RSS

MWENYE HAKI AU MWENYE DHAMBI?

Katika Matendo ya Mitume na Nyaraka zote za Mitume, Wakrsito huitwa “watakatifu” kama mara hamsini – ni jina la kawaida kwa waumini katika Agano Jipya! Kwa mfano, “kwa watakatifu walioko Efeso wanaomwamini Kristo Yesu.” (Waefeso 1:1). Hamna mstari mmoja katika Agano Jipya ambapo Wakristo wameitwa ‘wenye dhambi’! Kama wewe ni mwenye dhambi, sikiliza neno la Mungu juu ya watu hao,

“Lakini ikiwa sisi wenyewe, kwa kutafuta kuhesabiwa haki katika Kristo, tulionekana kuwa wenye dhambi, je! Kristo amekuwa mtumishi wa dhambi? Hasha! Maana nikiyajenga tena yale niliyoyabomoa, naonyesha ya kuwa mimi mwenyewe ni mkosaji.” (Wagal.2:17,18).

Kupitia toba kweli kweli na kuzaliwa kutoka juu, maisha ya dhambi yamebomolewa, sasa je, inakuwaje nijenge tena matendo ya makosa, isipokuwa ninajifanya mwenye dhambi tena? Paulo anasema siyo kazi ya Kristo kutufanya tuwe wenye dhambi! Hasha! Kwa hiyo, wao waliookoka kweli kweli waliacha kuishi kama wenye dhambi; waliacha kutumikia dhambi kwa sababu ya kazi ile Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, aliyoitimizwa msalabani! Kama mtume Paulo anasisitiza, “Mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena.” (Warumi 6:6). Sasa, Neno la Mungu linaongea nasi likisema, ‘MKIJUA neno hili…’. Sasa je, wewe unajua ‘neno hili’? Labda unajua kunukulu mistari nyingine. Sawa. Lakini unajua wewe ukweli wa ‘neno hili’ Paulo alilolitangaza kwenye mstari huo? Unajua kwamba ‘utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili tusitumikie dhambi tena.’? Paulo ananedelea kwa kutuambia, “Na mlipokwisha kuwekwa huru mbali na dhambi, mkawa WATUMWA WA HAKI.” (Warumi 6:18).

Neno la Mungu hutufundisha wazi kabisa kuwa kama vile wote walivyofanywa kuwa wenye dhambi kutokana na dhambi ya Adamu, vivyo hivyo wengi wamefanywa wenye haki kutokana na kutii kwa  Yesu msalabani,

“Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya WENYE HAKI.” (Warumi 5:19). Na tena, “Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi TUPATE KUWA HAKI YA MUNGU katika Yeye.” (2 Wakor.5:21).

Pasipo mabadiliko hayo katika maisha yangu, hamna Ukristo! Ni dini tu.

Unataka kunukulu Warumi sura ya 7? Sawa. Lakini zaidi ya hayo, je unajua ukweli wa Warumi 8:2 katika maisha yako?  “Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti.” Je, unapenda sana kunukulu 1 Yohana 1:8,10? Kwa nini? Je, unapenda kudumu katika dhambi? Kama unapenda kunukulu 1 Yohana 1, je, unakubali na Yohana anaposema, “Kila mtu ALIYEZALIWA NA MUNGU hatendi dhambi, kwa sababu UZAO WAKE wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu AMEZALIWA KUTOKANA NA MUNGU.” (1 Yoh.3:9). Je, jambo hili limetokea katika maisha yako? Unafurahia ukweli huo wa wokovu wetu? Au unapendelea kunukulu Yohana 1:10 tu, kwa sababu unafikiri inathibitisha hali yako  ya kutenda dhambi au inakupa kisingizio kwa ajili ya dhambi zako? Yohana anatuonya, “Watoto wadogo, mtu na asiwadanganye; atendaye haki yuna haki, kama yeye alivyo na haki; atendaye dhambi ni wa Ibilisi.” (1 Yoh.3:7,8).

