya umilele ndani yake na kupitia yeye! Je, ingekuwaje?

Watu wanapenda kuyapa uthamani mafundisho ya aina hii ya uasi kwa kisingizio kuwa ni neno la Mungu, kwa kuinukuu Biblia! Hivyo wananukuu sura ya 37 ya Zaburi ule mstari wanne ambao unasema kuwa, “Nawe utajifurahisha kwa Bwana naye atakupa haja za moyo wako.” Na ndipo watu hao husema, “Unaona! Mungu anataka kukupa wewe matakwa/haja za moyo wako!” Na kwa kuamini hilo ndipo hufungua mlango kwa kila ndoto zao binafsi, mataamanio waliyonayo pasipo hata kufikiria kwa ukweli juu ya nini mapenzi ya Mungu hasa katika maisha yao! Kwa kufanya hivyo wafanyavyo, wanasahau sehemu ya kwanza ya mstari huo isemayo kuwa “utajifurahisha kwa Bwana.”

Tatitizo hapa ni kuwa katika kitovu wa jambo lenyewe waumini wengi wanajifurahisha wenyewe kwa matamanio yao na ndoto zao tu. Ndipo hutumia mistari hiyo ili waweze kuyafuata matamanio yao! Kimsingi ni jambo la kujipendeza na kujifurahisha kuliko kutafuta, kufuata na kutimia mapenzi ya Mungu katika maisha yao. Ukijifurahisha katika Bwana, na ikiwa yeye ndiyo furaha yako, na ndiye pendo lako, basi litakuwa ni jambo la kawaida tu kwako kutafuta mapenzi yake na kuyafanya katika maisha yako!  Kama vile mwimba zaburi alivyosema, “Kuyafanya mapenzi yako ee Mungu wangu ndiyo furaha yangu.  Naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” (Zab. 40:8). Unaona? Neno la Mungu limo moyoni mwa Daudi, lakini watu wengi nyakati hizi za leo, mioyo yao imejazwa na ‘ndoto’ yao na ‘malengo’ yao au hatma yao, na neno la Mungu limeweka kando.

Wakristo wengi wachanga hujikuta wamedondokea katika mitego ambayo mtume Yakobo alishaonya. Katika nyaraka zake ile sura ya nne,  mstari wa 13 hadi kumi 16 unasema hivi, “Haya basi, ninyi msemao, ‘Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida’; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, ‘Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.’ Lakini sasa mwajisifu katika majivuno yenu; kujisifu kote kwa namna hii ni kubaya.”

Vivyo hivyo leo hii waumini wengi wanajivuna na kujifurahisha wao wenyewe katika mawazo yao tu   kuwa wanaweza kutimiliza mawazo ya matamanio yao na hatma yao kwa kutumia mawazo yao chanya, pasipo hata kuachilia au kukatishwa tamaa na kitu chochote kile. Neno la Mungu linasema kujivuna huko kote pamoja na kujifurhisha huko ni uovu tu. Huo ndio ukweli ulio wazi na rahisi. Ebu tuwe wazi hapa. Hapa si suala la kujiuliza kuwa je, tunapaswa kuwa na mipango kwa ajili ya maisha yetu ya baadae au la? Hapana. Lakini jambo la kuzingatia zaidi hapa ni iwapo kama unajukumika katika mambo ya Mungu na mapenzi yake katika maisha yako juu ya yale mambo unayoyapanga kuyafanya. Jakobo alikuwa hawashutumu watu kwa kule kuwa na mipango yao. Hapana. Bali yeye alikuwa anawakemea kwa kutokuwajibika kwao katika mambo ya Mungu pamoja na mapenzi yake. Alikuwa anawakemea kwa kule kutekwa kwao na mawazo ya mafanikio na mafanikio yao ya maisha ya baadae, na kule kumsahau Mungu wanapoendelea kutimiza mambo yao hayo. 

