RSS

Je, naweza kujua mapenzi ya Mungu kwa maisha yangu?

Tunaweza kumshukuru Mung kwani Yeye hajaficha mapenzi Yake juu yetu! Paulo anasema,

“Maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, KUTAKASWA KWENU, mwepukane na uasherati.” (1 Wathes.4:3).

Je, unataka kufanikiwa, unapenda kutimiza ndoto yako au lengo lako? Lakini haya yote hayana maana, ni bure tu kama ukianguka kwenye dhambi ya uzinzi, au dhambi nyingine ya siri? Siku hizi, wengi wanajitahidi sana wafanikiwe. Je, unajitahidi kufanakiwa katika kutakaswa kwako? Je, inawezekana wengi hawajajali mapenzi ya Mungu ya dhati katika maisha yao siku hizi ili waweze kuifuate ndoto zao tu, wakidai ‘ndoto’ zao ni ‘mapenzi ya Mungu’? Mambo mengine yote katika maisha yetu ni BURE tu kama tukifuata anasa ya mwili, kuona mambo machafu kwenye mtandao au kujiunga na facebook group ya picha za ngono.Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, KUTAKASWA KWENU, kuishi maisha ya UTAKATIFU kwa MOYO SAFI!  

Tuendeleeni! Paulo anafundisha kwamba, “FURAHINI siku zote; OMBENI bila kukoma; SHUKURUNI kwa kila jambo; maana HAYO NI MAPENZI YA MUNGU kwenu katika Kristo Yesu.” (1 Wathes.5:18).

Mapenzi ya Mungu kwa maisha yangu ni nini? Hayo ni mapenzi ya mungu kwangu! Tunaweza kumshukuru Mungu sana kwani alidhihirisha mapenzi yake kwa ajili ya masiha yetu kwa wazi! Kabla ya mambo mengine yote, Mungu amedhihirisha mapenzi yake juu maisha yangu na maisha yako ni tufurahi siku zote, tuombe bila kukoma na kumshukuru katika kila jambo! Kwa hiyo, usizunguke zunguke, usitafute tafute ukijiuliza ‘mapenzi ya Mungu katika maisha yangu ni nini?’, ila ‘pokea kwa upole neno lile lililopandwa ndani, liwezalo kuziokoa roho yako’. (Yakobo 1:21).

Je, naweza kujua MWITO wa Mungu kwa maisha yangu? Ndiyo, naweza! Paulo anatujulisha kwamba, “Mungu…alituokoa akatuita kwa MWITO MTAKATIFU si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake.” (2 Tim.1:9). Na Petro anathibitisha ukweli huo, “…kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi IWENI WATAKATIFU KATIKA MWENENDO WENU WOTE…” (1 Petro 1:15).

Paulo anatusihi, “mwenende kama inavyoustahili WITO WENU MLIOITIWA; kwa UNYENYEKEVU wote na UPOLE, kwa UVUMILIVU, mkichukuliana katika UPENDO;” (Waefeso 4:1,2)! Siku hizi wengi wanatafuta waitalo ‘kusudi’ la maisha yao wakati hawajali MWITO WA MUNGU ambao tayari ameshaudhihirisha kwetu kupitia neno lake! Je, tunafurahia zaidi kufuata ‘kusudi letu’ na kutimiza ‘ndoto yetu’ kuliko kufuata na kuishi sawasawa na neno la Mungu na kutumiza mwito wetu unaotokana moja kwa moja na Mungu?