Kama tukipenda kunukulu Biblia, tunapaswa kupokea “habari ya kusudi lote la Mungu” (Matendo 20:27), na siyo kuitaja mistari zile tuzipendeleazo kwa sababu tunafikiri zinatuletea faraja katika hali yenu ya kutenda dhambi. Wokovu wa Bwana Yesu Kristo ni mkuu mno!

“Kwa kuwa uweza Wake WA UUNGU umetukirimia vitu vyote vipasavyo UZIMA NA UTAUWA… Kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa WASHIRIKA WA TABIA YA UUNGU…”. (2 Petro 1:3,4).

Na tena katika Waebrania, “…hao (baba zetu) kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali Yeye (Mungu Baba) kwa faida yetu, ILI TUUSHIRIKI UTAKATIFU wake.” (12:10).

Tusicheze na mambo haya. Kwa sababu ya ‘dini’ watu wengi siku hizi wanapotea. Kuwa mkristo ina maana maisha yangu yamebadilika kabisa kwa ndani na niliacha kuitumikia dhambi. Labda unafikiri Paulo anajiita ‘mwenye dhambi’ katika 1 Timotheo 1:15, “Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi.” Ndiyo, Yesu alikuja kumwokoa Paulo. Kwa nini alisema ‘ambao wa kwanza wao ni mimi’? – ni kwa sababu ya mistari kabla ya mstari 15 ambapo anasema, “hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri” (m.13). Paulo alikuwa mwenye kuliudhi Kanisa la Bwana, kwa hiyo alisema alikuwa ‘wa kwanza’ kwa wenye dhambi – inahusu maisha yake kabla ya hajaokoka, kama vile mstari wa 16 unavyotuonyesha, “Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.” Kumbe! Maisha ya Paulo yamebadilishwa kabisa kwa sababu ya neema na rehema ya Mungu! Kama unataka kulinganisha na Paulo na kudai wewe ni ‘kwanza wa wenye dhambi’, ni sawa – kwa masharti ya kudai pia sasa maisha yako ni kielelezo kwa wale waoamini!

Biblia haongei dhidi ya Biblia! Hamna mabishano katika Biblia. Kama ukisisitiza wewe ni mwenye dhambi, ujue sawasawa na neno la Mungu hutaokoka siku ile,

“Kwa maana wakati umefika wa hukumu kuanza katika nyumba ya Mungu; na ikianza kwetu sisi, mwisho wao wasioitii injili ya Mungu utakuwaje? Na mwenye haki akiokoka kwa shida, yule asiyemcha Mungu na MWENYE DHAMBI ATAONEKANA WAPI?” (1 Petro 4:17,18).

Basi kama wewe ni mwenye dhambi, utaonekana wapi?

“Tuseme nini basi? Tudumu katika dhambi ili neema izidi kuwa nyingi? Hasha! Sisi tulioifia dhambi tutaishije tena katika dhambi? (Warumi 6:1,2). Je, wewe unasema nini?

 David Stamen 2015         somabiblia.com        

KUPAKUA SOMO HILI BONYEZA LINK: WENYE HAKI AU WENYE DHAMBI

KUSOMA ZAIDI BONYEZA LINKS ZIFUATZAO:

https://somabiblia.wordpress.com/uzima-wa-milele-ni-nini-injili-ni-nini/

https://somabiblia.wordpress.com/siku-ile-ni-siku-ya-nini-yohana-1420/

RUDI KWA HOMEPAGE

 

3 responses to “MWENYE HAKI AU MWENYE DHAMBI?

  1. STEVEN

    May 18, 2017 at 2:59 pm

    GOD IS GOOD ALL THE TIME, All of us believe on GOD

     
  2. Mwangomo N

    September 13, 2019 at 4:15 am

    Mimi ni mwenyehaki

     
  3. Anonymous

    April 4, 2024 at 10:15 am

    Mimi nimehesabiwa kuwa mwenye haki

     

Leave a Reply