Kumtegemea Mungu hakumaanishi kuwa sasa wewe unazizima akili zako kama vile unavyozima computer, wala haimanishi kuwa sasa unaacha kufanya maamuzi yako au mipango yako. Haimaanishi kuwa sasa uwe mvivu. Bali inamaanisha unajukumika katika mambo ya Mungu na mapenzi yake katika kila jambo ulifanyalo. Inamaanisha kujitoa mwenyewe kwake kama dhabihu iliyohai kwa mujibu wa kila hatua kubwa unayoichukua katika maisha yako, ukitafuta uthibitisho wake na kibali cha melekezo yake.

Hii inauchukua utumwa wote wa ‘fikra chanya’, yaani fikra zifuatzo, “Oh, sasa napaswa kuwa chanya.  Napaswa kutunza hali ya kuwa na mtazamo sawa. Siwezi kushindwa, wala sitakata tama, haijalishi watu wasemalo; nitasonga meble, nitafanikiwa, nitafanikiwa, nitatimiza ndoto yangu, nk. nk.” Je, tayari umeshatambua kuwa katika mawazao hayo hawataji Mungu? Ni vivyo hivyo katika mitandao ya kijamii – waumini (?) wengi wanaandika mawazo kama hayo bila kutaja Mungu – ili waweze kufanya wapendalo. Tunaweza kusema pamoja na Mariamu, “wamemwondoa Bwana wangu, wala mimi sijui walikomweka!”

Kama maisha yako yamejikabidhi kwake Bwana na kama unakabidhi kila hatua ya maisha yako kwake na kutafuta uthibitisho wake pamoja na maelekezo yake, ndipo utakapopata amani katika moyo wako, amani ile ipitayo ufahamu wote! Unaweza kuwa na furaha pamoja na ujasiri unaotokana na kule kujua kuwa unatembea katika mapenzi yake. Imani na amani hii ni hakikisho dhidi ya kila kukata tama na magumu yote yanayojitokeza.

Amani yako na ushindi wako unaoupata hautokani na kufikiri chanya kwako, bali inatokana na ile hali yako ya kumwamini Mungu na kujitoa kwako Kwake!

Sasa unaweza kuwa huru kutoka katika huko kazi ngumu ya kushugulisha sana akili kuhusu kuwa na mtazamo chanya, na uuwekee mbadala kwa kumwamini Mungu kwelikweli na kumtumainia Yeye. Yeye ndiye awezaye kukuongoza wewe kwenye njia uliyoichagua – kwa upande mwingine, anaweza kukuongoza wewe katika njia usiyoichagua na badala yake akakuongoza kuelekea kwenye njia nyingineyo sawasawa na mapenzi yake. Je, umejiandaa kuishi kwa jinsi hiyo au la?

Watu wengine wanadai kama huitumii “nguvu au uweza wa kufikiri chanya” katika maisha yako, basi utakuwa mtu uliyelegea mtazamaji tu, unayebebwa na mazingira ya maisha na hujui mwelekeo! Kufikiri kwa mtindo huu huko sio kufikiri hata kidogo!  Na wala sio kutumia akili zetu! Biblia imejaa mausia mengi na kutiwa moyo!

Tumeambiwa katika kitabu cha Warumi 12:11 kuwa ‘kwa bidii tusiwe walegevu, mkiwa na juhudi katika roho zenu’ katika mambo tuyafanyayo, na kwamba kila jambo tulifanyalo liwe ni katika neno au matendo yote tuyatimilize katika jina la Bwana Yesu, tukimshukuru Mungu na Baba kwa yeye (Wakolosai 3:17). Mtume Paulo anawaambia Wathesalonike kuwa kama mtu ni mvivu na hataki kufanya kazi basi asile pia (2 Wathes.3:10). Kuhusu maisha yetu ya baadae na lile kusudi lake Mungu kwa ajili ya maisha yetu ya baadae, Biblia haituambii lolote kuwa inakupasa kufikiri kwa mfumo ulio chanya!  Wala Biblia haituambii kwamba tuwe na tabia iliyo chanya ili kwamba tupate mafanikio katika maisha yetu. Kuhusu mapenzi yake Mungu kwa ajili ya maisha yetu ya baadae tunachopaswa kukifanya ni kule kufanyika upya katika nia zetu – hilo ndilo fundisho la Biblia. Hivyo tunasoma katika Warumi 12:1,2,

“Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”

Hayo ni mafundisho ya neno la Mungu juu ya maisha yako ya leo na kwa ajili ya maisha yako ya baadae! Kwa nini waumini wanajishughulisha na mambo matupu na yasiyofaa ya ‘fikra chanya’?