Katika Waebrania tunaambiwa jambo la ajabu juu ya mwito wetu, “Kwa hiyo, ndugu watakatifu, wenye kuushiriki MWITO WA MBINGUNI, mtafakarini sana…Yesu.” (3:1). Hii ni neema kubwa sana kwetu; tumeitwa na mwito wa mbinguni, tuwe kama Yesu Kristo ulimwenguni humu! Sawasawa na mafundisho ya Yohana, “…kama Yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu.” (1 Yoh.4:17). Na Paulo anaeleza ukweli mkuu sana, “Kwa maana sisi tu MANUKATO YA KRISTO, mbele za MUNGU, katika wao wanaookolewa, na katika wao wanaopotea; katika hao wa pili harufu ya mauti iletayo mauti; katika hao wa kwanza harufu ya uzima iletayo uzima.” (2 Wakor.2:15,16). Huo ndio mwito mkuu, siyo ndiyo? Je, tunautafuta mwito kuu kuliko huo? Kama ni hivyo, labda Mungu ataongea nasi kama vile alivyoongea na Baruku aliposema, “Je! Unajitafutia mambo makuu? Usiyatafute!” (Jer.45:5).

Sisi tumeitwa tuwe HARUFU YA KRISTO mbele za Mungu KWANZA na KWA KIMSINGI. Tunaishi mbele ya Mungu kwanza, siyo mbele ya watu. Bila kuwa harufu ya Kristo MBELE YA MUNGU, hatuwezi kuwa baraka kweli kweli kwao wengine! Kama ilivyoandikwa katika Kitabu cha Kutoka sura ya 29, Mungu aliwaagiza makuhani watoe, “wana-kondoo wa mwaka mmoja wawili SIKU BAADA YA SIKU DAIMA. Mwana-kondoo mmoja utamchinja asubuhi; na mwana-kondoo wa pili utamchinja jioni …IWE HARUFU NZURI,… Itakuwa ni sadaka ya kuteketezwa MILELE…MBELE YA BWANA. HAPO NITAKAPOKUTANA NANYI, ili ninene na wewe HAPO.” (29:38-42). Kumbe, Mungu Baba yetu anakutana nasi mahali pa madhabahu ya dhabihu naye anatazamia tutoe maisha yetu yawe harufu ya Yesu Kristo mbele Yake, ‘asubuhi na jioni’, yaani, wakati wote! Yesu Kristo ni Mwana-Kondoo wa Mungu! Na mahali pale pale pa sadaka anatutakasa ili tumtimikie tulipo. (“…nitaitakasa…hiyo madhabahu; pia Haruni na wanawe NITAWATAKASA, ILI WANITUMIKIE katika kazi ya ukuhani.” 29:44). Jambo la ajabu! Kwa hiyo Paulo anasema, “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, ITOENI MIILI YENU IWE DHABIHU ILIYO HAI, TAKATIFU, YA KUMPENDEZA Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, MPATE KUJUA HAKIKA MAPENZI YA MUNGU aliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.” (War.12:1,2).

Basi, usijisumbue kwa ajili ya mapenzi ya Mungu mawazoni mwako. Kwa kimsingi sasa unaijua njia. Njia ni Yesu Kristo. Fanya kama Paulo alivyofanya; uwe na fikra ya Paulo aliyesema,

“Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila NATENDA NENO MOJA TU; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; NAKAZA MWENDO, NIIFIKILIE mede ya THAWABU YA MWITO MKUU wa Mungu katika Kristo Yesu. Basi…na tuwaze hayo.” (Wafilipi3:13,14).

Lile usilolijua, subiri tu mbele Yake, na kwa wakati wake utalijua. Yatoe maisha yako yawe dhabihu iliyo hai, yawe harufu ya Kristo mbele Yake kila siku, bila kuitafuta njia yako mwenyewe, na neno la Mungu linatuambia utapata kujua hakika mapenzi ya Mungu, hatua kwa hatua na kwa wakati wake! Na kumbuka Paulo alilosema katika mstari unaofuata, yaani, “Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu ASINIE MAKUU KUPITA ILIVYOMPASA KUNAI.”  Mungu akubariki!

 

© David Stamen 2014                       somabiblia.com

Kupakua somo hili bonyeza link: mapenzi-ya-mungu-kwa-maisha-yangu-ni-nini

RUDI KWA HOMEPAGE

 

One response to “Je, naweza kujua mapenzi ya Mungu kwa maisha yangu?

  1. Pingback: somabiblia

Leave a Reply