Je, unafikiri kuwa matumaini yako na matamanio yako na hatma yako ipo katika kutishiwa iwapo utaamua kufanya hivi, kufuata neno la Mungu, kuishi sawasawa na neno la Mungu? Inaweza kuonyesha kuwa wengi wanafikiri ndiyo hivyo. Hasa kwa vile wananukuu tu kuhusu nguvu ya fikra chanya. Unawezaje kufanya upya katika nia zako ili kuyajua mapenzi yake Mungu iwapo unaujaza moyo wako na nia yako kwa mawazo yaliyo chanya kuhusu maisha yako yajayo pia! Hii ni thibitisho tosha kwa hakika kuwa upo mbali sana na Mungu, kwa hakika ni katika maisha haya na pia unahatarisha maisha yako yajayo.

Kama nilivyokwisha kusema hapo juu, ni kutokana na kujikabidhi sisi wenyewe kwa Kristo mara zote ndipo tunapata uelewa na uthibitisho wa wema wake, kukubalika na mapenzi yake ya utimilifu! Huu ndio ujasiri na amani tuliyonayo katika kukabiliana na mambo mbalimbali magumu yanapotujia.Ni kutokana na ujasiri huo na amani tuliyonayo hivi ndivyo vitu vinavyo shughulikia sana na kukata tamaa kokote kule kunako weza kutujia. Hupambani na kukatatamaa kwa kuushambulia kukatatamaa (kwa kutumia mawazo yako chanya) isipokuwa tunafanya hivyo kwa kuweka imani na matumaini yetu kwa Mungu. Kile ambacho watu wengi wanapost/weka kwenye mitandao ya kijamii kuhusu fikra chanya na jinsi ambavyo kila kitu kinapaswa kutegemea mtazamo wako au fikra zako, mambo kama hayo yanamwondoa Mungu nje ya swali, nje ya fikra za mifumo ya watu wanavyofikiri, pia nje ya maisha ya watu!

Watu hunukuu maandiko ili kuyapata mawazo ya watu waumini, kwa hiyo kwa mfano wananukuu Mithali 23:7, pale pasemapo kuwa, “kama mtu afikirivyo moyoni mwake ndivyo alivyo.” Kwa hiyo wale wanaotaka kujikuza wenyewe na kumkataa Mungu, husema kuwa, ‘Unaona mtazamo wako/fikra zako ni muhimu sana, jinsi unavyofikiri ndani ya moyo wako ndivyo inakutafsiri wewe. Ndiyo, kwa vyovyote mtazamo na kufikiri ni vitu muhimu, vitu vya msingi sana! Lakini sasa usisahau kuwa ni neno la Mungu ndilo linalotuchonga sisi vizuri kitabia na kufikiri. Neno la Mungu linatuelekeza sisi kwenye aina ya tabia tunayopaswa kuwa nayo, na namna ya kufikiri tunakopaswa kujishughulisha nako! Tunapaswa kuwa na imani katika Kristo, na kumtegemea Mungu katika mambo yetu yote! Huu ndio mtazamo wa kimsingi kabisa! Tunapaswa kufurahi katika Kristo Yesu mara zote!

Kuhusiana na namna ya kufikiri kwetu, ebu soma katika Wafilipi 4:8, ambapo panasema, “Hatimaye ndugu zangu, mambo yoyote yaliyo ya kweli, yoyote yaliyo ya staha, yoyote yaliyo ya haki, yoyote yaliyo safi, yoyote yenyekupendeza, yoyote yenye sifa njema, ukiwapo wema wowote, ikiwapo sifa nzuri yoyote yatafakarini hayo.” Nadhani kuwa kwa wengi mistari hii waiona haiwapi haki sana kana kwamba kule kufikiri chanya kwao kuhusu jinsi gani mafanikio ya elimu yao inakwenda kuwa katika maisha yao!

Kuhusu mtazamo wetu, nao pia tunao maagizo ya wazi kabisa katika Wafilipi kwenye ile sura ya 2, pale ambapo Paulo anasema kwenye ule mstari wa tano, “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwemo pia ndani ya Kristo Yesu.”

Ni mstari wa ajabu sana! Kuwa na nia ile ile ya Yesu ndani yetu. Je, hiyo ndiyo nia unayoitaka? Soma nusu ya sehemu ya kwanza ya sura hiyo ili kupata muktadha kamili na baraka zake! Kama wewe unataka kubadili mtazamo wako, unaonaje kama utauchukua mtazamo wa mtume Paulo, ambaye anasema katika Wafilipi ile sura ya 3 mistari ile wa 7-8, “Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo, Naam zaidi ya hayo nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Yesu Kristo Bwana wangu, ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama MAVI ili nipate Kristo.”

Je, hiyo ndiyo mtazamo wako! Kwa kujilinganisha na kumjua Kristo, kila kitu kingine ni kama mavi? Huo ndio mtazamo wako?

Watu huongelea kuhusu kufuata malengo yao au ndoto zao. Sawa, mtume Paulo alikuwa na malengo. Paulo alikuwa na lengo moja, kusudio moja, alisema hivi, “Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 3:13-14).

Kwa hiyo kama unaamini kuwa tunatakiwa kubadilisha mtazamo wetu, je, ni aina hii ya mtazamo ambao unafikiri kuwa tunapaswa kuwa nao? Je, hiyo ndiyo mtazamo wako? Je, ndio lengo lako? Au labda unafikiri kuwa mtazamo wa aina hiyo ulikuwa ni kwa mtume tu? Lakini sasa ebu soma ule mstari unaofuata nawe utagundua kuwa kumbe, hii haikuwa kwa ajili ya mitume pekee, isipokuwa Paulo anataka watu wote wawe na mtazamo huo! Paulo anasema kama unataka kuwa na mtazamo nzuri, kama utakuwa na ukamilifu katika kufikiri kwako, ndipo uwe na mtazamo huo!

Mapenzi ya Mungu katika maisha yako ni yapi? Neno la Mungu linakuambia, “Maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati; kila mmoja wenu ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima.” (1 Wathes. 4:3,4). Ikiwa utaangukia katika usherati / zinaa wakati unapoendelea kushughulikia elimu/shughuli/biashara yako ya mafanikio, basi elimu yako hiyo yenye mafanikio itakuokoaje wewe siku ile?! Mapenzi ya Mungu ni yapi katika maisha yangu? Neno la Mungu linaniambia, “Furahini siku zote; ombeni bila kukoma; shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu.”(1 Wathes. 5:16-18). Unaweza kupenda kuniuliza, “Hii inahusianaje na mambo yangu ya shughuli/biashara kwa maisha yangu ya baadae? Jibu ni hili, ina mambo yote yahusuyo maisha yako ya shughuli kwa ajili ya maisha yako! Kama wewe huna mahusiano mazuri na Mungu, kama huna tabia nzuri kwa Mungu, kama wewe hutembei katika ushirika mzuri na Mungu na kukabidhi maisha yako mara zote kwake, basi kwa vyovyote utapoteza mapenzi yake katika maisha yako! Au umetengeneza maisha yako yenye mafanikio ya baadae iwe sanamu katika maisha yako?

Wakristo wengi hufundisha mambo haya pasipo hata aibu yoyote, kama vile,

“Unatakiwa ugundue kusudi lako katika maisha yako! Unapaswa kutimiliza hatma yako katika maisha yako. Kama hujui kusudi lako je, utawezaje kutimiliza hatma yako!”

Huo ni ujinga mtupu! Wakristo wanakengeuka na kisha kuongea maneno kana kwamba Biblia haipo na wala Mungu hayupo! Hatma yetu hapa duniani na umilele imeshakuwa wazi kabisa kutoka katika sura ya kwanza ya Biblia, pale ambapo Mungu anasema, “Tumfanye mtu kwa mfano wetu”! Kusudio la Mungu la umilele kwa ajili yako na mimi ni kufananishwa naye, kung”aa kwa mfano wake, “Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi.” (Warumi 8:29, soma pia 2 Wakoritho 3:18). Tunatakiwa kufanana na Kristo hapa duniani na umilele! Hiyo ndiyo hatma yetu! Sasa watu wanawezaje kupuuzia wito huu mkuu wa Mungu katika maisha yetu na kisha kupunguza na kuchafua maana yake na kisha kutumbukiza elimu ya muda tu au biashara/shughuli tunayopaswa kuwa nayo hapa duniani? Hatma yangu hapa duniani siyo kuwa mwalimu, daktari, mwenye biashara, mkulima, mekanika au kadhalika! Hatma yangu ni ‘nipate kuwa mshirika wa tabia ya Uungu,’ (2 Petro 1:4) na ‘kuenenda vile vile kama Yesu alivyoenenda’ (1 Yoh.2:6), haijalishi nikiwa mwalimu, daktari, mwenye biashara, mkulima au mekanika!

Siku ile tutakaposimama mbele ya Mungu, ujasiri wetu utakuwa nini? Je, kusema, “nilitimiza ndoto yangu, hatma yangu, nilifanikiwa”? Au je, kusimama mbele ya Bwana kama ‘daktari’ au ‘mwenye biashara’? Hapana! Bali tutakuwa na ‘ujasiri katika siku ya hukumu, kwa kuwa, kama Yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu!’ (1Yohana 4:17). Ndiyo, ni nzuri kuwa na kazi fulani, kabisa. Lakini siku hizi wengi wanajishughulisha na mambo ya dunia hii kupita kiasi kabisa kuliko mambo ya kiroho. Wanapata hasara kubwa sana katika maisha ya kiroho yao kwa sababu wanayo hamu sana ‘kufanikiwa’ tu duniani hii.

Kusudi la Uzima wa Milele ni nini? Yesu Kristo mwenyewe anatupatia jibu la wazi kabisa katika Yohana 17:3, pale ambapo anasema, “Na uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” Kusudi letu katika nyakati na umilele ni kumjua Baba na Yesu Kristo! Shetani alitaka kuteketeza kusudi la Mungu kwa ajili ya Adamu na Hawa hapa duniani, na aliwashawishi kwa kuwanukulia jambo jingine ambalo lilikuwa la kweli (lakini kwa sehemu tu!). Na shetani anataka kufanya kwetu sisi mambo yaleyale aliyoyafanya kwa Adam na Hawa. Aliwambia kama yafuatavyo, “amini maneno yangu na utakuwa…”, naye aliwaahidi mambo makubwa sana! Na inaonekana siku hizi watu wengi wametekwa nyara na ‘ahadi’ zake kupitia mafundisho ya nguvu ya fikra chanya! Na kuna wahubiri nyakati za leo ambao wanafanya mambo haya vilevile. Wao hufundisha mafundisho ambayo mkazo wake ni nafsi zetu tu – kupitia kuhubiri kwa ‘fikra chanya’ na ‘mafanikio’ – na wanawavuta na kuwashawishi watu kwa kunukuu (na kupotosha!) mistari ya neno la Mungu michache ili kuunga mkono udanganyifu wao. Kuhubiri kwa ‘nguvu ya fikra chanya’ (the power of positive thinking) kunawakilisha ‘injili nyingine’ ambayo inaweka unachotaka wewe mwenyewe kiwe kitovu cha maisha yako!

Mungu anao uwezo mzuri wa kuchambua mambo na kuyaelekeza maisha katika njia alizozichagua kuhusiana na kazi yoyote ya matukio ya maisha yangu ya baadae, ambayo nitahusika nayo. Kama ninayaweka matumaini yangu kwa Yesu, na kukabidhi kila hatua ya maisha yangu ninayoyafanya kwake, ndipo yeye anakuwa na uwezo mzuri wa kuniongoza mimi kwenye kazi au elimu ambayo anapenda mimi niifanye na kunibariki pia! Lakini kazi yangu, elimu yangu au hata biashara yangu hivyo vyote sio kusudi la maisha yangu wala sio hatma yangu ya kesho. Kristo pekee ndiye hatma yangu – katika maisha haya na umilele! Kufanana naye, na kudhihirisha maisha yake hapa duniani katika kila jambo ambalo nalifanya – hilo ndilo kusudi langu na hatma yangu! Wakristo nyakati hizi wanageukia kwenye filosofia za kidunia, kwenye mafundisho ya kidunia tu, mambo ambayo yanawapora wakristo wengi sio tu lile kusudi la Mungu la umilele kwa ajili yao, bali hata yale mapenzi ya Mungu kwa ajili yao hapa duniani nayo yanaporwa na mafundisho haya ya wajanja. Wanajaza mioyo ya watu na vichwa vyao kwa mawazo ya fundisho la nguvu ya kufikiri chanya ambayo mkazo wake unaelekeza kwenye juhudi na nguvu yao, maamuzi yao na mtazamo wao tu kuliko kuweka mkazo kwa Mungu, na kuyakabidhi maisha yao kwake Mungu na kila hatua tunayochukua tukimruhusu yeye kuthibitisha mapenzi yake katika maisha yetu.

Ebu tu niseme kwamba, iwapo itatokea mmoja hajanielewa vizuri, mbadala wa kuwa na kile wanachokiita kuwa ni “kufikiri chanya”, sio kuwa hasi, kukata tamaa, kujisikia huna maana na hufai, au kujichukia mwenyewe! Kwa sababu hiyo nayo ni kazi ya shetani pia! Bali sasa mbadala wake ni kuweka matumaini yetu na mategemeo yetu yote kwa Yesu Kristo – Yeye aliyetupenda na akajitoa maisha yake kwa ajili yetu ili kwamba tuwe na uzima na kuwa nao tele. Mungu anafanya njia kwa ajili yetu kupitia mambo ambayo hayawezekeniki kabisa.(Isaya 43:1-3,16). Mistari ya neno la Mungu ambayo inatuhamasisha na kututia moyo ili kuyaweka matumaini yetu kwa Mungu ni mingi mno kuiorozesha hapa pasingetosha! Kama unapenda kufikiri kwako kuwe katika mifumo chanya kwa maana halisia ya kiBiblia, ndipo unachotakiwa kukifanya ni hiki, weka matumaini yako yote kwa Mungu aliye hai.

Hicho ndicho alichokifanya mtume Paulo, na ndio sababu aliweza kusema katika wafilipi 4:13, “Nayaweza yote katika Kristo anitiaye nguvu.” Sasa hili neno “mambo yote” ni kitu gani ambacho mtume Paulo anakitaja hapa? Hivi ndivyo asemavyo Paulo, “Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa.” Paulo alijiaanda na kuridhika na hali yoyote ile inayoweza kumtokea mbele yake, na aliweza tu kumudu kuyafanya mambo hayo yote kupitia Yesu Kristo. Watu wengi hawatapenda mambo kama haya kwa sababu kuyaweka matumaini yako kwa Yesu mara zote haiongozi mtu kuelekea kwenye yale anayoyataka kuyafikiria kuwa ni mafanikio, au kuwa mwenye mafanikio. Na hapa tunayo sababu ya lazima kabisa inayotujulisha kwa nini watu wa aina hii wanalipatia neno la Mungu migongo yao, na kisha kukumbatia fundisho hili la nguvu ya kufikiri chanya, ambayo kwa ujumla haimkumbuki Mungu wala Kristo Yesu.

Mambo wanayopenda kuyakazia kuyasema ni kama vile, “Badilisha mtazamo wako tu, na kisha utapata mafanikio! Usikate tamaa! Jipe ujasiri mwenyewe nawe utafanikiwa!” Nyingi ya maelezo yao hayaelekezi wala hayamrejei Mungu na Kristo Yesu. Kwa sababu shabaha yao moja kubwa si Kristo bali ni kupata mafanikio katika biashara zao au elimu! Na hawa wahubiri wa uongo kwa urahisi tu wanalichafua neno la Mungu na ndipo utagundua upumbavu mtupu unatumwa kwenye facebook na tovuti ya kijamii. Tunaweza kusema kwa mfano baadhi ya mambo ya uongo wanayoyatuma kwenye facebook ni kama iufuatavyo, “Mungu anakuamini wewe, kwa hiyo na wewe jiamini mwenyewe!” Mungu ananiamini? Wanapata wapi jambo hili jamani? Kwa nini sasa waumini wanameza sumu kali kama hii? Mungu anatupenda na amekwisha kutupatia mambo makuu yenye thamani kuu kwa kutaja tu ni mwanae Yesu Kristo, kwa sababu maisha yetu yalishapotea katika dhambi na giza, ili kwamba sasa tuyaweke matumaini yetu kwake yeye ambaye ni pekee ambaye ndiye mwenye thamani!

Hii ndio sababu Paulo anasema katika wafilipi 3:3, “Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili.” Hii ndiyo viashiria vya ukristo wa kweli tulio nao. Shida za maisha zipo ili kutufundisha jambo moja, yaani, “tusijitumainie sisi wenyewe bali tumtumainie Mungu ambaye anafufua wafu.” (2 Wakor. 1:9).

Tafadhali ebu nieleweke vizuri hapa, tatizo sio uwezo tulionao, wala sio kuwa kama tunautumia uwezo tulio nao au hapana, bali ni jambo ambalo linatupasa tujue ni wapi tunawekeza matumaini yetu. Unaona, uchaguzi hapa si kuwa na matumini au kutokuwa na matumaini, hapana; bali kuyaweka matumaini yetu kwa Mungu.

Kumjia Mungu kuhusiana na mambo kama haya ili tupate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu, inamaanisha kuwa kuna nyakati ambazo tutakuta kwamba mapenzi yake yako tofauti na kile kilichomo katika mioyo yetu! Na kama tutaishi mbele zake kama dhabihu iliyo hai, ndipo basi tunapaswa kujiandaa kwa jambo kama hili.

Miaka mingi iliyopita nilitamani sana kuchukua jambo fulani katika maisha yangu. Lakini kadiri nilivyoendelea kusubiria mbele za Mungu ndivyo ilivyo dhihirika wazi kabisa kuwa hiyo haikuwa njia ambayo Mungu alitaka mimi niiendee! Mara zote Mungu huthibitisha mapenzi yake kwa kutupatia amani anayotuwekea mioyoni mwetu. Au kwa kutukosesha amani kabisa. Nami sikuwa na amani kabisa ya kuchukua hatua kwa uchaguzi ule nilioutamani – na ingalikuwa hatua ya maana sana katika maisha yangu! Ninamshukuru Mungu sana leo kwamba sikuchukua hatua yoyote wakati ule juu ya kile nilichokitaka mimi, ambayo kwa leo nikitazama nyakati zangu za nyuma naona wazi kuwa ingekuwa ni majanga au ni maafa makubwa kwangu! Mungu tuliye naye ni wa ajabu ya namna gani! Yeye anayetujali sana na kwamba ndiye anayetuongoza kwenye maamuzi muhimu yahusuyo maisha yetu! Lakini hii inawezekana tu iwapo tutaikabidhi miili yetu pamoja na maisha yetu kwake kama dhabihu iliyo hai. Na kuyaweka mategemeo yetu yote kwake! Ninatumaini kwamba maneno haya machache yatakutieni moyo ili kuweka matumaini yenu kwake yeye tu!

© David Stamen 2016   somabiblia.com

 

Comments are closed.